Social Icons

Pages

Thursday, May 28, 2015

SHULE ALIOSOMA PINDA YAPIGWA JEKI MILIONI 6.5/-

Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, amepokea msaada wa vitabu 895 vyenye thamani ya Sh. milioni 6.5/- ikiwa ni jitihada ya wadau mbalimbali kuchangia Shule ya Msingi aliyosoma ya Kakuni iliyoko kijiji cha Kibaoni Wilaya ya Mlele mkoani Katavi.
Pinda alipokea msaada huo juzi kwenye Shule mpya ya Msingi Kakuni ambayo bado inaendelea kujengwa kwenye kijiji cha Kibaoni. Akizungumza katika hafla hiyo fupi baada ya kupokea msaada huo, Waziri Mkuu aliishukuru kampuni ya General Booksellers Ltd ya Dar es Salaam kwa msaada huo ambao alisema utachangia kwa kiasi kikubwa kutimiza ndoto yake aliyokuwa nayo ya kuisaidia jamii iliyomsomesha.
“Wazo la ujenzi wa Shule mpya ya Msingi Kibaoni lilitokana na ukweli kwamba nilisoma na kumaliza kwenye shule hii ya Kakuni. Nikiwa ni mtumishi wa serikali, Mbunge na sasa Waziri Mkuu, nilijiuliza hivi shule hii ninaweza kuiacha hivi hivi?,” alisema na kuhoji.
Aliongeza: “Nilijiuliza sana, ni jambo gani ambalo naweza kulifanya la kusaidia wanakijiji wenzangu na kata nzima ya Kibaoni kama shukrani kwa kunilea na kunifikisha hapa nilipo. Ndipo wazo la kujenga shule niliyosoma likazaliwa kama mwaka mmoja na nusu uliopita,” alisema Pinda wakati akiwahutubia wazazi, walimu na wanafunzi.
Awali, akiwasilisha msaada huo, mwakilishi wa kampuni ya General Booksellers Ltd, Bw. Joachim Masaburi alisema wameamua kuchangia vitabu hivyo kwa kutambua umuhimu wa elimu kwa watoto lakini pia wanatambua juhudi za serikali za kutoa elimu bora.
Akitoa mchanganuo wa vitabu hivyo, Masaburi alisema: “Kuna vitabu 600 kwa ajili ya shule ya awali ambavyo kati yake, 300 ni vya ngazi ya chini (nursery) na vitabu vingine 300 ni vya ngazi ya juu (pre-school). Vyote ni vya hisabati, Kiingereza na sayansi."

CHANZO: NIPASHE

No comments: