Dk. Benson Bana.
     
Wakati mzozo mkubwa umeibuka hivi karibuni juu ya 
kile kinachoelezwa kuwa serikali imekuwa ikipuuza maamuzi ya Bunge hasa 
kutokana na kinachoendelea nchini kwa sasa juu ya sakata za Escrow, 
Tokomeza na Richmond, mhadhiri mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Dar es 
Salaam, Dk. Benson Bana, amesema kimsingi kinachotokea ni kutokueleweka 
kwa dhana ya mgawanyo wa madaraka baina ya mihimili mitatu ya dola.
Katika mahojiano maalum na NIPASHE wiki hii, Dk. Bana ambaye ni 
mtaalamu wa utawala na sayansi ya siasa, alisema kuwa kwa bahati mbaya 
kumekuwa na msuguano mkubwa baina ya mihimili miwili, utawala 
(Executive) na Bunge (Legislature) kwa kiwango kikubwa nchini kila 
muhimili ukitaka kuuthibiti mwingine.
“Kwa bahati nzuri muhimili ambao umesurvive (umebaki salama) ni 
mahakama. Ukitazama kwa undani utaona bado muhimili huu hauingiliwi sana
 na mingine kama ilivyo kwa msuguano baina ya bunge na utawala,” alisema
 Dk. Bana.
Alisema kuwa wakati dhana ya mgawanyo wa madaraka ya dola baina ya 
mihimili mitatu ni mkamilishano, kinachoonekana katiba kuendesha mambo 
nchini kwa sasa ni: “Kuviziana na kutegeana.” Dk. Bana alisema kuwa hakuna ubishi kwamba Bunge kwa muda sasa 
limekuwa likifanya kazi nzuri katika kutimiza wajibu wake, lakini kuna 
tatizo moja kubwa juu ya namna mambo mengi yanavyoendeshwa na 
kuhitimishwa.
“Kwa nini kwa mfano uchunguzi haufanywi na kuwawajibisha mawaziri 
tu ndani ya Bunge ambao wana nafasi ya kujitetea ndani ya Bunge? Kwa 
nini mbunge anasimama na kumshughulikia mtendaji ambaye hawezi kujitetea
 ndani ya Bunge?” alihoji na kuongeza kuwa: “Dhana ya kudhibiti serikali inaweza kwenda mbali zaidi, hapa 
kinachojitokeza ni supremacy (kuwa na nguvu juu ya muhimili mwingine) na
 siyo mkamilishano. Kama Bunge linataka kuwa supreme, je, lenyewe 
linawajibishwa na nani? Mbona kwenye katiba inayopendekezwa wanakataa 
kuwajibishwa na wananchi?” alihoji.
Alisema katika sakata zilizotikisa nchi kama Tokomeza, ni kweli 
Kamati ya Bunge iliyochunguza madhila waliyofanyiwa wananchi iliibua 
mambo mengi na inasikitisha kwamba wananchi waliuawa, lakini cha 
kujiuliza ni kwamba, ni kwa kiwango gani kamati za Bunge zimekuwa na 
utaalam wa kuchunguza kila kitu.
Dk. Bana alisema kuwa ili Bunge liweze kutekeleza majukumu yake 
sawasawa na kuepuka kuingia katika mtego wa kutetea maslahi binafsi, ni 
vema kukawa na vitengo vya kudumu vya utafiti vyenye watalaamu wa 
kuendesha uchunguzi ili likitokea jambo, utaalamu wao uwaongoze wabunge 
kufikia hitimisho la kina la kile wanachofanya.
Alisema mara kadhaa kumekuwa na dalili za dhahiri za maslahi 
binafsi kuteka mijadala katika sakata kadhaa zilizotokea ndani ya Bunge. “Kwa mfano ukifuatilia na kusoma jinsi Mwakyembe (Dk. Harrison) alivyokuwa anawasilisha ripoti ya Richmond mbwembwe zote zile unaona wazi kwamba kulikuwa na mtu anawindwa. 
Ukisema mtu ajipime, ajitafakari unaona wazi kwamba hapa ni mtu 
anatafutwa katika mazingira haya tunaondoka kwenye hoja tunajadili 
personalities (watu),” alisema.
Alisema habari ya kumalizana na kuviziana inawaondoa watu kwenye 
hoja na matokeo yake kila anayepata fursa anamshughulikia mwingine na 
gharama yake ni kubwa kwa taifa. Dk. Bana alisema hadi sasa suala la Escrow limezidi kuwa zito na kwa maoni yake, bado ni tatizo kubwa.
“Serikali imeshindwa kuliweka sawa jambo hili, kuna wanaoamini 
kwamba fedha zilizokuwa kwenye akaunti ya Escrow zote ni za umma. Rais 
Kikwete alijaribu kulizungumzia hili, lakini halikupata wa kuli-amplify 
(kulipigia debe). Kuna tatizo la mawasiliano ndani ya serikali. Hakuna 
communication strategy (mkakati wa mawasiliano),” alisema na kuongeza:
“Umma unataka kujua ni kitu gani hasa kilisababisha ile fast 
tracking (kuharakisha) ya kuchukua zile fedha. Suala hili limeanzia 
mbali. Ni mkataba mbaya wa IPTL ambao ulianza mwaka 1994 chini ya Mwinyi
 (Ali Hassan), akaja Mkapa (Benjamin) na sasa chini ya Kikwete. Kuna 
nini hasa ndani ya kitu hiki?” alihoji na kusisitiza kuwa suala hili 
bado halijafanyiwa uchunguzi wa kutosha.
“Sitaki kuamini kwamba Takukuru wako makini kwenye suala hili. 
Yaani haijulikani nani alikuwa anagawa fedha? Escrow haijaisha bado,” 
alisisitiza. Alisema kuwa ni vigumu kina Profesa Muhongo na Eliackim Maswi na 
wote walioguswa na sakata la Escrow kurejea katika hali zao za kawaida 
mbele ya jamii hata kama kuna juhudi za kuwasafisha. “Maswi 
angestaafishwa mapema tu au sijui apelekwe wapi, hata kama ikifanyika 
nini, madhara kwa jamii dhidi yake yapo pale pale,” aliongeza.
Wakati Dk. Bana akionyesha madhara ya msuguano wa Bunge na utawala 
ambayo kwa kiwango kikubwa yamekuzwa na maslahi binafsi katika kufikia 
maamuzi mengi ambayo madhara yake yangeliweza kuepukwa, mchambuzi wa 
masuala ya siasa nchini, Alphonce Temba, alisema taarifa kwamba taifa 
sasa linadaiwa Sh. bilioni 120 baada ya serikali kushindwa kesi ya 
kuvunja mkataba wa Dowans huko Ufaransa katika mahakama ya usuluhishi, 
ni janga lingine linaloonyesha jinsi serikali ilivyozingirwa na makundi 
kiasi cha kujikuta ikifanya maamuzi bila kuwa makini.
“Kuna matabaka ndani ya CCM. Kila kundi linaweka mitego dhidi ya 
lingine. Ni mitego mitego, serikali siyo makini kwa sababu imegubikwa na
 mapambano ya makundi, kila moja likitaka kupata. Matokeo yake ni 
kutolewa kwa maamuzi ambayo siyo makini na yanayowagharimu wananchi,” 
alisema Temba.
“Yaani ndani ya CCM wenyewe kwa wenyewe wanashughulikiana kwa 
sababu tu kundi hili linapambana na mwekezaji, huyu afukuzwe kwa sababu 
tu wanaamini hakuletwa na kundi lao. Hali hii ni kielelezo cha serikali legelege. Siyo makini. Mwalimu 
alisema nchi imejaa nyufa, hii ni kansa inayoangamiza taifa,” alisema.
Temba alisema kuwa kwa kawaida makundi yanye maslahi binafsi hayana
 uzalendo ndani yake, hayana wito wa uongozi na katika maamuzi yake 
hayajali kwamba mwisho wake ni kuleta hasara kubwa kwa taifa kama ilivyo
 sasa kuhusu mkataba wa Dowans ambao nchi inadaiwa Sh. bilioni 120 baada
 ya kushindwa kesi.
Mei 12 mwaka huu, Kiongozi wa Kambi ya Upizani Bungeni (KUB), 
Freeman Mbowe, akiwasilisha msimamo wa kambi hiyo kuhusu makadirio ya 
matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha wa 2015/16, pamoja 
na mambo mengine alitaka kujua sababu za serikali kuchukizwa sana Bunge 
linapotekeleza wajibu wake na kutoa mifano ya juhudi za kuwasafisha 
watuhumiwa wa sakata za Tokomeza na Escrow, ambao ambao Bunge 
lilichunguza kashfa zao na kuwatia hatiani.
Katika hotuba hiyo iliyojaa makombora mazito dhidi ya udhaifu wa 
serikali hasa katika masuala ya uandikishaji wa wapigakura kwa mfumo wa 
BVR, Mbowe alisema makundi ndani ya CCM yamekuwa na madhara makubwa kwa 
taifa na kutoa mfano wa maamuzi yaliyokuwa yanasukumwa na makundi ya 
kugombea madaraka ndani ya chama hicho kiasi cha kukosekana kwa ukweli, 
uwazi na haki katika mchakato mzima wa kushughulikia kashfa ya Richmond.
Mbowe alisema wakati umefika kwa Serikali kusimama na kulielezea 
Taifa ni nani anasema kweli, ni nani alilidanganya Bunge na ni nani 
analindwa na serikali katika kashfa ya Richmond.
Katika hotuba hiyo ambayo Spika wa Bunge, Anne Makinda, alijitahidi
 kumzuia Mbowe asisome sehemu hiyo iliyokuwa inaivua nguo serikali na 
CCM kwa kisingizio cha muda na kwamba hatambui makubaliano ya kambi ya 
upinzani ya kuachiana muda ili hotuba nzima ya KUB isomwe yote na 
wananchi waisikie kwa kuwa ilikuwa ikirushwa moja kwa moja na TBC1, 
alisema katika mlolongo wa kushindwa kusimamia nchi, kuendekeza makundi 
na vita vya kisiasa ndani ya CCM na serikali yake, Taifa sasa linadaiwa 
Sh. bilioni 120 baada ya kushindwa kwenye kesi ya Dowans/Richmond katika
 Mahakama ya Kimataifa ya Usuluhishi (ICC) huko Paris, Ufaransa.
“Serikali haijataka kuliweka jambo hili wazi na ni dhahiri kuna 
siri kubwa inayosababisha jambo hili kuwa la usiri mkubwa. Huko mbele ya
 safari jambo hili litaligharimu Taifa mabilioni haya ya fedha ambayo 
yangeweza kuepukika kama ukweli, uwazi na haki vingetawala mchakato 
mzima wa kashfa ya Richmond. Serikali isimame sasa na ilieleze Taifa ni 
nani anasema kweli, ni nani alilidanganya Bunge na ni nani analindwa na 
serikali katika kashfa hii?” alisisitiza.
     CHANZO:
     NIPASHE
    
 

No comments:
Post a Comment