Social Icons

Pages

Wednesday, December 24, 2014

USAFIRI WAWATESA ABIRIA WA MOSHI, ARUSHA


Uhaba wa mabasi yanayokwenda mikoa ya Kilimanjaro na Arusha umeendelea kuwatesa abiria wa mikoa hiyo hali iliyowalizimu wagombee mabasi ya usafiri wa  jijini hapa maarufu  kama ‘daladala’ ambayo yameruhusiwa kufanya safari katika mikoa hiyo. Picha|Maktaba
Mapema juzi, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usafirishaji wa Majini na Nchi Kavu (Sumatra), Gilliard Ngewe alinukuliwa na gazeti  hili kuwa  jana wangeongeza mabasi makubwa matano ili kukidhi mahitaji ya abiria lakini jitihada hizo ziligonga mwamba baada ya mabasi hayo kudai kuwa yamejaa.
Akikagua na kutoa vibali kwa daladala hizo katika Kituo  cha Mabasi yaendayo mikoani kilichopo Ubungo, Ofisa Mfawidhi wa Sumatra, Conrad Shio alisema jana kuwa kila jitihada za kuyapata mabasi mengine makubwa lakini ilishindikana na kuamua kuendelea kutumia usafiri wa daladala hizo aina ya Eicher kusafirisha abiria.
“Leo (jana) kuanzia saa moja asubuhi hali ilianza kuwa mbaya tofauti na siku zingine ndiyo maana tunazikagua hizi daladala ili ziwasafirishe hawa abiria, tukishatoa kibali abiria wanaanza kugombania.
“Hatuna jinsi tutaendelea kuzitumia hizi daladala maana mabasi ya njia nyingine tuliyokuwa  tukiyatagemea kurahisisha kazi hii nao  wana kilio chao cha abiria kuwa wengi wanaelekea katika mikoa wanayokwenda,” alisema.
Shio alisema daladala hizo zenye uwezo wa kubeba abiria 41 zilianza kuruhusiwa juzi na zaidi ya Eicher 25 zimepewa vibali na  kutoza nauli ya Sh25,000 iliyopangwa na Sumatra.  
Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Awath Haji alisema polisi wamejipanga kuhakisha abiria hao wanalindwa kwa kipindi chote watakachokuwa wakisubiri usafiri kituoni hapo.
“Tangu asubuhi nipo hapa nikikagua  magari zikiwamo hizi daladala na sijapokea malalamiko yoyote kutoka  kwa abiria,” alisema Haji.
Albert Kitale ni miongoni mwa abiria waliokuwa wakisubiri mabasi kuelekea Same mkoani Kilimanjaro, alisema hali ya usafiri ni mbaya, kwani mabasi yote yamejaa hadi Desemba 27.
“Huu umati wa abiria  unaonekana upo toka saa 11 alfariji  mabasi ya kuunganisha hakuna na sidhani kama hizi daladala zilizopo zitatosha. Jana (juzi) nilisikia  kulikuwa na utaratibu wa kupanga foleni ya kupanda katika daladala lakini leo suala hilo hakuna gari likishakaguliwa na kupewa kibali  abiria tunagombania,” alisema Kitale.

No comments: