Pages

Wednesday, January 21, 2015

ANNA ABDALLAH ATAKA VIGOGO WAPIGWE RUNGU


Mjumbe wa Kamati ya Uongozi ya Wabunge wa CCM, Anna Abdallah amesema wanachama wote wanaoendelea kukiuka kanuni na taratibu za chama hicho, lazima wachukuliwe hatua kali za kinidhamu.
Alisema chama kitapunguza heshima yake endapo wanachama hao hawataadhibiwa kwa sababu walishapewa adhabu lakini hawataki kujirekebisha. Ingawa hakuwataja, waliopewa adhabu ni; Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Stephen Wasira, Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja. Adhabu zao zinamalizika Februari 18, mwaka huu. Kauli hiyo imekuja wakati Kamati ndogo ya maadili ya chama hicho inayoongozwa na Makamu Mwenyekiti wake (Bara), Philip Mangula, ikimaliza kazi ya kutathmini adhabu hizo juzi huku Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye akisema inashangaza kuona baadhi yao wakiendelea kufanya kampeni licha ya kamati Kuu ya CCM kupiga marufuku.
Msimamo wa Anna Abdallah
Akizungumza jana, Abdallah ambaye ni Mwenyekiti wa Umoja wa Wanawake Wanasiasa Tanzania (Ulingo), alisema chama hakitakiwi kuogopa lolote juu ya kuwaadhibu wanachama hao. “Mwanachama asipokuwa mtii wa kanuni za chama, huyo hatakiwi tena kuwa mwanachama, lazima ashughulikiwe na kama hataki kutii agizo la chama basi ajiondoe kwenye chama ili aende huko anakodhani kuna uhuru wa aina hiyo,” alisema na kuongeza: “Chama kisiogope lolote kwani nidhamu inajengwa na utii wa kutekeleza maagizo ya chama, kisipowachukulia hatua nadhani inaweza kuleta athari kwa wengine kutotii maagizo.”
Kauli ya Nape
Akizungumza jana CCM Kisiwandui, Zanzibar baada ya Kamati Ndogo ya Maadili kumaliza kazi ya kuwajadili viongozi wa waliokumbwa na kashfa ya ufisadi wa fedha za Akaunti ya Tegeta Escrow, Nape alisema: “Chama hakitasita kuwanyima nafasi ya kuwania urais wagombea watakaobainika na kudhibitika kuendelea kufanya kampeni kabla ya wakati kinyume na mwongozo uliotolewa mwaka jana.” Aliwataka wagombea na wapambe wao kuheshimu utaratibu na uamuzi wa chama na wakati ukifika, kila mgombea atapewa haki ya kufanya kampeni. Alisema licha ya wagombea hao kutahadharishwa, lakini bado wapo na wapambe wao wanaondelea kufanya kampeni. Nape pia alisema kumewa na uzushi mwingi kuhusu baadhi ya wagombea kujadiliwa na vikao vya chama na kuelezwa kuwa wapo katika hatari ya kupoteza hata uanachama wao mambo ambayo hayana ukweli. Aliwataka wananchi kutosikiliza taarifa za uvumi kuhusu wagombea au shughuli za chama hicho. Katibu huyo aliwataka wagombea wa nafasi ya urais waliojitokeza kusimamia miiko ya chama na kuwakanya wapambe wao na watu wanaosambaza taarifa za uongo dhidi ya chama na kujiepusha na kampeni mapema kabla ya kuwavurugia. “Wengi wanaosambaza taarifa hizi ni wagombea au wapambe wao wasiojiamini kutokana na matendo yao, ambayo hata wao wana shaka na uadilifu wao. Hatuoni sababu ya mgombea anayefuata sheria, kanuni na taratibu za chama kuhofia kuchuliwa hatua kila vikao vya chama vinapofanyika,” alisema Nape.
Kashfa ya escrow
Alisema pia kwamba kamati hiyo imemaliza kuwajadili viongozi waliokumbwa na kashfa ya escrow na kwamba uamuzi na mapendekezo yake yatawasilishwa katika kikao cha Kamati Kuu. “Tumemaliza na Kamati itawasilisha mapendekezo yake kwa Mwenyekiti, Rais Jakaya Kikwete baadaye Februari.” Waliokumbwa na kashfa ya miamala ya Akaunti ya Tegeta Escrow ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti ya Bunge na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka, Mwenyekiti wa Kamati ya Katiba na Sheria na Mbunge wa Segerema, William Ngeleja.
Kinana na mabango
Katika hatua nyingine, Kinana ambaye yuko katika ziara ya siku 10 Visiwani Zanzibar, amepokewa kwa mabango na wananchi wa Kijiji cha Miwani, Mkoa wa Kusini Unguja, waliokuwa wakilalamikia kero ya muda mrefu ya uchakavu wa barabara, ukosefu wa huduma za maji, afya na mgogoro wa masilahi ya kisiasa uliyoibuka baina ya Mbunge wa Uzini, Mohamed Seif Khatib na Mwakilishi, Mohamed Raza. Wananchi hao walinyanyua mabango yao muda mfupi baada ya kiongozi huyo kuwasili katika mkoa huo kukagua uhai wa chama. Wakizungumza muda mfupi baada ya kuwasilisha ujumbe wao kwa amani, wananchi hao walisema kwa muda mrefu wamekuwa wakikabiliwa na matatizo hayo bila dalili za suluhu. Mkazi wa Miwani, Juma Mussa Ussi alisema mgogoro wa masilahi ya kisiasa baina ya Khatib na Raza unadumaza maendeleo ya jimbo na kwamba wameamua kuwasilisha ujumbe huo kwa kiongozi wa juu baada ya viongozi wa chama na Serikali Zanzibar kushindwa kuutatua. Kinana aliwataka viongozi wa chama hicho Mkoa wa Kusini Unguja, pamoja na viongozi wa CCM Zanzibar kuchukua hatua za haraka kusuluhisha mgogoro huo. Khatib alisema anaunga mkono hatua ya wananchi kulalamika juu ya kero zinazowakabili kwa kuwa yamekuwa ya muda mrefu yakiwamo ya uchakavu wa barabara, ukosefu wa daktari na dawa katika Kituo cha Afya Miwani na uhaba wa Majisafi. Alisema tatizo la maji limesababishwa na kuungua kwa mashine ya kuyasukuma kutoka katika Manzese lakini licha ya kuwasilisha taarifa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA), hakuna hatua zilizochukuliwa. Kuhusu mgogoro wake na Raza alisema hakumbuki kuwa na mgogoro na mwakilishi huyo.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment