
Waziri Mkuu Mstaafu Frederick Sumaye akiwa na mkewe Esther pamoja na
aliyekuwa Mbunge wa Ubungo, Charles Keenja akielekea katika mkutano wake
wa kutangaza nia ya kugombea urais kupitia CCM, Dar es Salaam jana.
Waziri Mkuu wa
zamani, Frederick Sumaye ametangaza nia ya kuwania urais kupitia CCM,
huku akibainisha kuwa amejipima, ametafakari na kujiridhisha kuwa
anatosha kushika wadhifa huo wa juu nchini.
“Kama kuna mtu mwingine amekamilika kuliko mimi
niambieni na nitampisha (katika mbio za urais),” alisema Sumaye wakati
akitatangaza nia hiyo jana jijini Dar es Salaam mbele ya wanahabari,
akitumia takriban saa moja na nusu kueleza sifa za Rais ajaye na
vipaumbele vyake.
Sumaye, mmoja wa makada sita waliokuwa wamefungiwa
na CCM kwa kukiuka taratibu za kampeni, alikuwa Waziri Mkuu kwenye
Serikali ya Awamu ya Tatu kwa kipindi chote cha miaka kumi na pia
alikuwa mbunge wa Hanang hadi alipoamua kutogombea nafasi hiyo mwaka
2010.
Waziri huyo mkuu wa zamani amekuja na kauli mbiu
ya Uongozi Bora: Komesha Rushwa, Jenga Uchumi, huku akibainisha
vipaumbele vyake kuwa ni pamoja na kujenga na kuimarisha uchumi.
Vipaumbele vingine ni kulinda Muungano,
mshikamano, amani na utulivu na kuboresha huduma za kijamii na maisha ya
Watanzania, kupambana na maovu ya rushwa, ufisadi, dawa za kulevya,
mauaji ya kishirikina, uhusiano wa kimataifa na masuala muhimu ya
uhifadhi wa mazingira, kilimo, ajira, ulinzi wa rasilimani na michezo na
utamaduni.
Sumaye alisema Watanzania wanataka Rais
anayetambua uzito wa kazi iliyopo mbele yake na wananchi wote na awe
tayari kuwa Jemedari wa Jeshi hilo ili kupata ufumbuzi wa matatizo yao
yanayowakabili.
Alisema wananchi wengi wanamfahamu kwa utendaji
wake naye anajua wanachokihitaji na sifa za Rais wanayemhitaji, hivyo
yeye ndiye anayefaa kwa nafasi hiyo. “Mtu anayetaka kuwa Rais ni lazima awe tayari
kujipima, kutafakari, ajiridhishe, kuwa anatosha kiafya, kiakili,
kimaadili na kidhamira kuwaongoza Watanzania. “Kama kuna mtu anapungukiwa kimojawapo, hana sifa
za kuwaongoza Watanzania,” alisema Sumaye huku akishangiliwa na baadhi
ya wafuasi waliomsindikiza katika mkutano huo uliofanyika Hoteli ya
Hyatt Regency.
Alisema kiongozi huyo awe tayari kupimwa na umma vigezo hivyo na siyo ajipime na kwamba yeye yupo tayari kupimwa na umma. Katika hotuba yake hiyo iliyokuwa ikirushwa na
baadhi ya televisheni na redio nchini, alisema Watanzania wanahitaji
Rais atakayekuwa mtumishi wa kuwaongoza na siyo bosi, na pia awe mtu
atakayewaongoza kwa uadilifu.
Sifa nyingine za kiongozi huyo ni kuwa mzalendo wa
dhati anayejua Watanzania walipotoka, wanapopitia na wanakoelekea;
mwaminifu, mjasiri, mtiifu wa sheria na katiba na anayeheshimu mipaka ya
cheo chake. “Tunamtaka Rais mwenye msimamo na anayekubali kushauriwa, aliye
tayari kutengeneza Serikali inayowajibika kwa umma na atakayelinda
masilahi ya umma na siyo masilahi yake na rafiki zake,” alisema Sumaye. Mbunge huyo wa zamani wa Hanang, alisema Rais
anatakiwa kuwa na uwezo mkubwa wa kusimamia na kukuza uchumi nchini kwa
kuondoa matabaka kati ya walionacho na wasionacho.
Aliongeza kuwa Rais ajaye anatakiwa kutoa huduma stahiki za jamii kwa kuondoa matabaka katika kupata elimu na afya bora.
Kwa nini katangazia Dar?
Awali akianza hotuba yake, Sumaye aliyewahi
kugombea urais mwaka 2005 wakati Jakaya Kikwete aliposhinda na baadaye
kuchaguliwa kuwa Rais wa Serikali ya Awamu ya Nne, alisema ameamua
kutangazia nia yake jijini Dar es Salaam kwa sababu anataka kura za
wananchi wote siyo tu wananchi wa maeneo ambako anatokea kama
wanavyofanya watangazania wengine.
“Sitaki watu wa Hanang’ wanipe kura kwa sababu
mimi ni wa kwao au wa Musoma waninyime kura waseme huyo siyo wa kwetu,
mimi ni wa Tanzania nzima na kazi hii ni ya Watanzania wote.
Nimetangazia Dar es Salaam kwa kuwa ni mji mkuu kwa maana ya majiji,”
alisema.
Sumaye alisema ana uzoefu wa kutosha katika nafasi
mbalimbali za uongozi wa kisiasa na kiserikali kwa kuwa mbunge, naibu
waziri na hatimaye Waziri Mkuu kwa miaka kumi katika utawala wa Rais
Benjamin Mkapa. Alitumia muda huo kubainisha mafanikio mbalimbali
waliyoyapata akiwa Waziri Mkuu, yakiwamo ya kupunguza mfumuko wa bei
kutoka asilimia 27 hadi asilimia 4.1 na kuongeza ukusanyaji wa mapato
kutoka Sh27 bilioni kwa mwezi hadi Sh200 bilioni.
Alisema walipambana kwa hali na mali kuondoa
vitendo vya rushwa kwa kuanza na kuunda tume za kupambana na rushwa na
kuanzishwa utaratibu wa wananchi wa kupiga Kura ya Maoni kwa watu
wanaowahisi ni wala rushwa, jambo lilisababisha watumishi wengi wa
Serikali wasimamishwe au kustaafishwa kwa maslahi ya umma.
Sumaye, ambaye katika hotuba yake alikuwa
akikemea rushwa mara kwa mara, alisema yeye ni mwadilifu asiyehusishwa
na tuhuma zozote za kifisadi tofauti na wanasiasa wengine wanaokemea
ufisadi bila kuonyesha kwa vitendo. “Leo unasikia mgombea anasema hatutaki kiongozi
masikini. Unaomba urais kwa Watanzania masikini halafu unasema hatutaki
kiongozi masikini… hakutaka tu kusema tunataka kiongozi tajiri,”
alisema.
“Unasema mimi siyo tajiri lakini unatafuta nafasi
ya kwenda Ikulu utafikiri utajiri unapatikana huko. Kama unataka utajiri
nenda kafungue kampuni ufanye biashara na kukimbizana na polisi,”
alisema Sumaye bila kumtaja mgombea aliyekuwa akimzungumzia.
Alisema akipata ridhaa ya kuwa Rais, atapambana na maovu ya
ufisadi na rushwa kwa kuunda chombo maalumu kitakachokuwa kikifanya
uchunguzi wa rushwa, ufisadi na uhujumu uchumi. “Chombo hiki kitachunguza kwa wiki na baadaye
kukufikisha mahakamani. Baada ya wiki moja au mbili unahukumiwa, kama ni
viboko au kwenda jela,” alisema Sumaye.
Akielezea kwa undani vipaumbele vyake, Sumaye
alisema atatekeleza ilani ya CCM kikamilifu na kuhakikisha anasimamia
ukuzaji wa uchumi kwa kuwa ndiyo msingi wa mafanikio wa kila nyanja ya
maisha ya mwanadamu. Alisema uchumi umekuwa ukikua kwa namba, lakini
hauwagusi watu wa vijijini ambao ni masikini wa kutupwa, hivyo yeye
atahakikisha unauimarisha katika maeneo yote ya vijijini na mijini kwa
kuimarisha kilimo na viwanda. Sumaye alisema huwezi kuboresha afya na elimu bila
kuwa na msingi imara wa kupata mapato stahiki na mgawanyo mzuri wa
rasilimali kwa Watanzania wote.
Waziri huyo wa zamani wa Kilimo na Mifugo alisema
atahakikisha mfumo mzima wa kilimo unaimarika na siyo kuimarisha sehemu
moja ya kuleta matrekta nchini wakati huduma zinazochangia uzalishaji
kama mbegu, utafiti, mfumo mzuri wa utunzaji mazao zinazorota.
“Siyo kama nakosoa kuhusu matrekta kwa sababu hata
wakati wa utawala wa Mwalimu Julius Nyerere yalikuwepo, lakini
hayakufanya kazi kiufanisi. Unaweza ukawa na trekta likalima ekari 50,
lakini una uwezo wa mbegu za ekari tatu, kupalilia na kuhifadhi mazao
kwa kiwango hicho. Ila mimi nikipata ridhaa nitaboresha hayo na kutafuta
masoko ya uhakika,” alisema huku akishangiliwa. Pia, alibainisha kuwa atahakikisha anakuza na
kulinda viwanda vya ndani ili kuzuia Tanzania kuwa dampo la bidhaa za
nje zisizohitajika. “Ni muhimu kuendeleza viwanda ili kuongeza
uzalishaji wa bidhaa na huduma kwa ajili ya matumizi ya ndani na bidhaa
za kuuza nje ya nchi ili kuongeza utajiri kwa fedha za kigeni,” alisema.
Kuhusu suala la ajira, Sumaye alisema atahakikisha
anatoa elimu bora ya ufundi katika ngazi za chini hasa kwa kuweka
mikondo ya ufundi katika shule za kata na pia kuongeza uwekezaji katika
viwanda vidogo vya kuongeza mazao ya kilimo na kuwekeza katika kilimo
kutaondoa tatizo la vijana kutokuwa na kazi.
“Mfumo wetu unawaandaa vijana kuendelea na elimu
ya juu badala kuwawezesha kuwa na uwezo wa kumudu changamoto za maisha
kwa kila hatua ya kielimu anayoifikia mwanafunzi. Hivyo uzalishaji wa
madarasa ya ufundi katika shule zetu utakuwa muhimu ili vijana
kujiajiri,” alisema.
Kuhusu huduma za jamii alisema kipaumbele chake ni
kuweka elimu bora kwa watu wote kwa kuhakikisha anatafuta rasilimali za
kutosha zitakazosaidia kuondoa mwanya wa walichonacho na wasionacho. “Tunataka shule nzuri za Serikali ambazo zitachukua vijana wenye
akili kutoka vijijini ili waweze kusoma bila kujitofautisha na shule
binafsi, hospitali nzuri ambazo Watanzania wanaweza kupata huduma bora
muda wote…mtu akishindwa kutibiwa Aga Khan basi akienda Mwananyamala
atibiwe bila kuona tofauti,” alieleza.
Asisitiza dhamira ya kuihama CCM
CHANZO: MWANANCHI
Sumaye alitumia pia mkutano huo kupangua tuhuma
mbalimbali za kashfa dhidi yake na utawala wake, zikiwemo ununuzi wa
rada, ubinafsishaji wa nyumba za serikali, umiliki wa ardhi, uuzwaji wa
benki ya NBC, ununuzi wa mgodi wa makaa ya mawe ya Kiwira na sakata la
Meremeta.
Kuhusu masuala hayo, alisema Watanzania wanapaswa
kutofautisha uamuzi wa serikali na wizi na sehemu kubwa ya mambo hayo
yalikuwa ni uamuzi wa Serikali na chama, hasa sera ya ubinafsishaji.
“Nilishawahi kuyatolea maelezo yote haya. Suala la
rada lilikuwa muhimu sana. Ukumbuke nchi ilikuwa haina chombo cha
kuongozea ndege…ilikuwa ni hatari kwa usalama wa nchi na sekta ya anga,”
alisema Sumaye akizungumzia suala hilo la ununuzi wa rada kwa bei ya
juu kulinganisha nay a sokoni. “Mashirika makubwa ya ndege yalishaanza
kukataakutua nchini. Hata jeshi halikuwa na rada. Hali ilikuwa mbaya.
Suala la ununuzi lilihusisha wataalamu hata mimi sikuiona inafananaje na
hata Mzee Mkapa haijui ikoje. “Kama mtu aliiba ni jambo jingine. Kama mtu amebainika aliiba, Serikali imchukulie hatua.”
Katika sakata hilo, Bunge la Uingereza lilihoji
sababu za nchi maskini kama Tanzania kununua rada kwa bei kubwa na
baadaye kuagiza uchunguzi ambao ulibaini kuwapo ufisadi wa kupandisha
bei kwa hila. Iliagizwa fedha hizo zirejeshwe nchini.
Asisitiza dhamira ya kuihama CCM
Alipoulizwa iwapo ataendelea na msimamo wake wa
kukihama chama hicho kama ambavyo amekuwa akinukuliwa na vyombo vya
habari kwamba kama CCM itamteua mgombea mla rushwa katika Uchaguzi Mkuu
wa mwaka huu, Sumaye alisema “hawezi kushirikiana na wala rushwa”.
“Nitatoka CCM, ndiyo…kama huwezi kuungana nao utabakiaje? Ila naamini
chama changu hakitamchagua mla rushwa na ndiyo maana sitegemei kutoka
kwa sababu hawatachagua mla rushwa,” alisema.
Kuhusu ubinafsishaji wa mashirika ya umma ambao ni
moja ya masuala ambayo Serikali yake na rais Mkapa ilinyooshewa vidole,
Sumaye alisema alikuta sera zilizopitishwa na CCM na Serikali, hivyo
hatakiwi kulaumiwa kwa kutekeleza yalikuyokubaliwa na mfumo.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment