 
  
            
Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu akizungumza bungeni wakati wa 
kupitisha Muswada wa Sheria ya Miamala ya Kielektroniki wa Mwaka 2014 na
 Sheria wa Makosa ya Mtandao wa Mwaka 2015 mjini Dodoma, juzi usiku.
Mwanasheria Mkuu wa 
Chadema, Tundu Lissu amesema Kura ya Maoni kwa ajili ya kupitisha Katiba
 Inayopendekezwa haitaendeshwa bila kuifanyia marekebisho sheria 
inayoongoza mchakato huo.
Lissu, ambaye ni mbunge wa Singida Mashariki, 
alisema hayo jana wakati akiwasilisha hotuba ya Kambi ya Upinzani ya 
makadirio ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano) 
mjini hapa.
Kura ya Maoni ilipangwa kufanyika Aprili 30 lakini
 ikaahirishwa kwa muda usiojulikana kutokana na kasi ndogo ya 
uandikishaji wapigakura, lakini Lissu aliliambia Bunge jana baada ya 
kuahirishwa kuwa hakuna uwezekano wa kura hiyo kupigwa bila ya kufanyia 
marekebisho Sheria ya Kura ya Maoni ya mwaka 2013.
Vikao vinavyoendelea mjini Dodoma ni vya mwisho 
kwa Bunge la 10 lililochaguliwa mwaka 2010 na iwapo Serikali 
haitawasilisha muswada wa marekebisho ya sheria hiyo, Kura ya Maoni 
haitafanyika mwaka huu, kwa mujibu wa Lissu.
“Kwa kifupi Mheshimiwa Spika, hakuna uwezekano 
kisheria wa kurudia tena hatua zozote muhimu ambazo zilikwishachukuliwa 
kwa ajili ya kufanyika kwa Kura ya Maoni iliyokuwa imepangwa Aprili 30, 
2015,” alisema Lissu. 
“Mpaka sasa Serikali hii ya CCM haijawasilisha 
muswada wowote wa marekebisho ya sheria hiyo ili kuwezesha kufanyika kwa
 kura ya maoni siku za usoni.
“Kama ilivyokuwa kwa ahadi ya Kura ya Maoni ya 
Aprili 30,  Serikali hii ya CCM inadanganya Watanzania kuwa kutakuwa na 
Kura ya Maoni wakati kila mwenye akili timamu anajua hilo haliwezekani 
bila kwanza kuwa na mazingira wezeshi ya kisheria.”
Akiwasilisha hotuba ya upinzani, Lissu alisema 
kila hatua inayotakiwa kuchukuliwa, haiwezekani kuahirishwa wala 
kuongezewa muda kama ilivyofanywa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na 
Serikali. Lissu alisema kitendo cha kutofuata muda uliowekwa katika sheria hiyo, kinaiondolea sheria hiyo uhalali wa kuendelea kutumika.
Lissu, ambaye ni wakili wa kujitegemea, alisema 
ndani ya siku 14 tangu tarehe ya kupokea Katiba Inayopendekezwa, Rais 
alitakiwa kwa kushauriana na Rais wa Zanzibar, kuielekeza Tume ya 
Uchaguzi kwa amri iliyotangazwa katika Gazeti la Serikali kuendesha Kura
 ya Maoni.
Alisema amri ya Kura ya Maoni inatakiwa kufafanua kipindi cha kampeni na kipindi ambacho kura hiyo inatakiwa kufanyika.
“Rais Kikwete alikwishatoa amri kwa mujibu wa 
kifungu cha 4 cha Sheria ya Kura ya Maoni, lakini hana mamlaka yoyote, 
kwa mujibu wa sheria hii, ya kutengua amri yake au kutoa amri mpya ili 
kuwezesha kura ya maoni kufanyika kwa tarehe nyingine tofauti na tarehe 
iliyotangazwa kwenye amri ya  kwanza,” alisema.
Kauli ya Waziri
Alisema ndani ya siku saba baada ya kuchapishwa kwa Katiba 
Inayopendekezwa, NEC inatakiwa kuandaa swali la Kura ya Maoni na 
kulichapisha katika gazeti la Serikali. “Na ndani ya siku 14 baada ya kuchapisha swali 
hilo, Tume inatakiwa kutoa taarifa ya kufanyika kwa Kura ya Maoni, 
itakayoeleza kipindi cha kuhamasisha na kuelimisha umma juu ya kura hiyo
 na siku ya kura ya maoni,” alisema.
Alisisitiza kuwa kila msimamizi wa kura anatakiwa 
ndani ya siku 21 baada ya kuchapishwa kwa taarifa ya NEC, kuwajulisha 
wananchi katika jimbo lake la uchaguzi kuhusu utaratibu wa kufanyika kwa
 Kura ya Maoni.
Mbunge huyo aliongeza kuwa Tume inatakiwa kutoa 
elimu kwa umma juu ya Katiba Inayopendekezwa kwa muda wa siku 60 tangu 
Katiba Inayopendekezwa ilipochapishwa. “Tume ilishaandaa na kuchapisha swali la kura ya 
maoni na ilikwishatoa taarifa ya kura ya maoni na ratiba yake nzima na 
haina mamlaka yoyote, kwa mujibu wa Sheria ya Kura ya Maoni, kutengua 
taarifa yake na kutoa taarifa nyingine, au kuweka ratiba nyingine badala
 ya ratiba iliyokwishatolewa.
“Vile vile, Tume haiwezi kujiongezea muda wa kutoa
 elimu kwa umma juu ya Katiba Inayopendekezwa au kujipa muda mwingine 
kwa vile muda uliowekwa na sheria haukutumika ipasavyo.”
Alisema wasimamizi wa Kura ya Maoni hawana mamlaka
 yoyote kisheria ya kuongeza au kuongezewa muda wa kutoa taarifa kwa 
umma chini ya kifungu cha 5(2) cha Sheria ya Kura ya Maoni.
Lissu pia aligusia suala la Muungano, akisema 
Zanzibar haipati mgawo wa fedha za nje kwa ajili ya miradi ya maendeleo 
zikijumuisha misaada na mikopo, kwa kuwa mwaka 2013/14 zilikuwa Sh2,292 
bilioni, lakini zilikuwa kwa miradi ya maendeleo ya Tanzania Bara.
Kauli ya Waziri
Akiwasilisha bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais 
Mazingira na Muungano, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Samia Suluhu Hassan
 aligusia jinsi Serikali ya Awamu ya Nne ilivyodumisha Muungano na 
kulinda mazingira. Bajeti ya wizara hiyo ni Sh43 bilioni.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
 

No comments:
Post a Comment