Juzi, Rais Jakaya Kikwete alitangaza uamuzi wake
kuhusu sakata la uchotwaji wa fedha kwenye Akaunti ya Tegeta Escrow
ambayo ilifunguliwa kutunza fedha za malipo ya tozo ya uwekezaji kutoka
Shirika la Umeme (Tanesco) kwenda IPTL baada ya kutokea mzozo baina ya
pande hizo mbili.
IPTL iliingia mkataba wa kuiuzia umeme Tanesco
miaka 20 iliyopita. Lakini mkataba huo ukaingia dosari baada ya Tanesco
kufungua mashtaka mahakamani ikidai tozo hiyo ni kubwa, hali ambayo
ililazimisha pande hizo mbili kukubaliana kufungua akaunti maalumu ya
kutunza fedha hizo hadi suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.
Lakini suala hilo liliisha katika njia ambayo
ilizua shaka baada ya taarifa kuvuja kuwa fedha zilizokuwa kwenye
akaunti hiyo zilichotwa kinyemela na kwamba zimelipwa kwa watumishi wa
umma, viongozi wa kidini na watu wengine.
Shaka hiyo ndiyo iliyofanya Bunge lihoji na
kuamumuru uchunguzi ufanywe na Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za
Serikali (CAG) pamoja na Takukuru na baadaye Kamati ya Bunge ya Hesabu
za Serikali (PAC) ipitie ripoti hizo na kutoa taarifa bungeni. Baada ya
kuwasilisha taarifa yake, Bunge lilijadili na kufikia maazimio manane,
yakiwamo ambayo yalimtaka Rais atoe uamuzi kwa mujibu wa mamlaka yake.
Katika uamuzi wake, Rais Kikwete amemuondoa Waziri
wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, bado
anasubiri uchunguzi dhidi ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa
Sospeter Muhongo na katibu wake, Eliakimu Maswi, wakati Bodi ya Tanesco
iliyotakiwa ivunjwe kutokana na ushiriki wake kwenye sakata hilo,
imeshamaliza muda wake na hivyo kurahisisha kazi.
Hali kadhalika, suala la kumchukulia hatua
Mwanasheria Mkuu, lilishajitatua kutokana na Jaji Frederick Werema
kujiuzulu. Rais pia amekataa azimio la kutaifisha mitambo ya IPTL kwa
kuwa kitendo hicho kitawatisha wawekezaji wa nje, huku azimio la
kuimarisha Takukuru likiendelea kufanyiwa kazi.
Kiu ya wananchi ilikuwa ni kuona sakata hilo
linamalizwa kabisa, lakini wengi waliozungumza na vyombo vya habari juzi
na jana na kwenye mitandao ya kijamii baada ya hotuba ya Rais Kikwete,
wameonyesha kuwa mkuu huyo wa nchi hajakidhi kiu yao.
Wengi walitegemea kuwa angehutubia wakati akiwa na
uamuzi kamili kuhusu maazimio yanayomhusu moja kwa moja baada ya suala
hilo kuchukua muda mrefu na kutafuna fedha nyingi za walipa kodi kwa
njia moja au nyingine.
Baada ya kuwa na muda mwingi wa kutafakari tangu
Bunge lifikie maazimio hayo Novemba 29, ilitegemewa kuwa Rais angekuwa
na uamuzi kuhusu Profesa Muhongo kama ilivyokuwa kwa Profesa Tibaijuka,
katibu mkuu wa nishati, majaji, suala la uwazi wa mikataba na hata hatua
kwa ajili ya kudhibiti hali kama hiyo isitokee hapo baadaye.
Hatua za awali dhidi ya majaji zilitakiwa ziwe
zimeshachukuliwa kama kuwasimamisha wakati uchunguzi unaendelea kwa
mujibu wa Ibara ya 110 (A) (3).
Si nia yetu kumpangia Rais nini cha kufanya,
lakini kunapokuwa na kiu kubwa ya wananchi kujua hatima ya suala zito
kama hilo ambalo linahusu mabilioni ya fedha na lililoonekana kugubikwa
na ukiukwaji mkubwa wa maadili kwa viongozi wa juu, hatua ya Rais
kutangaza uamuzi, inatakiwa ifanywe wakati kukiwa na majibu ya maswali
mengi.
Kwa hali ilivyo sasa, fikra za wananchi ni kuwa
suala hilo ndiyo limeshamalizika kama masakata mengine yalivyoisha,
yakiwamo ya EPA na Richmond.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment