Pages

Thursday, April 02, 2015

NAMNA YA KUANDIKA, KUTEKELEZA WASIA


Uwanja wa Kambole leo unakupa fursa ya kusoma na kuelewa juu ya sheria za mirathi hasa kwenye kipengele cha wasia, watu wengi wanaweza kudhani wanajua juu ya wasia lakini si kweli.
Wasia ni tamko la mdomo au maandishi anayotoa mtu wakati wa uhai wake kueleza jinsi atakavyotaka mali zake zigawanywe au mwili wake utendewe, atakapokuwa amefariki. Wasia ni siri ambayo hufichuliwa pale marehemu anapofariki. Mtu anayekufa kistaarabu ni yule anayeacha wasia. Mtu yeyote anaweza kuandika wasia iwapo ana umri wa zaidi ya miaka kumi na nane na ana akili timamu. Mtu anayeumwa sana au amezeeka sana unapaswa kuhakikisha anaelewa nini anachoandika kwenye wasia. Kuandika wasia siyo lazima uwe na mali nyingi. Watu wanadhani kuandika wasia ni mpaka uwe na mali nyingi au fedha nyingi.
Tunakosea sana. Mali siyo sifa ya kukufanya uandike wasia, hata ukichagua sehemu ya kuzikwa ni wasia tosha. Faida za kuandika wasia zipo nyingi. Baadhi ya hizo ni pamoja na kuweka mambo bayana na kuondoa utata wowote kwenye familia na jamii yako.
Unapata fursa ya kumchagua msimamizi wa mirathi unaye mtaka, pia unatoa maelekezo juu ya mwili na mali zako kama unavyopenda wewe na kwa mujibu wa sheria. Pia ni ustaarabu kuandika wasia.
Wasia unaokubalika kisheria una sifa zifuatazo: unaweza kuwa wa maandishi au mdomo. Wasia wa maandishi unatakiwa uwe na mashahidi wawili, na ule wa mdomo unatakiwa uwe na mashahidi wanne.
Ni muhimu mmoja wapo wa mashahidi awe ndugu wa karibu ila asiwe mrithi. Wasia uwe ni wa mali zako binafsi, siyo za watu wengine, yaani, huwezi kuandika wasia kugawa mali za watu. Pia, haikubaliki wasia kumnyima mali mrithi halali wa kisheria. Lakini anaye andika wasia awe na akili timamu na asiwe mgonjwa sana kiasi cha kushindwa kuelewa anapotoa wasia. Wasia ulioandikwa kwa kulazimishwa, siyo halali.
Warithi halali kisheria ni mke ama mume, watoto waliozaliwa ndani ya ndoa, watoto waliohalalishwa kisheria, pia watoto wa nje wanaweza kurithi, inategemeana na mila na desturi za marehemu, lakini siyo ustaarabu kuwanyima maana siyo kosa lao.
Wasia ulioandikwa vizuri ni ule unaoweza kugawa mali zilizopo na zile zitakazofuata kabla ya kifo, lakini wasia unaweza kubadilishwa muda wowote kabla ya mhusika kufa na mwenye uwezo wa kubadili wasia huo ni yeye mwenyewe aliyeuandika.
Mgawanyo wa mali ya marehemu utategemea wasia ulivyoandikwa. Wasia unapaswa kuheshimiwa, maana yale ni matakwa na nia ya marehemu kwa hiyo, unapaswa kuheshimiwa kwa kila namna, labda awe marehemu ametaka vitu visivyowezekana.
Iwapo mtu ambaye marehemu amemtaja kwenye wasia usimamie mali zake, kama huwezi ni bora kujitoa na sio kukubali halafu baadaye unachezea mali za marehemu na kujinufaisha mwenyewe.
Hiyo ni kinyume cha sheria na anaweza kushtakiwa na kudaiwa au kufunguliwa kesi. Wasia unaweza kuhifadhiwa kwa wakili, mahakamani, benki, taasisi za dini kama kanisani au msikitini, pia wasia unaweza kutunzwa kwa mtu yeyote ambaye anaaminika na anaweza kutunza siri, lakini asiwe ni mnufaikaji wa wasia husika. Tuwekane sawa kuwa kuandika wasia siyo uchuro, bali ni kuweka mambo sawa baada ya wewe kufariki, mali zako zitumike kuwanufaisha na kuwasomesha watoto na ndugu wa karibu kama wapo.
Hata hivyo, aina za wasia zinategemea mila na desturi za marehemu na kwa mujibu wa sheria husika. Uhalali wa wasia unategemea pia sheria husika. Kuna sheria za kiislamu, Kikristo na kimila.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment