Social Icons

Pages

Wednesday, May 20, 2015

UFISADI

Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Profesa Musa Asad.
Dhambi ya kuendelea kulipa mishahara hewa kwa watumishi wa umma imesababisha serikali kupoteza Sh. bilioni 1.01 zilizokuwa zitumiwe na halmashauri na serikali za mitaa kwa mwaka wa fedha unaoishia Juni 30, 2014.
Hasara hiyo imetokana na halmashauri 36 kulipa zaidi ya Sh. bilioni 1.0 kwa wafanyakazi marehemu, wastaafu, watoro na waliofukuzwa. Taarifa hizo ni kwa mujibu wa ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) iliyotangazwa jana mjini Dodoma . Mkaguzi Mkuu ,Profesa Musa Asad, alisema na kuongeza kuwa hali kama hiyo ilijitokeza kwenye watumishi wa umma na serikali ambako zaidi ya Shilingi milioni 141. 4 zililipwa kwa mwaka huo.
Mkaguzi Mkuu alieleza kuwa marehemu walioacha kazi, wastaafu mbali na kulipwa mishahara walilipiwa bima za matibabu, kodi ya mshahara (Paye) na   michango ya mifuko ya hifadhi ya jamii. “Hili linatokana na kuchelewa kuwaondoa watumishi hao kwenye mtandao ya orodha ya mishahara  ya watumishi wote.”
Aliongeza:  “Hali hii bado  inaendelea licha ya kuwa serikali imewekeza kwenye mfumo wa kompyuta wa LAWSON kama njia  mojawapo ya kudhibiti upotevu huu,” alisema Mkaguzi Mkuu. Aliongeza kuwa milioni 845 zinazohusiana na halmashauri 32  zililipwa kama makato ya pensheni, bima ya afya, TRA kwa watumishi hewa.

HUJUMA MADINI
Makampuni ya  madini ya Geita Gold Mine na Resolute Tz Ltd, yameisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 22.33 kwa kuhujumu misamaha ya kodi waliyopewa. Wawekezaji hao walipewa msamaha wa kodi ya mafuta yanayotumika kwenye migodi yake ambayo yana thamani ya Sh. bilioni 22.33, kwa mujibu wa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Profesa Musa Asad.
Alikuwa akizungumzia ripoti ukaguzi ya hesabu za serikali kwa mwaka unaoishia Juni 30,2014. Alisema ufisadi huo uliotokea kwa vile kampuni hizo, hazikutumia mafuta hayo badala yake iliyatoa kwa wakandarasi wasiostahili msamaha huo hivyo kutumiwa bila kulipiwa ushuru na kuisababishia serikali hasara ya Sh. bilioni 22.33.
Alitaja ufisadi mwingine uliosababisha hasara ya Sh. milioni 392.7 ulifanywa na kampuni ya Kiliiwarrior Expeditions ya Arusha iliyokuwa imesamehewa kodi ya  Sh. milioni 465.2 ili kuingiza magari 28. Alifafanua kuwa kampuni hiyo ilitumia misamaha hiyo kinyume cha malengo na Mamlaka ya Mapato (TRA) ilipata kiasi cha Sh. milioni 72.

CCM, CHADEMA CUF HATI MBOVU
VYAMA vya  siasa vya CCM, Chadema, CUF, NCCR-Mageuzi vimepata hati zenye shaka zilizotolewa na Ofisi ya CAG, kutokana na taarifa za fedha zisizoridhisha. Alisema vingine vilivyopata hati hiyo ni TLP na Chaumma, huku vyama vya NLD, UMD, ADC, NRD, APPT na SAU vilipata hati mbaya ya ukaguzi.
Akizungumzia vilivyopata hati zenye shaka, alisema katika ukaguzi wa vyama 12 ilibainika kuwa taarifa zao za fedha zilifanywa tofauti na misingi ya uhasibu na mfumo wa uandaaji wa taarifa za fedha. Alieleza kuwa hadi Juni mwaka 2013 hesabu za vyama vya siasa 21 zilikaguliwa  kati ya hivyo  ni vyama 12 vilivyowasilisha taarifa zake  wakati vyama tisa  havikuwasilisha  taarifa.
“Vyama hivi ni UPDP, TADEA, UDP, Demokrasia Makini, CHAUSTA, DP, Jahazi Asilia, AFP na CCK.” Alisema Profesa Asad. Alisema katika ukaguzi wa taarifa za fedha tatizo la kuchelewesha uwasilishaji ripoti za fedha za vyama kwa CAG limejiri na kupendekeza kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kwa kushirikiana na Bodi ya Taifa ya Wahasibu waandae muongozo wa aina ya muundo wa taarifa za fedha utakaotumiwa na vyama vyote vya siasa.

MASHIRIKA YANAYOCHAKACHUA
Pia GAC ameitaja Mamlaka  ya Bonde la Ngorongoro kuwa imefanya ufisadi wa zaidi ya Sh. bilioni 2.3  (Dola milioni 5.54) kwa kununua bidhaa zisizokuwa na sababu ya msingi. Pia Kampuni ya Simu ya TTCL nayo ilinunua manunuzi yasiyokuwa na lazima yenye thamani ya Sh. milioni 381.97 (Dola 986, 938)  kama ilivyofanya Ngorongoro.
Kadhalika imelitaja  Shirika la Nyumba la Taifa, (NHC) kuwa limefanya manunuzi bila kushindanisha wazabuni yenye thamani ya Sh. bilioni 1.75. Kwa upande wa deni la serikali katika mifuko ya hifadhi ya jamii limefikia Sh. bilioni 1.6  Juni mwaka jana, kwa mujibu wa Mkaguzi  Mkuu Profesa Mussa Asad.
Akizungumzia suala la kukataa kutumia mashine za stakabadhi za kielektroniki (EFDs) , ameshauri serikali isifanye biashara  na kampuni kama haitumii EFDs. Alisema  ofisi yake ilibaini kuwa yamefanyika malipo ya Sh. bilioni 4.4 yasiyo ya risiti  hizo kwenye serikali kuu, wakati malipo mengine ya Sh. bilioni 4.6 yalifanywa kwa  halmashauri mbalimbali.
Alisema ili kuondoa kiburi cha kukataa EFDs serikali kuu na zile za mitaa zisifanye biashara na wasiotumia risiti hizo.

CHANZO: NIPASHE

No comments: