Social Icons

Pages

Monday, June 01, 2015

WAKUU EAC: UCHAGUZI BURUNDI UAHIRISHWE

Katibu Mkuu wa EAC, Dk. Richard Sezibela.
Wakuu  wa nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), wameishauri serikali ya Burundi kusogeza mbele mwezi mmoja na nusu uchaguzi mkuu nchini humo.
Uchaguzi wa wabunge ulitarajiwa kufanyika Ijumaa wiki hii na wa urais ukipangwa kufanyika mwezi huu. Hatua hiyo imetokana na kutoimarika kwa hali ya amani na utulivu kufuatia baadhi ya vyama vya upinzani na mashirika yasiyo ya kiserikali kuendelea na maandamano kupinga hatua ya Rais wa nchi hiyo, Pierre Nkurunziza, kutangaza kuwania urais kwa muhula wa tatu.
Taarifa ya kuomba kusogezwa mbele kwa uchaguzi huo ilitolewa jana na wakuu wa nchi hizo katika mkutano wao uliofanyika jana jijini Dar es Salaam. Katibu Mkuu wa EAC, Dk. Richard Sezibela, alisema  wakuu hao waliishauri serikali ya Burundi kusogeza uchaguzi huo kutokana na nchi hiyo kutotengemaa kisiasa.
Alisema wakuu hao pia walitoa wito kwa makundi yenye silaha kuziweka chini. Pia, waliishauri serikali ya Burundi  kuwarejesha raia wake wote waliokimbilia nchi jirani.
Kadhalika, walitoa wito kwa serikali ya nchi hiyo kukutana na makundi hayo ili kurejesha amani na utulivu. Dk. Sezibera alisema wakuu wa EAC pia walitoa wito kwa wadau wa amani ukiwamo Umoja wa Mataifa (UN) na Umoja wa Afrika (AU), kuingilia kati mgogoro huo.
Waliohudhuria mkutano huo ni Mwenyekiti wa AEC, Rais Jakaya Kikwete (Tanzania); Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta; Rais wa Uganda, Yoweri Museveni huku Rais wa Afrika Kusini, Jacob Zuma, akihudhuria kama mlezi wa Burundi.
Rwanda iliwakilishwa na Waziri wake wa Mambo ya Nje, Valentine Rugwaiza huku Burundi ikiwakilishwa na Waziri wa Mambo ya Nje, Allen Nyamizwe.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: