Waziri Mkuu, Mizengo Pinda 
            
    
Alitoa uthibitisho huo juzi akiwa London, Uingereza 
ambako yuko katika shughuli za kikazi. Hatua hiyo inaondoa uvumi ambao 
umekuwapo kwa takriban miezi mitatu sasa kwamba naye tayari ameingia 
katika kinyang’anyiro hicho.
Siyo tetesi tena. Sasa ni rasmi 
kwamba Waziri Mkuu, Mizengo Pinda ambaye amekuwa akitajwa kuwania urais 
amethibitisha wazi kuwa atagombea kiti hicho katika uchaguzi mkuu 
mwakani.
Alitoa uthibitisho huo juzi akiwa London, 
Uingereza ambako yuko katika shughuli za kikazi. Hatua hiyo inaondoa 
uvumi ambao umekuwapo kwa takriban miezi mitatu sasa kwamba naye tayari 
ameingia katika kinyang’anyiro hicho.
Pinda aliweka wazi nia ya kuelekea Ikulu 
akisisitiza kuwa hajatangaza rasmi lakini akasema kuwa ameanza harakati 
hizo ‘kimyakimya’. Alikuwa akijibu moja ya maswali aliyoulizwa katika 
Kipindi cha Dira ya Dunia kinachorushwa na Shirika la Utangazaji la 
Uingereza (BBC).
Alitamka rasmi kuwania nafasi hiyo baada ya 
kuulizwa kuwa anafikiri ni kiongozi gani anayefaa kurithi mikoba 
itakayoachwa na Rais Jakaya Kikwete.
“Mikoba ya Rais Kikwete inaweza kuchukuliwa na 
yeyote atakayeonekana mwisho wa safari kwa utaratibu wa chama na ndani 
ya Serikali .... kama anafaa. Waliojitokeza sasa ni wengi na mimi 
ninadhani ni vizuri,” alisema Pinda.
Alipoulizwa kama yupo miongoni mwa wengi alisema, 
“… umesikia kama nimo … basi tukubali hilo na yeye Waziri Mkuu yumo. Hao
 wote waliojitokeza pamoja na Waziri Mkuu aliyejitokeza ni katika 
jitihada za kusema hebu Watanzania nitazameni je, mnaona nafaa au 
hapana?”
“……..fanyeni hivyo kwa mwingine na mwingine, 
mwisho wa yote zile kura zitakazopatikana kwenye mkutano mkuu kama ni 
kutokana na chama kile kinachotawala na hatimaye Watanzania 
watakaojitokeza kupiga kura Oktoba kutokana na wagombea watakaojitokeza 
kutoka kwenye vyama mbalimbali huyo ndiye tutakayempata kama rais. Hivyo
 natangaza nia hiyo kimyakimya.”
Kiongozi huyo atakuwa wa pili kutangaza nia hiyo 
kupitia vyombo vya habari vya kimataifa, baada ya Naibu Waziri wa 
Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba.
Alitangaza nia hiyo Julai 2, 2014, alipokuwa 
Uingereza katika mkutano wa sekta ya mawasiliano baada ya kuhojiwa 
kwenye kipindi hicho hicho cha Dira ya Dunia.
Urais CCM
Kuingia kwa Pinda katika mbio za urais kupitia CCM
 tayari kumebadili mwelekeo wa kinyang’anyiro cha nafasi hiyo kubwa ya 
uongozi nchini kutokana kuzigawa baadhi ya kambi za wagombea ambao 
walikuwa wakitajwa kwa muda mrefu kabla yake.
Wengine ambao wamekuwa wakitajwa kuwania nafasi 
hiyo kupitia CCM ni Waziri Mkuu wa zamani Edward Lowassa, Waziri Mkuu 
Mstaafu Frederick Sumaye, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), 
Profesa Mark Mwandosya, Mbunge wa Songea Mjini, Dk Emmanuel Nchimbi na 
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe. Wengine ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Uhusiano na Uratibu), 
Steven Wassira, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta,
 Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba, Mbunge wa Sengerema, William 
Ngeleja na Mbunge wa Nzega, Dk Hamis Kigwangalla.
                
              
Nguvu ya Pinda
Manung’uniko
Nguvu ya Pinda
Baadhi ya wapiga debe wa Pinda wakiongozwa na 
Mwenyekiti wa Mamlaka za Mitaa Tanzania (Alat), ambaye pia ni Meya wa 
Jiji la Dar es Salaam, Dk Didas Masaburi, wamekuwa wakiweka kambi zao 
Dodoma kila kunapokuwa na vikao rasmi vya CCM ili kuwashawishi wajumbe 
wa vikao vya juu vya chama hicho wamuunge mkono.
Wakati wa vikao vya CC na NEC vya CCM 
vilivyomalizika wiki iliyopita mjini Dodoma, kundi la wafuasi wa Pinda 
likiongozwa na Dk Masaburi lilikuwa mjini humo kuendelea na jitihada za 
kusaka wafuasi.
Harakati hizo zinaweza kuwa ndiyo maana ya kauli 
ya Pinda pale aliposema kwamba tayari ametangaza ‘kimyakimya’ nia yake 
ya kugombea nafasi hiyo.
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), 
Dk Benson Bana anaunga mkono msimamo wa Pinda na wengine waliojitangaza 
katika chama chake huku akivilaumu vyama vya upinzani kwa wagombea wao 
kukaa kimya badala ya kujitokeza ili wananchi wawapime kama wa CCM 
wanavyofanya.
Kuhusu Pinda, Dk Bana alisema: “Ni mzoefu amekaa 
Ikulu muda mrefu na kwa wadhifa wake, si vibaya kujitangaza kwani 
anayejitangaza wananchi wanapata muda wa kumpima na chama pia kinampima 
tofauti na wale ambao hawajitangazi ambao ni hatari sana kwa kuwa 
wanapita chinichini kutoa rushwa.”
Kuhusu upinzani, alisema: “Sijui upinzani wana 
matatizo gani, ningefurahi kuona (Halima) Mdee, (John) Mnyika au 
(Willbrod) Dk Slaa wanajitokeza ili wananchi wawapime kwani Dk Slaa wa 
2010 siyo Dk Slaa wa sasa. Wakijitokeza italeta uhai kwenye hizi 
harakati na wananchi watakuwa na nafasi nzuri ya kuwapima,” alisema na 
kuongeza: “Upinzani wanapokaa kimya wanatunyima fursa wananchi 
kuwapima.”
Manung’uniko
Tangu kuanza kwa tetesi kwamba Pinda ameingia 
katika kinyang’anyiro cha urais, kumekuwa na malalamiko ya chinichini 
dhidi yake kwamba amekuwa akicheza rafu kama ambazo ziliwafanya na 
makada wenzake wenye nia sawa na yake kufungiwa na Kamati Kuu ya CCM.
Itakumbukwa kwamba makada sita wa chama hicho 
ambao ni Sumaye, Lowassa, Membe, Makamba, Wasira na Ngeleja wanatumikia 
adhabu na wapo chini ya uangalizi wa chama hicho baada ya kutiwa hatiani
 kwa makosa ya kuanza kampeni za urais kabla ya muda kutangazwa.
Baadhi ya wagombea na makada wa CCM wamekuwa 
wakidai kuwa Pinda naye anacheza rafu hivyo kutaka ashughulikiwe, lakini
 wengine wamekwenda mbali zaidi na kuhoji ushiriki wake katika Kikao cha
 Kamati Kuu ambacho kilitoa adhabu hiyo ilhali akijua kwamba naye 
atakuja kugombea.
Makamba, Kigwangalla 
Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na 
Teknolojia, January Makamba na Mbunge wa Nzega, Dk Hamisi Kikwangalla 
wamesema wanamkaribisha Waziri Mkuu Mizengo Pinda katika mpambano wa 
kuwania safari ya kwenda Ikulu kupitia CCM.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti jana, Makamba na 
Kigwangalla walionekana kutostushwa na uamuzi wa Pinda kuingia rasmi 
katika mbio hizo huku wakisema siyo tishio kwao.
Makamba kwa upande wake alisema hakuna cha ajabu 
kwa Pinda kuwania nafasi hiyo kwani 1995 alijitokeza Cleopa Msuya ambaye
 alikuwa pia waziri mkuu kupambana na mawaziri wengine kama Jakaya 
Kikwete na Edward Lowassa lakini alishindwa na Benjamin Mkapa ambaye 
alipitishwa.
Alisema pia mwaka 2005 alijitokeza Waziri Mkuu, Frederick Sumaye dhidi ya mawaziri wengine wadogo, lakini walimshinda.
“Mara zote hizo wagombea wengine walifanikiwa 
dhidi ya mawaziri wakuu. Nafasi za madaraka ya kiserikali hazina nafasi 
katika uteuzi wa wagombea ndani ya CCM,” alisema Makamba.
Makamba ambaye pia ni Mbunge wa Bumbuli alisema 
anamkaribisha ili wapimane ubavu lakini akasema ni muhimu kuanzia sasa 
hadi Mei mwakani, harakati hizo zisiathiri kazi za Serikali hasa 
ikizingatiwa kuwa Pinda ndiye msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali.
Dk Kigwangalla ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati 
ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) inayosimamia
 Ofisi ya Waziri Mkuu alisema haogopi mgombea hata mmoja, hata akiwa na 
cheo kikubwa au kidogo kwake si tishio.
“Waziri Mkuu anakaribishwa kwenye mbio hizi na 
asifikiri zitakuwa rahisi kwani watu tumejipanga na tuna mikakati ya 
kushinda,” alisema Kigwangalla.
Hata hivyo, Dk Kikwangalla alisema kuingia kwa 
Pinda kunaweza kuharibu mchakato mzima kwenye chama kwa kuwa ni mmoja wa
 watu wanaotoa uamuzi hasa ikizingatiwa kuwa kwa nafasi yake, anaingia 
kwenye Kamati Kuu na Halmashauri Kuu.
“Waziri Mkuu yuko kwenye nafasi ya kutuchuja, 
hivyo ni kama kusema refa ameamua kucheza kitu ambacho ni tatizo. 
Kitendo cha kutaka uongozi katika nafasi kama yake kitaondoa usawa,” 
alisema Dk Kikwangalla.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment