Padre Baptiste Mapunda (M.Afr)
Tunapouanza mwaka 2015 tujue kwamba huu ni mwaka wa Uchaguzi Mkuu kwa wabunge, madiwani pamoja na rais.
Kisiasa ni mwaka wa kihistoria kwa sababu Katiba
Inayopendekezwa inapaswa kupigiwa kura ya “Ndiyo” au “Hapana” mwezi
Aprili 2015 kama Serikali haitabadili mwelekeo wake. Mimi ni kama nilivoandika kwamba kura yangu kwa Katiba hiyo ninayoiita ya CCM ni “hapana, hapana, hapana”.
Nitapiga kura ya “Hapana” na kuwashawishi
Watanzania wanaopenda mabadiliko na maendeleo kuungana nami kwa sababu
katiba hii iliyopendekezwa kwa mabavu ya bunduki na mabomu ya dola,
haina masilahi kwa wananchi wa kawaida. Katiba hii inayopendekezwa, ina kazi moja tu; kulinda ufisadi na mali za kikundi cha watu wa chache ndani ya Serikali ya CCM.
Wewe mwananchi wa kawaida ambaye huna manufaa nayo, utaipigia kura ya kuipitisha ili iweje?
Maoni ya Tume ya Marekebisho ya Katiba iliyokuwa
chini ya Jaji Joseph Warioba yalipendekeza kuwapo kwa “TUME HURU YA
UCHAGUZI” ambayo inakidhi mahitaji ya siasa za vyama vingi na sio chama
tawala tu cha CCM.
Swali langu ni je, Serikali ya CCM itakubali
kuunda Tume Huru ya Uchaguzi, wakati ikijua kwamba ushindi wake katika
chaguzi unategemea sana tume hii ya sasa ya CCM chini ya mamlaka ya Rais
ambaye ni mwenyekiti wa CCM?
Nathubutu kuandika kwamba, sasa Watanzania
wenzangu kazi ni moja tu, yaani kudai kuundwa kwa TUME HURU YA UCHAGUZI”
kama ilivyokusudiwa na wananchi kwenye Rasimu ya Katiba. Chombo hiki ni cha kitaifa si cha chama kimoja.
Kwa hivyo wananchi wote bila kujali chama, dini, kabila, cheo, ukanda
unakotoka wala rangi, tuungane kudai ili iundwe haraka na kushughulikia
masuala yote ya uchaguzi kwa haki, uhuru, uwazi na usawa kwa vyama vyote
na kuondokana na malalamiko ya miaka mingi.
Tume hii huru itaratibu sheria na kanuni za
uchaguzi, kusimamia uchaguzi wenyewe, kushughulikia kesi na kero pamoja
na kuwatangaza washindi wa kweli mwisho wa uchaguzi.
Tume hiyo itashughulika na uboreshwaji wa daftari la wapiga kura nchini Tanzania.Masuala haya mawili yaani Tume Huru ya Uchaguzi na uandikishwaji
majina ya wananchi kwenye darftari la Wapigakura ni mambo muhumu sana
katika ukuaji, ukomavu wa demokrasia na utawala bora nchini. Wapinzani mkirogwa kuingia kichwa kichwa katika
Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu bila ya TUME HURU YA UCHAGUZI, basi mjue
itakuwa “imekula kwenu”.
Ushindi wa CCM unategemea tume ya sasa ambayo mimi
binafsi naiona kuwa ni poliCCM ambayo imejaa rushwa, fitina, wizi wa
kura, uchakachuaji, upendeleo na vurugu. Mimi kama mchezaji mpira wa miguu katika jamii
hasa nikiwa katika shule na vyuo mbalimbali, mara nyingi tulikuwa
tunakataa timu yetu kushiriki katika mchezo ambao kanuni zilikuwa za
upendeleo. Ni mtu mjinga pekee, tena mwenye ‘umaskini wa
akili’ ndiyo atakubali kushiriki katika shughuli ya pamoja ambayo
inaendeshwa bila sheria na kanuni na pengine hata upendeleo mkubwa.
Wapinzani chondechonde nawasihi anzeni kudai
uundaji wa katiba mpya mwanzoni mwa mwaka huu, kuishinikiza Serikali
kwani hilo ni la msingi kuliko hata kufanya kampeni za uchaguzi.
Usalama wa kura zenu na ushindi upo mikononi mwa
“TUME HURU YA UCHAGUZI” na siyo tume ya sasa ambayo ipo chini ya mamlaka
ya Rais ambaye ni mwenyekiti wa CCM la hasha. Madai ya TUME HURU YA UCHAGUZI siyo ya wapinzani
tu bali ya Watanzania wote wenye kupenda haki, uhuru katika chaguzi zetu
pamoja na maendeleo ya demokrasia na utawala bora. Viongozi wa
madhehebu ya dini yote na waumini wao ni wadau wa demokrasia
inayostawisha amani na uhuru wa kuabudu, hivyo ni vyema washiriki
kikamilifu katika madai hayo ya msingi wa demokrasia.
Wanaharakati, vyama vya wafanyakazi, wakulima na
wafugaji nao pia ni waathirika wa tume hii ya sasa. Wanafunzi wa vyuo
vikuu pamoja na vijana wote ambao wanapaswa kujiandikisha na kupigia
kura, basi nao washiriki harakati za kudai TUME HURU YA UCHAGUZI badala
ya kungoja kuhongwa ili kuwavusha wanasiasa wanaotumia “umaskini wa
akili’ kuwahadaa kwa ahadi hewa mfano uundwaji wa baraza la vijana.
Jinsi uchaguzi wa viongozi wa serikali za mitaa
uliofanyika Desemba mwaka jana na kuvurugwa kwa makusudi; ulivyojaa
mizengwe, fitina, chuki, vitisho, majeruhi, utekaji, mauaji, wizi wa
kura na maovu mengine ni alama tosha kwamba “ sasa TUME HURU YA
UCHAGUZI” haiepukiki ni muda mwafaka iundwe hata kama ni kesho.
Kama CCM wana ujasiri wa kubadilisha matokeo,
kuongeza kura na vituko vingine vikafanyika mbele ya hadhara, itakuwaje
kama kura zitahesabiwa na kujumlishwa na Tume ya sasa chini ya mamlaka
ya Rais?
Maana yake ni kwamba wananchi wataendelea kupigia
kura lakini mabadiliko hawatayaona na hii ndiyo sababu ya kule Kenya
mwaka 2007 hawakuwa na njia nyingine isipokuwa akina Raila Odinga
kukataa kata kata kuyatambua matokeo na ushindi wa Kibaki na hatimaye
vurugu zukatokea na kuzaa maafa ya zaidi ya watu elfu moja. Usipotenda haki, usitegemee kupata amani, labda amani ya bunduki kama hii inayohubiriwa na Serikali ya CCM hapa nchini. La mgambo limepigwa enyi Watanzania amkeni
tuungane pamoja bila kujali tofauti zetu. Tudai uundwaji wa TUME HURU YA
UCHAGUZI kwa maendeleo ya demokrasia na utawala bora nchini. Ndiyo kwa maana nathubutu kuandika kwa uwazi na uhuru kwamba “ sasa kazi ni moja tu; kudai TUME HURU YA UCHAGUZI”.
hakuna kulala mpaka kieleweke.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment