Nchi za Kenya na India 
zimeipita kwa mbali Tanzania kwa kusafirisha na kuuza katika soko la 
dunia, madini ya tanzanite ambayo yanapatikana hapa nchini pekee.
Kamishna wa Madini katika Wizara ya Nishati na 
Madini, Mhandisi Paul Masanja aliwaambia waandishi wa habari jijini hapa
 jana kwamba kwa mwaka jana, Tanzania haikufikia hata nusu ya Kenya kwa 
mauzo ya madini hayo ya vito.
Kamishna Masanja alisema mwaka jana pekee, Kenya 
ilisafirisha na kuuza nje ya nchi tanzanite yenye thamani ya zaidi ya 
Dola 100 milioni za Marekani (Sh173 bilioni) dhidi ya Dola 38 milioni 
(Sh45.5 bilioni) zilizouzwa na Tanzania.
“Katika kipindi hicho cha mwaka jana, India iliuza
 tanzanite zenye thamani ya zaidi ya Dola za Marekani 300 milioni (Sh509
 bilioni) kiasi cha baadhi ya wanunuzi wakubwa, hasa kutoka Marekani 
kujiuliza iwapo madini hayo yanachimbwa India,” alisema Masanja.
Bila kumtaja jina, Kamishna huyo alisema mmoja wa 
wanunuzi wakubwa wa madini ya vito kutoka nchini Marekani aliwahi 
kumuuliza iwapo kuna migodi ya tanzanite India kwa sababu akifika huko 
hupata tanzanite bora na zenye ukubwa kuliko anayopata Tanzania.
Alisema zaidi ya asilimia 80 ya tanzanite 
inayopatikana Mirerani, Wilaya ya Simanjiro, Manyara huuzwa kwa njia za 
panya nje ya nchi na kwamba Serikali imeanza kuchukua hatua.
“Serikali inakusudia kuunda kikosi kazi 
kitakachojumuisha askari kutoka vyombo vyote vya ulinzi na usalama 
kukabiliana na utoroshaji madini nje ya nchi.”
Alisema hivi karibuni, wizara itawasilisha muswada
 bungeni kurekebisha Sheria ya Madini Namba 6 ili kumpa mamlaka Kamishna
 wa Madini kutaifisha madini yote yanayokamatwa yakisafirishwa kinyume 
cha sheria.
“Tunataka sheria ya madini ifanane na ile ya 
misitu inayotaifisha mazao yote ya misitu yanayovunwa kinyume cha 
sheria, tofauti na sasa ambapo tunalazimika kusubiri uamuzi wa Mahakama 
kutaifisha madini iwapo watuhumiwa wanatiwa hatiani,” alisema.
Hadi sasa, Serikali imekamata na kutaifisha madini
 yenye thamani ya zaidi ya Sh15 bilioni yaliyokamatwa yakitoroshwa nje 
ya nchi baada ya watuhumiwa kutiwa hatiani na Mahakama.
“Tuna mpango wa kujenga kituo maalumu cha madini 
kitakachojulikana kama Madini House kitakachokuwa na ofisi zote za 
kununua na kuuza madini ya vito ili kudhibiti biashara holela,” alisema 
Masanja.
Alisema katika kituo hicho kutakuwa na huduma za 
kodi na malipo mbalimbali ya Serikali pamoja na usafiri wa helikopta za 
kusafisha madini kwenda viwanja vya ndege ili kuepuka wizi na uvamizi 
njiani.
Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Ngosi Mwihava aliwataka Watanzania kushiriki katika vita dhidi ya uhujumu uchumi na kwamba juhudi za Serikali za kupambana na wanaotorosha madini nje ya nchi haziwezi kufanikiwa bila ushiriki wa umma kwa kutoa taarifa kwa vyombo na mamlaka husika.
CHANZO: MWANANCHI
Naibu Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Ngosi Mwihava aliwataka Watanzania kushiriki katika vita dhidi ya uhujumu uchumi na kwamba juhudi za Serikali za kupambana na wanaotorosha madini nje ya nchi haziwezi kufanikiwa bila ushiriki wa umma kwa kutoa taarifa kwa vyombo na mamlaka husika.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment