Pages

Tuesday, January 13, 2015

NYALANDU APINGA KENYA KUYAZUIA MAGARI YA TANZANIA

Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu
Serikali imesema haikubaliani na uamuzi wa Serikali ya Kenya ya kuendelea kuzuia magari ya Tanzania kuingia katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyata kupeleka na kupokea watalii wanaokuja Tanzania.

Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, aliyasema hayo wakati akizugumza na wasafirishaji wa abiria na watalii katika maegesho ya Mezaluna. Alisema serikali imeshtushwa mno na hatua hiyo ambayo imeleta usumbufu mkubwa kwa wasafiri hasa watalii wanaokuja Tanzania kupitia uwanja huo. 
Nyalandu alisema hatua hiyo inahatarisha mahusiano mazuri ya muda mrefu ya kibiashara kati ya Kenya na Tanzania. “Tunafahamu tulikuwa na mkataba na Kenya kuhusu mwingiliano katika biashara kwenye sekta ya utalii. Serikali ya Awamu ya Kwanza ilifunga barabara Bologonja iliyopo kusini mwa hifadhi ya Serengeti na Kenya walituomba tufungue barabara hiyo tukawaaambia watupe nafasi ya kufanya utafiti iwapo inawezekana,” alisema Nyalandu.
Alisema baada ya Tanzania kuonyesha msimamo huo, wakaamua kuzuia magari kuingia Uwanja wa Ndege kama kulipiza kisasi. "Ni jambo la ajabu sana kwani uwanja wa ndege hauwezi kuwa sehemu ya vivutio vya utalii," alisema. Aliongeza: “Wiki ijayo nitakwenda Nairobi kuzungumza na Waziri wa masuala ya utalii wa Kenya kuhusu jambo hili ili tujue hatua za  kuchukua."
Awali wasafirishaji walimwambia Waziri Nyalandu kuwa toka Desemba 22, mwaka jana, magari yao yalizuiwa kuingia katika Uwanja wa Ndege wa Jomo Kenyata na kusabababisha adha kubwa kwa watalii. Mkurugenzi wa kampuni ya Riverside, Mosses King’ori, alisema kuwa watalii wamekuwa wakihofu usalama wao kila wanaposhushwa na mizigo yao nje ya uzio wa uwanja. “Biashara yetu ipo katika tishio kubwa, lakini hata kwa utalii wakwetu. Wageni wanaogopa sana hali hii...napata maswali mengi kutoka kwa mawakala wa Ulaya ambao tunafanya kazi wanadai wageni wanalalamika na wengine wana hofu kuja Tanzania,” alisema King’ori.
Naye Mkurugenzi wa kampuni ya Rainbow, Mathew Mollel, alieleza kuwa serikali imechelewa mno kufuatilia jambo hilo na kusababisha madereva na Watanzania wengine kupata shida kubwa kutokana na katazo hilo. “Serikali sasa ituambie ukweli utalii ni sehemu kubwa ya uchumi wa nchi yetu, ni eneo linalopaswa kulindwa sana,” alisisitiza Mollel.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment