Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira (kushoto)
akizungumza alipokuwa akifanyiwa mahojiano maalumu na waandishi wa
gazeti la Mwananchi, ofisini kwake Dar es Salaam.
Waziri wa
Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira amewakosoa baadhi ya vigogo
wanaojinasibu kuanzisha programu ya shule za sekondari za kata nchini
akisema ni ujinga kusema hivyo kwa kuwa miradi yote hufanywa na Serikali
na siyo mtu binafsi.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na Mwananchi
ofisini kwake juzi, Wasira alisema wazo la kujenga sekondari kila kata
ni ahadi ya CCM katika ilani ya mwaka 2005 na si wazo la mtu mmoja kama
inavyodaiwa. Huku akitumia nadharia ya uendeshaji Serikali,
Wasira alisema miradi yote ya maendeleo inafanywa kwa pamoja na kwamba
kama ni kuihusianisha na mtu mmoja, basi mwenye sifa hiyo ni Rais.
Kauli ya Wasira ilikuja baada ya kuulizwa juu ya
changamoto mbalimbali zinavyoikabili nchi na masuala ambayo rais ajaye
anatakiwa kufanya ili kuiletea nchi maendeleo.
“Mtu anayesema alijenga sekondari za kata
anawadanganya Watanzania. Ile kitu ipo kwenye ilani ya CCM… jitihada na
sifa za kujenga sekondari huwezi kuzihamisha kutoka kwa rais anayeongoza
nchi na kusema waziri mmoja tu ndiyo anahusika, nakataa kabisa na
yeyote anaweza kuninunia kwa hilo,” alisema Wasira huku akisisitiza
anazungumzia masuala (issues) na siyo kumshambulia mtu.
Alisema Serikali inapoamua kufanya mradi ni jambo
la pamoja na huendeshwa kama familia, hivyo hakuna mtu mmoja katika
baraza anaweza kusema ni la pekee yake kutokana na kuangukia katika
wizara yake.
“Mimi ni waziri wa kilimo, sisi tumeanzisha mambo
mengi ikiwamo kuishauri Serikali ianzishe benki ya wakulima inayoanza
Julai mwaka huu lakini siwezi kusema bila mimi kusingekuwa na benki au
ruzuku kwa wakulima… sasa kila mtu akichukua sifa hizo Rais atachukua
sifa ipi?” alihoji.
Ingawa Wasira hakutaja jina la mtu, Waziri Mkuu wa
zamani, Edward Lowassa amekuwa akihusishwa kusema mara kwa mara kuwa
alikuwa kiungo muhimu katika uanzishwaji wa mpango wa shule za kata
nchini.
Ukawa si tishio
Katika mahojiano hayo ya takriban saa 1.30, Wasira
alipuuza nguvu ya Ukawa kisiasa kwa sasa akisema umoja huo wa Chadema,
NCCR-Mageuzi, CUF na NLD, hauinyimi usingizi CCM kwa kuwa vyama vya
upinzani havina maono ya maendeleo kama ilivyo kwa chama tawala.
Alisema anajua Ukawa ina mbinu na sera zake lakini siyo tishio kwa sababu CCM itakwenda kwa wananchi kwa hoja. “Wenzetu ukiwauliza wana mikakati gani hawana…
huwezi kwenda kwa wananchi kwa kelele tu wakakuchagua… lazima uonyeshe
mwelekeo, unataka kuipeleka nchi yao wapi, kwenye maandamano?
“Nimekaa na vyama hivi sijapata kusikia jambo la msingi la
maendeleo au dira ya maendeleo ya vyama vyao. Hata ukimkamata Mbowe
(Mwenyekiti wa Chadema, Freeman) leo ukimuuliza wewe unataka kuongoza
nchi, utafanya nini... hana lolote la kukwambia,” alisema.
Alisema vyama hivyo vinaongoza kwa kulalamika
badala ya kutafuta majibu ya matatizo yanayowakabili wananchi na kusema,
ifikie kipindi viongozi waache kuwatengeneza wananchi kuwa jamii ya
kulalamika mara kwa mara isipokuwa tu pale Serikali inapotokea kushindwa
kabisa.
Wasira aliyekuwa makini kujibu maswali hayo,
alipoulizwa CCM imejiandaaje kisaikolojia iwapo itashindwa Uchaguzi Mkuu
ujao, alisema imejiandaa kushinda na siyo kushindwa na ikitokea
ikashindwa itajulikana mbele kwa mbele.
Alisema CCM ni chama tawala kilichofanikiwa mambo
mengi ya maendeleo hivyo hakijiandai kushindwa na kwamba ikitokea mtu
anakwenda kugombea akijua atashindwa, basi hana akili. “Unavyokwenda kugombea unakuwa umeshafanya utafiti
kuwa utashinda na hiyo ndiyo nguvu inayowapeleka, lakini kushindwa ni
kama ajali ambayo huwezi kuipanga… sisi tunapanga kushinda, tena siyo
kidogo, bali kwa kishindo na uwezo tunao, nia tunayo na sababu zipo
nyingi,” alisema huku akicheka.
Serikali za Mitaa
Pamoja na kwamba CCM ilipoteza viti vingi kwa
upinzani katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa mwaka jana, Wasira alisema
hilo si tishio na bado anaona kwamba vyama hivyo bado ni dhaifu. Alisema katika uchaguzi huo, CCM ilishinda kwa
kishindo kwa asilimia 80 na kwamba asilimia za upinzani ni halali
kuongezeka kwa kuwa vyama hivyo pia vinakua.
CCM na uteuzi
Akizungumzia kuchelewa kwa kipenga cha kuruhusu
makada wa CCM kuanza mchakato wa kugombea nafasi mbalimbali za uongozi,
Wasira alisema kunatokana na kubadilika kwa taratibu za kichama ambazo
si sheria lakini lazima zifuatwe. “Kuna vyama 22 nchini kwa nini watu wanasema CCM
imechelewa... imechelewa nini mbona hata wanaojiita Ukawa nao kwani
wamemaliza? Kwanza CCM ina watu wengi wanaojulikana hata ukimteua leo
mmoja wao, wananchi watasema ni huyu lakini vyama vingine hata
hawajulikani sana, sasa tatizo lipo wapi?” alihoji Wasira.
Alipoulizwa iwapo kuchelewa huko ni mbinu za
kutegeana na Ukawa kusimamisha wagombea kama inavyodaiwa na wachambuzi
wa mambo, alisema CCM haiwezi kutegea chama chochote. “CCM haina mapatano na chama chochote wala haiwezi kungojea
chama kingine wala kutegea, hatujafika huko. Sisi ni chama kikubwa tukae
tunategea Ukawa hadi lini lakini mkumbuke zile kanuni zinategemea
nafasi.
Uhusiano na uratibu
Kugombea urais
Uchaguzi Mkuu
Ilani ya CCM
“Kulikuwa na mambo mengi hapo mbele kama Kura ya
Maoni Aprili na mambo mengine yaliyotakiwa yapeane nafasi lakini Tume
(NEC), imeamua lipelekwe mbele kwa sababu haijamaliza kuandikisha
wapigakura… sasa ni uamuzi wa chama!
Uhusiano na uratibu
Alipotakiwa kuelezea iwapo kusuasua kwa uhusiano
baina ya Serikali na baadhi ya wadau wengine kama taasisi za kidini
kulisababishwa na yeye kwa kutomshauri vizuri Rais akiwa Wazira wa Nchi,
Ofisi ya Rais, Uhusiano na Uratibu, Wasira alijibu: “Hilo utaamua
mwenyewe.”
Ila alibainisha kuwa kwa miaka yote ya nyuma
kumekuwa na uhusiano mzuri tangu Rais Kikwete aingie madarakani lakini
mambo yamebadilika baada ya kuanza mchakato wa Katiba kutokana na kuwapo
maoni tofauti. “Mahusiano ni mchakato, hakuna kipindi ukasema
yametosha kwa sababu kila siku mambo mapya yanaibuka na huwezi kuzuia
yasije. Ukumbuke mwaka 2010 mambo yalikuwa mazuri lakini baada ya Katiba
vyama vikaja na ajenda zao, taasisi za dini nazo… hivyo Serikali haina
mgogoro wowote na wadau wake,” alisema.
Kugombea urais
Wasira ni miongoni mwa makada wa CCM wanaotajwa
kugombea urais mwaka huu na tayari alishapigwa adhabu ya mwaka mmoja kwa
kuanza kampeni mapema akiwa na vigogo wengine watano wa chama hicho.
Hata hivyo, juzi alipotakiwa kueleza akiwa rais
anatakiwa kufanya nini, alisema asingependa kuzungumza kama mgombea,
bali alisema kwa ujumla kiongozi ajaye anatakiwa kuendeleza mikakati ya
maendeleo ikiwamo dira ya maendeleo ya miaka mitano baada ya ile sasa
kumalizika mwakani.
Alisema japo hamfahamu, alisema rais huyo,
anatakiwa awekeze katika ukuzaji wa kilimo na viwanda ikiwa ni
mwendelezo wa dira iliyopo iliyojikita katika kuondoa vikwazo vya
kiuchumi na biashara kwa kuwekeza kwenye miundombinu.
Alisema Rais Kikwete imefanya mambo mengi mazuri
ya maendeleo yakiwamo kukuza elimu ikiwamo ujenzi wa sekondari za kata,
miundombinu lakini tatizo Watanzania hawataki kuangalia mema. “Hakuna mtu anayeweza kuthibitisha kuwa akiwapo
Rais mwingine hakutakuwa na matatizo. Hata hizo shule za kata
wanazokosoa bado zinasaidia sana na wanafunzi takriban milioni 1.5
wanasoma. “Kama mchumi nafahamu mkiharakisha sana hatua za maendeleo, kuna
wakati mnashusha ubora ila baada ya hapo mnachukua hatua,” alisema
Wasira.
Uchaguzi Mkuu
Mbunge huyo wa Bunda (CCM) naye hakuacha kuwananga
wale wanaonyesha wasiwasi kuwa Uchaguzi Mkuu huenda usifanyike mwaka
huu akidai ni vigumu kuahirisha shughuli kwa kuwa ipo kikatiba na
haiwezi kutokea katika hali ya kawaida.
Alisema kama alivyosema Rais Kikwete wakati wa
maadhimisho ya Mei Mosi, uchaguzi huo utakuwapo na hakuna haja ya watu
kuanza kulalamika wakati bado ni mapema. “Haiwezekani kubadilisha Katiba kirahisi na hakuna
mwenye mamlaka hayo zaidi ya Bunge na kuahirisha siyo jambo la kawaida
labda kuwe na vita. Sasa hao wanaosema utaahirishwa wamepata wapi hayo
maneno? Wanazidi kuwafanya wananchi kuwa watu wa kulalamika.”
Ilani ya CCM
Wasira ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya kuandaa
Ilani ya Uchaguzi ya chama hicho mwaka 2015 - 2020, alisema wanaendelea
vizuri shughuli hiyo huku akikataa kueleza mambo ya msingi
yatakayozingatiwa.
Baada ya kukamilisha rasimu ya hiyo, alisema
watapeleka kwa mamlaka zilizowaagiza ambazo ni Kamati Kuu (CC) na
Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kwa maboresho zaidi na kuipitisha tayari
kwa ushindi wa kishindo.
Hata hivyo, Wasira alipotakiwa kueleza iwapo
kuchaguliwa kwake katika kamati hiyo kuna lengo la kupunguza nia yake ya
kugombea urais, alijibu kuwa hakuna kitu kama hicho na kwamba yeye ni
mjumbe wa NEC hivyo ana sifa ya kufanya hivyo.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment