Social Icons

Pages

Thursday, April 02, 2015

KIONGOZI WA WAFANYABIASHARA APATA DHAMANA


Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA)
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Dodoma Mjini, Roda Ngimilanga, imemrudishia dhamana Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara nchini, Johnson Minja. Hatua ya kumfutia dhamana mfanyabiashara huyo ilizua mjadala mkali bungeni juzi, baada ya wabunge wengi kuilalamikia na kuituhumu serikali kwamba inahusika kuishawishi mahakama kuchukua hatua hiyo. Wabunge hao walitaka Minja arudishiwe dhamana yake ili kuwezesha kufanyika kwa majadiliano kati ya serikali na wafanyabiashara ambao walikuwa wamegoma na kufunga maduka katika sehemu mbalimbali za nchi kushinikiza kiongozi wao arejeshewe dhamana yake. Mahakama hiyo ilimfutia dhamana kiongozi huyo wa wafanyabiashara na kuamuru awekwe rumande kwa muda wa wiki moja kwa tuhuma za kuvunja kanuni za dhamana aliyopewa na mahakama hiyo Januari 28, mwaka huu.
Jana baada ya kusikiliza hoja zilizowasilishwa mahakamani hapo na  pande za utetezi na Jamhuri, Hakimu Ngimilanga alieleza kuwa Mahakama haioni sababu yoyote ya kuendelea kumshikilia Minja gerezani, kwani madai yaliyowasilishwa na Mwendesha Mashitaka wa Serikali, Rose Shio, hayana mashiko ya kisheria ya kumuondolea dhamana Minja.
Aidha, alisema kuwa kwa mujibu wa jalada la kesi hiyo, hakuna kifungu chochote cha dhamana ambacho mtuhumiwa amekivunja na kwamba kwa mujibu wa masharti ya dhamana husika, hakuna kifungu chochote kinachomkataza Minja kufanya mkutano na wanachama wake. “Baada ya kusikiliza hoja za pande zote mbili na kupitia jalada la kesi, ninatamka kuwa Minja ataendelea kuwa huru kwa masharti ya dhamana yake ya Shilingi milioni nne na wadhamini wawili,” alisisitiza Hakimu Ngimilanga.
Kadhalika, alisema kuwa masharti mengi yanayodaiwa kuwa chanzo cha kufutwa kwa dhamana ya mtuhumiwa katika kesi iliyosomwa mahakamani hapo wiki moja iliyopita, hayakuandikwa katika jalada la kesi hiyo. Shio aliitaka Mahakama kuendelea kumshikilia mshtakiwa kwa tuhuma kwamba hali ya amani nchini bado siyo shwari kutokana na migomo ya wafanyabiashara inayoendelea maeneo mengi nchini.
Pia Shio alidai kuwa wafanyabiashara wengi bado wanaigomea Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kutumia mashine maalum ya kufanyia malipo  (EFD). Kwa upande wake, Wakili wa Minja, Godfrey Wasonga, aliieleza Mahakama kuwa kwa mujibu wa ibara (13 (6) b na 15 (1) za Katiba ya nchi, mteja wake hakustahili kufutiwa dhamana na kuwa  jukumu la kuhakikisha kwamba wafanyabiashara wanafungua maduka siyo la mteja wake, bali la Jeshi la Polisi.
Hata hivyo, mwanasheria huyo aliiambia Mahakama kuwa kama kweli mteja wake alikuwa na makosa ambayo yalisababisha kufutiwa dhamana, Polisi walitakiwa kumkamata wakati ule ule walipobaini akiwa katika mwendelezo wa kufanya makosa hayo. Hakimu huyo aliahirisha kesi hiyo kwa ajili ya kutajwa hadi Aprili 9, mwaka huu huku  Jeshi la Polisi likiendelea na upelelezi.
 
HALI ILIVYOKUWA
Kabla ya kuanza kwa kesi, idadi kubwa ya wafanyabiashara kutoka maeneo mbalimbali nchini walikusanyika kwenye eneo la Mahakama, wakisubiri kuletwa kwa Mwenyekiti wao huku polisi waliovaa sare na makachero wakiwa wamelizunguka eneo hilo kuimarisha ulinzi. Kabla mahakama hiyo haijamrejeshea dhamana mshtakiwa huyo, maduka katika maeneo kadhaa nchini yalikuwa yamefungwa.
Waziri wa Fedha, Saada Mkuya, aliwataka wafanyabiashara kufungua maduka yao wakati serikali ikiendelea kushughulikia tatizo hilo. Alisema tayari kamati imeshaundwa kushughulikia malalamiko yao na kwamba wanapaswa  wasubiri  badala  ya  kufunga maduka.
CHANZO: NIPASHE

No comments: