Pages

Thursday, October 29, 2015

MAALIM SEIF APINGA KUFUTWA MATOKEO

Mgombea urais wa Zanzibar wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amepinga uamuzi wa Tume ya Uchaguzi visiwani humo (Zec) kufuta matokeo ya uchaguzi na kwamba kuna njama za makusudi za kutaka kuvuruga demokrasia na kuingiza nchi katika machafuko kwa maslahi ya watu binafsi.
Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa jana, Maalim Seif alisema Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (Zec), Jecha Salim Jecha, hakutafakari kufuta Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar, kwani una athiri pia Uchaguzi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa sababu wapiga kura ni walewale waliomo katika Daftari la Wapigakura la Zec na kufanya kazi ya uwakala wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec).
Alisema hali hiyo inaitia Jamhuri ya Muungano katika taharuki bila ya sababu yoyote ya msingi.
Alisema Rais wa Jamuhuri ya Muungano hawezi kupatikana kwa kupigiwa kura na wananchi wa Tanzania Bara pekee, hivyo Cuf inaona uwamuzi huo umekuja baada ya majaribio yote ya kutaka kulazimisha ushindi usiokuwapo wa CCM kushindikana.
“Tumetambua zilikuwapo njama za kutaka kumtangaza mgombea urais wa CCM, Dk. Ali Mohammed Shein, kwa nguvu lakini njama hizo zimeshindikana kutokana na ukweli uliokuwa ukiibuka kupitia uhakiki wa matokeo ya uchaguzi,” alisema Seif.
Maalim Seif alidai CUF ndiyo mshindi wa uchaguzi wa urais wa Zanzibar pamoja na majimbo yote 18 ya Pemba na majimbo tisa ya Unguja na kuzitaka jumuiya za kimataifa kutoiruhusu CCM kukandamiza haki za kidemokrasia za wananchi wa Zanzibar kwa mara nyingine na kuwataka wananchi kubakia watulivu na kuitunza amani iliyopo.
“Tunatamka wazi CUF hatutambui uamuzi huo binafsi wa mwenyekiti wa tume na tunaitaka serikali na CCM kuiachia tume iendelee na kazi yake ya uhakiki wa matokeo ya uchaguzi na kisha kutangaza mshindi,” alisema.
Kwa upande wake, Mratibu wa Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa) Zanzibar, Mzuri Issa Ali, alisema uwamuzi wa Zec umetia doa kubwa katika historia ya Zanzibar na kuwataka viongozi wa vyama vya siasa pamoja na tume ya uchaguzi kukaa pamoja kutafuta muafaka kuepusha gharama za uchaguzi mpya kufanyika visiwani hapa.
“Tume ya Uchaguzi na wanasiasa wanatakiwa kukaa pamoja na kukubaliana kwa sababu sasa hivi huduma za kijamii Zanzibar zimesimama na suala la kurejea uchaguzi ni gharama kubwa,” alisema Mzuri.
Rais wa Chama cha Wanasheria Zanzibar (ZLS), Awadhi Ali Said, alisema uamuzi wa Mwenyekiti wa Zec umeingiza Zanzibar katika mgogoro wa kikatiba na Rais pamoja na mawaziri wake wakiendelea kubaki huku muda wao ukiwa umemalizika wa miaka mitano.
“Uamuzi wa tume umeingiza nchi katika mgogoro wa kikatiba kuhusu uhalali wa Rais kukaa madarakani wakati miaka mitano imepita na anatakiwa kuchaguliwa Rais mpya kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar,” alisema Awadhi.
Alisema kwamba kwa mujibu wa katiba ya Zanzibar baraza la wawakilishi linapovunjwa ndani ya siku 90 wajumbe wake wanatakiwa kuchaguliwa ili uwepo uwakilishi wa wananchi na baraza hilo lilivunjwa Agosti 13, mwaka huu.
Baadhi ya waangalizi wa uchaguzi huo wametofautiana na madai ya kasoro za uchaguzi zilizodaiwa kufanyika akiwamo muangalizi kutoka Jukwaa la Vijana Zanzibar (Zyf), Ali Khamis, ambaye alisema haikuwa muafaka matokeo ya uchaguzi huo kufutwa wakati kazi ya kupiga na kuhesabu kura ikiwa imefanyika na kukamilika katika majimbo.
Thabir  Shaabani muangalizi wa uchaguzi alisema maeneo mengi ya Unguja uchaguzi ulikwenda vizuri na sababu za kuahirisha uchaguzi zilizotolewa hazikuwa na hoja ya msingi na badala yake majimbo yenye matatizo kasoro zilihitaji kurekebishwa ili kuepusha hasara ya kurejea uchaguzi.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment