Pages

Thursday, April 02, 2015

NAMNA YA KUSAJILI MASHIRIKA YA KIJAMII


Mashirika au vyama vya kijamii yanasimamiwa na Sheria ya Vyama vya Kijamii (The Societies Act). Usajili wa mashirika haya hufanyika katika Wizara ya Mambo ya Ndani kupitia ofisi ya Msajili wa Vyama.
Ofisi hii ndiyo inapokea maombi ya usajili na kuyapitisha na kuidhinisha juu ya usajili wa shirika hilo au hapana. Ili kufanikiwa kusajili shirika au chama cha kijamii, unahitaji vitu kadhaa, mfano ni katiba. Katika zitahitajika ziandaliwe nakala kulingana na uhitaji uliopo.
Kwa kuwa katiba hiyo yaweza kuhitajika katika ngazi ya kata na wilaya, kabla ya kwenda Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Ni vyema zikaandaliwa nakala tano au zaidi. Mwishoni zinatakiwa zibaki nakala tatu za katiba hiyo ambazo zitapelekwa Wizara ya Mambo ya Ndani kwa ajili ya kuwasilisha maombi ya usajili. Vilevile, wahusika watapaswa kujaza fomu mbili, yaani SA. 1 na SA. 2 na kutoa nakala nyingine mbili za fomu hizo. Fomu hizo zinapatikana katika ofisi za Wizara ya Mambo ya Ndani na ofisi ya msajili wa mashirika ya kijamii.
Katika fomu hizo, mtahitajika kujaza taarifa mbali mbali ikiwemo; jina la shirika, mahali ofisi za shirika zilipo au zitakapokuwepo, anwani ya shirika, madhumuni ya shirika na sahihi za viongozi.
Muhtasari wa kikao cha wanachama ni muhimu pia. Muhtasari huu utaonyesha kwamba kikao kilifanyika na kuamua kuanzisha shirika hilo, kuteua viongozi wa shirika pamoja na kupitisha rasimu ya katiba ya shirika hilo na kila aliyehudhuria kikao hicho anapaswa kusaini kuonyesha kuwa alikuwapo.
Orodha ya wanachama waanzilishi pia ni muhimu. Wanachama hawa waanzilishi hawapaswi kuwa siyo chini ya 10. Wasifu wa viongozi wa shirika (CV) na picha zao. Pia ni jambo muhimu. Hii itajumuisha wasifu wa viongozi pamoja na picha zao (passport size). Wasifu huo wa kila kiongozi unapaswa kuwa nakala mbili au zaidi kulingana na uhitaji uliopo.
Barua ya utambulisho ikiashiria kuungwa mkono, inapaswa kutoka kwa mkuu wa wilaya ambayo ofisi ya shirika ilipo. Wataambatanisha pia barua ya maombi ya usajili kutoka kwa uongozi wa shirika. Barua hiyo ndiyo inayowasilisha maombi ya shirika katika wizara ili ianze mchakato wa kushughulikia usajili.
Ada ya usajili inalipiwa katika ofisi za wizara ili kusaidia mchakato wa usajili upate kuendelea. Ada imegawanyika katika mafungu mbalimbali ikiwamo; ya usajili, usajili na ya kila mwaka baada ya kusajiliwa.
Baada ya kusajiliwa shirika hilo linakuwa na nguvu za kisheria za kushtaki na kushtakiwa, kuajiri, kumiliki mali na kuendelea na shughuli za shirika hilo.
Jambo la kuzingatia baada ya usajili ni kwamba, shirika linapaswa kuendesha shughuli zake kwa mujibu wa katiba na sheria za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Shirika pia halipaswi kujihusisha kwenye shughuli zozote za kisiasa na linapaswa lidhihirishe kweli limesajiliwa ili kuisaidia na kuinufaisha jamii na siyo kuwanufaisha watu wachache.
Mnapaswa kuanzisha miradi na kuwa na mipango yenye kuleta mguso katika jamii husika kwa kuangalia ile inayoweza kuharakisha maendeleo kulingana na malengo ya shirika.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment