Social Icons

Pages

Friday, December 19, 2014

SHEIN AZINDUA UMEME DONGONGWE

Rais wa Zanzibar na mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk Ali Mohamed Shein akizindua mradi wa umeme katika Kijiji cha Dongongwe, Mkoa wa Kusini Unguja.

Akihutubia katika uzinduzi huo, Dk Shein alisema Serikali ina wajibu wa kuwapa wananchi huduma bora za kijamii, kiuchumi na maendeleo wananchi. Akinukuu ibara ya 10 ya Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984, Dk Shein alisema: “Kwa madhumuni ya kuendeleza umoja na maendeleo ya watu na ustawi wa jamii katika nchi, itakuwa ni wajibu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kutoa huduma za kutosha kwa ajili ya kuendeleza watu.”
Alisema maendeleo ni mchakato na ni jambo ambalo halikamiliki kwa siku moja, badala yake huenda hatua kwa hatua, hivyo Serikali itaendelea kupeleka huduma nyingine zilizobaki kijijini humo, ikiwamo barabara akiahidi kuwa itajengwa hatua kwa hatua. Alisema maendeleo hayachagui mtu wala eneo analotoka, hivyo Serikali anayoiongoza itahakikisha inawapelekea maendeleo wananchi wote bila kujali itikadi zao kwani hilo ndilo jukumu la Serikali na pia ni malengo ya Mapinduzi ya Januari 12, 1964 ya Zanzibar .
Dk Shein alisema jitihada za kupeleka umeme vijijini ni kubwa kwa upande wa Unguja na Pemba na kusisitiza ingawa Zanzibar ni nchi ya mwanzo katika Afrika Mashariki kuwa na umeme toka mwaka 1875, lakini sio watu wote waliobahatika kuupata.
Akitoa historia ya huduma hiyo Zanzibar, Dk Shein alisema matumizi rasmi ya umeme kwa kisiwa cha Unguja yalianza mwaka 1908 na kwa kisiwa cha Pemba ni mwaka 1959 na kusema kuwa wananchi wengi walianza kupata huduma ya umeme baada ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, mwaka 1964. Dk Shein alisema hayo ndiyo yaliyoleta maendeleo ikiwamo kusambaza huduma za umeme kwa wananchi.
Aliongeza kuwa watawala wote walioitawala Zanzibar wakiwemo Wareno na Sultan kutoka Oman ambaye ametala zaidi ya miaka 100 hawakupeleka umeme katika kijiji hicho cha Dongoongwe lakini Serikali ya Mapinduzi Zanzibar chini ya Chama cha Mapinduzi kimepeleka huduma hiyo na nyenginezo. Alisema kuwa hatua kubwa za maendeleo hapa Zanzibar zimefanywa kutokana na Sera za ASP na sasa ni CCM chama ambacho kimekuwa kikitekeleza Sera na Ilani yake. Aidha, Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa pongezi na shukurani kwa shirika la umeme Zanzibar ZECO, Wizara husika pamoja na wananchi wa kijiji hicho na viongozi wao.
Katika sherehe hizo za uzinduzi Dk. Shein alitoa wito kwa wananchi wa Dongongwe kuitumia huduma hiyo ya umeme kama inavyotakiwa kwa lengo la kuwapatia maendeleo pamoja na huduma zao nyenginezo za kijamii. Dk. Shein katika Sherehe hizo za uzinduzi wa umeme kijijini hapo, alitoa vyeti maalum kwa viongozi wa Kamati za Umeme katika Jimbo hilo la Uzini huku sherehe hizo zikipambwa kwa tenzi na ngoma ya maubwa ambayo ilitoa burudani safi.
Nae Waziri wa Maji, Ujenzi, Nishati na Ardhi Mhe. Ramadhan Abdalla Shaaban alisema kuwa hayo yote ni Matunda ya Mapinduzi kwani bado yanaendelea na kusisitiza kuwa umeme si anasa ni kitu muhimu hivyo ni lazima kitumike hasa katika dunia ya leo ya sayansi na teknolojia.
Mapema Mkurugenzi wa Shirika la umeme Zanzibar ZECO Bwana Hassan.. alisema kuwa Sera ya Serikali ya Mapindyuzi ya Zanzibar ni kuhakikisha kuwa inawasogezea huduma za kijamii wananchi wake popote walipo na kazi hiyo ni endelevu hadi Serikali ihakikishe wananchi wote wanafikiwa na huduma zote muhimu ikiwemo umeme.
Alisema kuwa gharama zilizotumika katika kupelekea umeme kijijini hapo ni shilingi milioni 100,480,500.00 ambapo kati ya fedha hizo Shirika limechangia jumla ya shilingi milioni 85,480,500.00 na Mbunge wa Jimbo hilo amechangia shuilingi milioni 15,000,000.00. Alieleza kuwa kazi ziliyofanywa ni pamoja na ujenzi wa njia kubwa ya umeme ya mkondo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 2.7, uwekani wa vitop viwili vya transfoma zenye uwezo wa 100KVA kwa Ghana na 50 KVA kwa Dongongwe, ujenzi wa njia ndogo zenye urefu wa kilomita 2.5 pamoja na malipo ya fidia ya vipato shilingi milioni 18,614,7000.00 huku akiwataka wananchi wa kijiji cha Mkuku kujiandaa kupata huduma hiyo hivi karibuni.
Katika risala yao wananchi wa Dongongwe walisema kuwa wanakamilisha safari ndefu ya kusaka umeme na wanakuwa kijiji cha mwisho katika jimbo la Uzini kupata umeme na kutoa shukurani kwa Serikali, Shirika la Umeme, pamoja na viongozi wao wa Jimbo akiwemo Mbunge wa Jimbo hilo Mhe. Mohamed Seif Khatib.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: