Pages

Tuesday, December 16, 2014

WALIOSABABISHA UCHAGUZI KUVURUGIKA WAWAJIBISHWE

Askari wakiwataka wananchi kutawanyika baada ya kuahirishwa uchaguzi wa Serikali za mitaa katika kituo cha Mabibo Mpakani Mtaa wa Jitegemee, Dar es Salaam jana.


Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika juzi nchi nzima ulikumbwa na kasoro nyingi ambazo wananchi wengi wanasema zilitokana na uzembe au hujuma kwa upande wa maofisa walioteuliwa kuuratibu na kuusimamia. Ni dhahiri sasa kwamba kasoro nyingi zilizougubika uchaguzi huo hazikutokea kwa bahati mbaya, kutokana na kutokea katika mazingira yanayoonyesha kwamba aidha zilitokea kwa uzembe au kwa makusudi kwa lengo la kutimiza malengo fulani ya kisiasa.
Haijawahi kutokea uchaguzi huo, ambao husimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu inayohusika na Serikali za Mitaa (Tamisemi), kugubikwa na kasoro nyingi kama ilivyotokea katika uchaguzi huo. Pamoja na vyombo vya habari na asasi nyingi zisizo za kiserikali kuonya mapema kwamba uchaguzi huo ungekabiliwa na matatizo mengi kutokana na kutofanyika matayarisho ya kutosha, viongozi serikalini wakiwamo wa Tamisemi walikaa kimya, hivyo kusababisha hofu kwamba uchaguzi huo ungevurugika.
Kama tulivyosema hapo juu, kasoro zilizojitokeza hazikuwa za kawaida. Vituo vingi vya kupigia kura viligeuka kuwa viwanja vya mapambano, kutokana na kuwapo sintofahamu iliyosababishwa na kutokuwapo kwa uhakika wa kupiga kura. Katika sehemu nyingi, uchaguzi uliahirishwa kutokana na kutokuwapo kwa karatasi za kupigia kura, huku katika baadhi ya sehemu uchaguzi ukiahirishwa kutokana na karatasi hizo kuibwa. Baadhi ya maeneo yalikumbwa na tatizo la majina ya baadhi ya wagombea kubadilishwa vyama wakati sehemu nyingine zilishuhudia wapigakura wakishindwa kuona majina yao kwenye orodha ya wapigakura, huku wengine wakikuta majina yao yamewekwa alama za kuonyesha kwamba walikuwa tayari wamepiga kura.
Katika maeneo mengi, wananchi walicheleweshwa kupiga kura kutokana na kuchelewa kwa vifaa vya kupigia kura, wakati wengine walipiga kura pasipo kujiandikisha au kutumia wino unaotumiwa kubaini watu ambao tayari wamepiga kura. Kero kubwa ilikuwa pale baadhi ya wasimamizi walipopima umri wa wapigakura kwa macho na kuwakataa baadhi ya wapigakura waliokuwa wamejiandikisha. Katika mazingira yaliyoonyesha kwamba hapakuwapo ulinzi wa kutosha, ulitokea wizi wa maboksi ya kura katika baadhi ya maeneo, huku katika maeneo mengine wapigakura wakipelekwa vituoni kwa mabasi yaliyokodiwa kinyume na kanuni za uchaguzi huo.
Matokeo ya hali hiyo ni vurugu zilizosababisha, kwa mfano, kuchomwa moto Ofisi ya Mtendaji wa Serikali za Mitaa, Sumbawanga mkoani Rukwa na kusababisha uchaguzi kuahirishwa katika kata tisa kati ya 19 mjini humo. Katika maeneo mengi nchini polisi walitumia mabomu ya machozi kutuliza vurugu za aina hiyo zilizotokana na wananchi kupinga kuvurugwa kwa uchaguzi huo kwa kutokuwapo maandalizi ya kutosha na matatizo mengine ambayo yangeweza kuepukwa kama mamlaka zilizoandaa uchaguzi huo zingekuwa na dhamira ya kuufanikisha.
Ni katika mazingira hayo tunasema uchaguzi huo haukuwa huru na wa haki katika sehemu nyingi nchini. Jambo la kushangaza ni pale wagombea wengi wa upinzani walipowekewa pingamizi zisizo za msingi na wenzao wa CCM, huku rufaa zao zikitupwa ama kutosikilizwa na kamati za rufaa. Matokeo yake ni wale wa CCM kupita bila kupingwa. Ndiyo maana tunasema viongozi wote katika ngazi zote za mchakato huo kuanzia wizarani hadi vijiji, vitongoji na mitaa waliosababisha hali hiyo, wawajibishwe. Uvurugaji wa chaguzi mbalimbali nchini utaendelea kuwa utamaduni wa kudumu, kama mamlaka husika zitaendelea kushindwa kuwawajibisha viongozi ‘nyangumi’ na kuwaonea maofisa ‘dagaa’.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment