Pages

Monday, May 04, 2015

MCHAKATO WA KATIBA MPYA: KATIBA ILIVYOLIGAWA TAIFA

Rais Jakaya Kikwete akizungumza siku alipozindua Bunge la Katiba. Anayefuata (kushoto) ni Spika wa Bunge la Katiba, Samuel Sitta na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein.
Wahenga walisema dalili ya mvua ni mawingi. Usemi huo umejidhihirisha kwenye mchakato wa mabadiliko ya Katiba ambao tayari umeonyesha kuligawa taifa katika makundi matatu; Serikali, taasisi za dini na vyama vya siasa. Dalili za vikwazo vya kukamilika kwa mchakato huo zilianza kuonekana wakati wa Bunge la Katiba, ambako April 16 mwaka jana,  wabunge zaidi ya 200 wanachama wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), walisusia vikao vya Bunge hilo na kutoka nje.
Hata hivyo, hatua hiyo haikuonekana kuathiri Bunge hilo kwa kuwa wajumbe wengine kutoka taasisi mbalimbali, kikiwamo chama tawala CCM, United Democratic (UDP), Tanzania Labour (TLP) na UPDP, waliendelea na mjadala.
Bunge hilo lilimalizika baada ya kupata zaidi ya theluthi mbili ya kura kutoka pande zote mbili za Muungano, yaani Tanzania Bara na Zanzibar, licha ya wajumbe wa Ukawa kulisusa.
Kitendo cha Ukawa kususia Bunge la Katiba kilionekana kuchochea taasisi zingine kutoa matamshi mbalimbali ya kutishia kuususia mchakato huo kama ifuatavyo;

Jumuia na Taasisi za Kiislamu
Mapema Februati mwaka huu, Jumuia na Taasisi za Kiislamu zipatazo 11, zikiwamo Baraza Kuu, Tampro, Basuta, Jasuta, IPC, Haiyat Ulamaa na Shura ya Maimamu Tanzania, zilitangaza kuwa zitafanya kampeni za  kuhamasisha wanajumuia wake kususia kupiga Kura za Maoni ya Katiba Inayopendekezwa hadi pale watakapopata uhakika wa uwepo wa Mahakama ya Kadhi yenye meno. Tangazo hilo lilitolewa na Naibu Katibu wa Jumuia ya Shura ya Maimamu Wilaya ya Kinondoni, Rajab Katimba.  
Jumuia hizo zikaeleza  kuwa kinachoendelea katika mchakato wa  upatikanaji wa Mahakama ya Kadhi, ni mwendelezo wa ulaghai ambao umekuwa ukifanyika miaka yote hasa kinapofika kipindi cha kupiga kura kwa lengo la kupata kura za waumini hao. Shehe Katimba anasema  kuna baadhi ya taasisi za kidini na vyombo vya habari vinapotosha kuwa  Mahakama ya Kadhi italeta vurugu.
Anasema kwamba Mahakama hiyo inatuhumiwa kuwa itatoa adhabu   za kikatili, ikiwamo kukata watu mikono, kuhukumu wasiokuwa Waislamu na kuwabagua wasiokuwa Waislamu.
Shehe Abdallah Bawazir ambaye ni Makamu Mwenyekiti wa Hay Atul-Ulamaa, akasema katika taarifa rasmi ya Jumuiya hiyo kuwa muswada unaojadiliwa ili kupatikana Mahakama ya Kadhi ni kiini macho.
Bawazir katika taarifa hiyo anafafanua kuwa muswada huo unaitaka Mahakama ya Kadhi ijiendeshe yenyewe bila kupata fedha kutoka Serikalini kitu ambacho hakiwezekani.
“Zipo mahakama za makundi ya watu maalumu ambazo zinaendeshwa kwa pesa za Serikali ambazo ni kodi za Watanzania wote. Mfano ni kama vile Mahakama ya Kazi, Ardhi na Mahakama ya Biashara. Kwa nini mahakama itakayotafsiri sheria za Kiislamu iwe nongwa?” alihoji.

Tamko la viongozi wa PCT
Machi 12, mwaka huu, Jukwaa la Kikristo Tanzania (PCT) linaloundwa na Baraza la Makanisa ya Kipentekoste Tanzania (CPCT) na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) lilitoa tamko la kutounga mkono Katiba Inayopendekezwa likidai kuwa katiba hiyo imeandaliwa katika mazingira yasiyokuwa ya kiuadilifu.
Waraka wa baraza hilo, kwa vyombo vya habari ulisainiwa na Askofu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheli Tanzania (KKKT), Dk Alex Malasusa kwa niaba ya (CCT), Rais wa Baraza la Maaskofu Katholiki Tanzania Tracius Ngalalekumtwa (TEC) na Daniel Aweti kwa niaba ya Wapentekoste (CPCT).
Katika tamko hilo PCT  ilibainisha kwamba  kutokana na hali hiyo, kanisa haliwezi kuunga mkono kupitishwa kwa Katiba Inayopendekezwa, hivyo liwataka waumini wao kuipigia kura ya hapana.
Jukwaa hilo limeeleza kuwa Katiba Inayopendekezwa haijajibu matakwa na malalamiko ya wananchi kwenye masuala mbalimbali yanayohusu muundo wa Serikali, miiko na maadili ya viongozi wa umma, uwiano wa mihimili ya dola, madaraka ya Rais na  haki za binadamu. 
“Kanisa haliwezi kuunga mkono kupitishwa kwa Katiba Inayopendekezwa kutokana na hali hii,  hivyo basi  Jukwaa linawataka waumini wake wote wajitokeze kwa wingi kujiandikisha katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, waisome Katiba Inayopendekezwa na kushiriki kikamilifu vipindi vya elimu juu ya Katiba Inayopendekezwa na kisha wajitokeze kwa wingi kupiga kura ya hapana,” ikasema sehemu ya taarifa hiyo.

Hatua ya Serikali
Siku chache baada ya kauli ya viongozi hao, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe alitangaza hatua ya Serikali kukusudia kuzifutia usajili taasisi mbalimbali za kidini, endapo zitabainika kukiuka sheria ya vyama vya kijamii. Chikawe akasema kinachofanywa na taasisi hizo ni kinyume cha sheria ya vyama vya kijamii Sura ya 337 na kanuni zake inayosimamia uendeshaji wa taasisi hizo.
“Kuanzia Aprili 20, mwaka huu taasisi zitakazoshindwa kuwasilisha taarifa za ukaguzi wa fedha za mwaka pamoja na kulipa ada zao zitachukuliwa hatua,” akaeleza Chikawe.
“Viongozi wa taasisi hizi, wanapokutana na kutoa matamko yanayolenga kuwashawishi waumini wao wafuate maelekezo yao kuhusu masuala ya Katiba Inayopendekezwa au uchaguzi mkuu ujao, matamshi kama hayo yanakiuka sheria za usajili wa taasisi hizo,” anasema Chikawe.

Wachambuzi wanasemaje?
Dk Benson Bana anaeleza kuwa “Si vizuri kukataza watu kushiriki zoezi halali kisheria, aidha siyo vizuri kuanza kujenga tabia ya kushinikiza mamlaka halali kufanya uamuzi kukidhi matakwa ya vikundi shinikizi.”
Kwa mujibu wa Dk Bana ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, katika masuala ya utawala na siasa  kufanya hivyo ni kujenga msingi mbaya kinyume na utawala bora.
Anasema Sheria ya Kura ya Maoni ipo wazi kwamba kambi zinazotakiwa ni inayoikubali mapendekezo yaliyopo  na kambi inayoyakataa mapendekezo hayo. Kundi lolote linaruhusiwa kuhamasisha upande unaotaka.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment