Pages

Wednesday, June 03, 2015

DENI LA MSD LAWAKERA WABUNGE

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid akiwasilisha bungeni makadirio ya mapato na matumizi ya wizara yake kwa mwaka 2015 / 2016, Dodoma jana.
Wabunge wa Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii na wa Kambi ya Upinzani Bungeni, wameitaka Serikali kulipa deni la Sh125 bilioni ambalo Bohari Kuu ya Dawa (MSD) inadaiwa na pia kuilipa Hospitali ya Apollo ya nchini India.
Wamesema kitendo cha Serikali kushindwa kuongeza bajeti katika sekta ya afya hadi kufikia asilimia 15 ya bajeti yake yote, ni kukiuka Azimio la Abuja linalozitaka nchi wanachama kutekeleza suala hilo ifikapo mwaka 2015.
Kamati hiyo pia ilieleza matatizo mbalimbali yanayoikabili sekta hiyo ikiwa ni pamoja na upungufu wa watumishi, gharama kubwa za matibabu ya saratani, kutotekelezwa kwa mpango wa bima kwa wote na huduma kwa watu wenye ulemavu wa ngozi.
Akiwasilisha taarifa ya kamati jana kuhusu utekelezaji wa bajeti ya Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii mwaka 2015/16, mjumbe wa kamati hiyo, Martha Umbulla alisema deni la Hospitali ya Apollo linalotokana na gharama za matibabu ya Watanzania limefikia Dola 9milioni za Marekani (Sh17bilioni), huku deni la MSD likifikia Sh108 bilioni.
Umbulla alisema mbali na madeni hayo, wizara hiyo inakabiliwa na changamoto 17 zinazotakiwa kupatiwa ufumbuzi wa haraka.
“Serikali ilipe deni la MSD na kutoa fedha za ununuzi wa dawa, vifaa tiba na vitendanishi kwa mkupuo.  Pia, taarifa za mapokezi ya dawa kutoka MSD katika hospitali au vituo vya afya nchini ziwekwe wazi na MSD itoe takwimu za usambazaji wake wa dawa ili kujitathmini katika utendaji wake,” alisema.
“Serikali inatakiwa kulipa deni la Apollo ili kutokiuka mkataba wa makubaliano baina ya Serikali na hospitali hiyo kwa kuwahudumia wagonjwa wa Tanzania,” alieleza.
Alisema kwa sasa idadi ya wagonjwa wanaokwenda nje ya nchi kwa ajili ya matibabu imeongezeka ikilinganishwa na bajeti inayotengwa.
Alisema bado sehemu kubwa ya shughuli za maendeleo za wizara hiyo zinategemea fedha za wahisani, kwamba mwaka 2014/15 zilitengwa Sh305 bilioni za maendeleo, Sh251.7 bilioni kati ya fedha hizo zilitoka kwa wadau wa maendeleo, jambo linaloathiri ununuzi wa dawa, vifaa tiba, vitendanishi na chanjo.
Akiwasilisha taarifa ya Kambi ya Upinzani kwa wizara hiyo, msemaji wake Dk Antony Mbassa alisema: “Fedha za maendeleo zilizotolewa katika wizara hiyo ni asilimia 26 ya mahitaji. “Mpaka Machi mwaka huu ilipatiwa Sh8.8 bilioni za maendeleo kati ya Sh305.7 bilioni ya mahitaji halisi ya wizara.”
Kambi hiyo pia iligusia suala la uhaba wa dawa katika hospitali nyingi nchini na kufafanua kuwa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO), zinaonyesha kuwa upatikanaji wa dawa katika vituo vya Serikali ni asilimia 24 na vituo binafsi ni asilimia 47. “Jambo ambalo tafsiri yake ni kwamba, dawa zinazosambazwa na MSD zinafika kwanza katika vituo binafsi kabla ya kufika katika vituo vya Serikali. Pia, tunataka majibu ya Serikali kuhusu deni la MSD na kuongezeka kwa gharama za kuwapeleka wagonjwa nje ya nchi,” alisema Mbassa.
Akiwasilisha bajeti ya Sh813.9 bilioni ya wizara hiyo, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid alieleza mafanikio katika sekta hiyo kwa mwaka 2015/16, akitaja vipaumbele vinane vya bajeti hiyo kwa mwaka ujao wa fedha.
Vipaumbele hivyo ni kuimarisha huduma na tiba, kuimarisha miundombinu kwenye vyuo vya afya na ustawi wa jamii, ukarabati wa miundombinu ya kutolea huduma za afya, kuimarisha Tehama na kutekeleza mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Kuhusu wakimbizi wa Burundi, Dk Rashid alisema hadi Mei 25, mwaka huu, wakimbizi 50,829 walikuwa wameingia nchini. “Pamoja na hali hiyo, kumetokea mlipuko wa ugonjwa wa kipindupindu na tangu Mei 25, mwaka huu, kuna wagonjwa 4,435 wa kipindupindu na 31 walifariki dunia,” alisema.
Bajeti hiyo haikupitishwa jana kutokana na kifo cha mbunge wa Ukonga (CCM), Eugen Mwaiposa. Bunge litaendelea kesho.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment