Social Icons

Pages

Monday, May 18, 2015

WABUNGE KUWASHA MOTO BAJETI YA UTAWALA BORA LEO


Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema.
Bunge la Bajeti linaendelea tena mjini hapa leo, baada ya mapumziko mafupi ya mwishoni mwa wiki, ikiwa ni zamu ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora) kuwasilisha hotuba ya makadirio ya bajeti ya wizara yake.Masuala kadhaa ya utawala bora ikiwamo hatua ya Ikulu kuwasafisa baadhi ya vigogo waliotajwa katika kashfa ya fedha za akaunti ya Tegeta Escrow katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT), huenda yakazua mjadala mkali. Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, (Chadema), alipinga kauli ya Waziri Mkuu Mizengo Pinda kudai kuwa Ikulu haijawasafisha baadhi ya vigogo akisema inazua maswali mengi magumu.
“Nimeomba kuchangia wizara hii, hususan, masuala ya utawala bora, inaonekana wengi hawafahamu umuhimu wa jambo hili. “Utawala bora unahusika na utu, maadili, haki za binadamu, maisha ya kesho ya Mtanzania, maisha ya mtumishi wa umma.
“Sidhani kama serikali inafahamu utawala bora wenye maadili, hekima na utawala wenye upendo…tuna tatizo kubwa hapa la rushwa, ufisadi unaofanywa na viongozi wa umma,” alisema na kutaja mfano wa fedha zilizochotwa katika akaunti ya Tegeta iliyofunguliwa BoT ambapo zaidi ya Sh. bilioni 300 zilichotwa.
Alisema pamoja na baadhi ya mawaziri, wabunge na watendaji wengine kuwajibika kutokana na kashfa hiyo, wahusika waliochota fedha hizo kwenye akaunti iliyofunguliwa benki ya Stanbic bado hawajatajwa. Alisema waliochukuliwa hatua ni wale waliopewa mgawo wa fedha hizo, lakini wale/yule aliyeidhinisha fedha hizo zitolewe BoT hajachukuliwa hatua yo yote. “Huo sio utawala bora,” alisema.
Baadhi ya wabunge walishangaa kutochukuliwa hatua ya kusimamishwa mnikulu wa Ikulu Shaban Gurumo ambaye naye alifikishwa mbele ya Baraza la Sekretarieti la Maadili ya Viongozi wa Umma akikabiliwa na kosa la kukiuka maadili kwa kupokea Sh. 80, 850,000.
Mwanasheria wa sekretarieti hiyo, Hassan Mayunga, alidai Gurumo anatuhumiwa kukiuka vifungu mbalimbali vya Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma namba 13 ya mwaka 1995 kama ilivyorekebishwa mwaka 2001. Gurumo ambaye alikuwa Naibu Katibu wa Rais, aliteuliwa kuwa mnikulu Machi 9, 2011 kuchukua nafasi iliyoachwa wazi na marehemu Rajab Kianda aliyefariki Februari 7, 2010.
Masuala ya usawa katika ugawaji wa raslimali za umma na ushughulikiaji wa tatizo la rushwa, muundo na mfumo wa utawala wa sheria na demokrasia, ushirikishwaji, uwakilishi na uwajibikaji yanaweza kuwa moja ya mambo yanayoweza kuzua mjadala mkali baada ya waziri mwenye dhamana, George Mkuchika (pichani) kuwasilisha makadirio ya bajeti kwa mwaka 2015/16.
Katika siku za hivi karibuni, wananchi wengi wameonyesha kutoridhishwa na utendaji katika Jeshi la Polisi na mamlaka za kisheria, masuala kama ya rushwa na ucheleweshaji wa kesi na hata masuala ya kubambikiwa kesi na wanyonge kutopata haki yalijitokeza kwa kiasi kikubwa.
Wiki iliyopita katika hotuba ya makadirio ya bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge, wabunge hususani wa upinzani waliibana serikali kwa kushindwa kumpeleka fedha za kutosha kwenye miradi ya maendeleo. Suala la uchaguzi mkuu pia lilipata nafasi kubwa baada ya wabunge wa upinzani kuishinikiza serikali kutothubutu kuahirisha uchaguzi mkuu Oktoba mwaka huu.
Mjadala kuhusu hotuba hiyo kama ambavyo itakuwa katika wizara zingine utachukua siku mbili kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Habari, Elimu kwa Umma na Uhusiano wa Kimataifa wa Bunge, Jossey Mwakasyuka.
CHANZO: NIPASHE

No comments: