Kwa muda mrefu sasa, tumekuwa tukionya kuhusu
udanganyifu katika chaguzi mbalimbali zinazofanyika katika nchi yetu na
kusema hiyo hasa ndiyo sababu inayowakwaza wananchi wengi kiasi cha
kutojitokeza kupiga kura.
Tumekuwa tukisisitiza kuwa, pamoja na takwimu kuonyesha bayana kwamba idadi ya watu wanaojitokeza kupiga kura inapungua mwaka hadi mwaka, Serikali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NecC) zimekaa kimya bila kuona umuhimu wa kutafuta kiini cha tatizo hilo na kulitafutia ufumbuzi. Hofu yetu muda wote imekuwa kwamba madhara yanayoweza kusababishwa na udanganyifu katika uchaguzi ni makubwa.
Tumekuwa tukisisitiza kuwa, pamoja na takwimu kuonyesha bayana kwamba idadi ya watu wanaojitokeza kupiga kura inapungua mwaka hadi mwaka, Serikali na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NecC) zimekaa kimya bila kuona umuhimu wa kutafuta kiini cha tatizo hilo na kulitafutia ufumbuzi. Hofu yetu muda wote imekuwa kwamba madhara yanayoweza kusababishwa na udanganyifu katika uchaguzi ni makubwa.
Hakuna asiyejua kwamba wizi wa kura na udanganyifu
mwingine katika uchaguzi umesababisha maafa makubwa katika nchi nyingi
barani Afrika, ikiwa ni pamoja na vita ya wenyewe kwa wenyewe. Ikumbukwe
kwamba baadhi ya nchi zilizokumbwa na maafa hayo zilikuwa zikisifika
kwa umoja na utulivu kama ilivyo kwa Tanzania. Hivyo, somo tunalopaswa kujifunza kama Taifa ni
kuwa, amani iliyopo katika taifa lolote ikichezewa, kwa maana ya
watawala kufanya hila na udanganyifu katika chaguzi ili waendelee kubaki
madarakani, husababisha Taifa husika kusambaratika.
Tusisahau kwamba Tanzania siyo kisiwa, hivyo
tusijidanganye kudhani kwamba amani na utulivu tulionao utadumu hata
kama wananchi wataendelea kunyimwa haki zao za kikatiba, ikiwa ni pamoja
na kuchagua viongozi wanaowataka.
Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika Jumapili
iliyopita umewafadhaisha wananchi wengi. Uligubikwa na vimbwanga na
kasoro nyingi ikiwa ni pamoja na vitendo vya udanganyifu, hila na
hujuma.
Waziri Hawa Ghasia, ambaye wizara yake ya Tamisemi
ndiyo husimamia uchaguzi huo, anasema wizara yake haiwezi kutolea
ufafanuzi malalamiko kuhusu kasoro lukuki zilizojitokeza katika uchaguzi
wa Jumapili hadi itakapopata ripoti kutoka mikoani. Lakini waziri huyo
anasahau kwamba kabla ya uchaguzi huo, alikutana na vyama vya siasa
mjini Morogoro, ambako vyama hivyo viliainisha na kujadili kasoro za
uchaguzi hata kabla hazijatokea katika uchaguzi wenyewe. Pamoja na mambo
mengine, vyama hivyo viliunga mkono kauli ya awali ya Rais Jakaya
Kikwete kuhusu umuhimu wa kusogeza mbele tarehe ya uchaguzi huo ili
kukamilisha maandalizi.
Tunaambiwa kwamba kikao hicho pia kiliona kasoro
katika maeneo mbalimbali ya mapendekezo ya Serikali kuhusu kanuni za
uchaguzi, ambazo hata katika uchaguzi wa Jumapili, zilileta matatizo
makubwa. Hata hivyo, Waziri Ghasia alishikilia msimamo wa Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda kwamba uchaguzi ufanyike Jumapili iliyopita, hivyo
viongozi hao wawili hawawezi kukwepa lawama na kuwajibika kwa kasoro
zote zilizojitokeza katika uchaguzi huo.
Ndiyo maana tunasema visingizio vinavyotolewa na
Waziri Ghasia na Tamisemi kwa jumla haviwezi hata kidogo kuhalalisha
udhaifu, hujuma, uzembe na udanganyifu uliojitokeza katika uchaguzi wa
juzi.
Baada ya kukataa kwa muda mrefu mapendekezo ya
wadau kwamba chaguzi za Serikali za Mitaa pia zisimamiwe na Tume ya
Taifa ya Uchaguzi (NEC), Serikali sasa imesema utaratibu huo utaanza
wakati wa uchaguzi wa mwaka 2019.
Hata hivyo, hatudhani kama kutakuwa na mabadiliko
yoyote katika chaguzi zetu kama Nec haitaundwa upya na kuwa tume huru ya
taifa ya uchaguzi (NIEC).
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment