Tangu Februari mwaka 2014, siasa za Tanzania
zimekuwa na mwelekeo chanya kwa vyama vya upinzani kushirikiana, tofauti
na wakati wowote tangu mfumo wa vyama vingi uanzishwe nchini.
Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) umeweza
kuunganisha vyama vitatu vikubwa na chama kimoja kidogo, na kitendo cha
umoja huo kuendelea kuwapo ni mafanikio makubwa.
Haya ni mafanikio makubwa kwa vyama vya siasa vyenye utamaduni wa kisiasa na itikadi tofauti. Ukawa umewafanya wananchi waamini kabisa kuwa
mwisho wa CCM umefikia, kwani kwa muda mrefu wananchi wamekuwa
wakitamani vyama vya siasa kushirikiana.
Ukawa ni umoja ulioundwa kwa ajili ya kushinikiza
kupatikana kwa katiba inayotokana na maoni ya wananchi walio wengi, kama
ilivyoonyeshwa katika taarifa ya Tume ya Marekebisho ya Katiba. Tume hiyo iliyokuwa inaongozwa na Jaji Joseph
Warioba pamoja na mambo mengine, ilipendekeza kuwepo kwa Jamhuri ya
Muungano yenye serikali tatu.
Tafiti mbalimbali zilikuwa zinaonyesha kuwa huu
ndio msimamo wa wananchi wengi. Hata hivyo, CCM walifanikiwa kwa
kutumia nguvu kubwa kuzuia mfumo huo kuanzishwa na hivyo kupitishwa kwa
Katiba Inayopendekezwa, yenye mfumo wa sasa na iliyoondoa maeneo mengi
yenye kujenga mfumo madhubuti wa uwajibikaji nchini.
Ukawa ilijiandaa kushawishi wananchi kutojitokeza kupiga kura ya maoni ya Katiba, lakini hiyo imeahirishwa na hivyo Ukawa kubakia na ajenda kubwa kuhusu Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Ukawa imepanga kuweka wagombea wa ubunge, udiwani na urais kwa kushirikiana. Wakifanikiwa hilo itakuwa ni hatua kubwa ya kimaendeleo katika siasa za Tanzania.
Ukawa ilijiandaa kushawishi wananchi kutojitokeza kupiga kura ya maoni ya Katiba, lakini hiyo imeahirishwa na hivyo Ukawa kubakia na ajenda kubwa kuhusu Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015. Ukawa imepanga kuweka wagombea wa ubunge, udiwani na urais kwa kushirikiana. Wakifanikiwa hilo itakuwa ni hatua kubwa ya kimaendeleo katika siasa za Tanzania.
Kwa mujibu wa Ukawa inayoundwa na vyama vya
NCCR-Mageuzi, CUF, NLD na Chadema, kila chama kitaachiwa maeneo kadhaa
ya kugombea nafasi za ubunge na udiwani. Pia chama kimojawapo katika
vyama hivi kitatoa mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
wa kiti cha urais Zanzibar.
Wasiwasi
Baadhi ya watu wana shaka kubwa na uwezo wa vyama
hivi kuendelea kukaa pamoja, kwa sababu ya maslahi binafsi ya vyama
vyao. Chama cha siasa chochote kina melengo ya kushika dola ili kiweze
kutekeleza sera na mipango yake. Hata hivyo, kwenye demokrasia kuna
uwezekano wa chama zaidi ya kimoja kushika dola kwa kushirikiana, ama
kwa makubaliano ya baada ya uchaguzi au kabla ya uchaguzi.
Mwaka 2010 huko Uingereza, vyama viwili vya siasa
viliunda serikali ya pamoja baada ya matokeo kuonyesha kuwa hakuna chama
kilichoweza kuunda serikali peke yake. Vyama vikubwa nchini humo,
yaani Conservatives na Labour vyote havikuwa na idadi ya wabunge
inayotosha kuunda Serikali.
Ukawa ijifunze haya
Hivyo chama cha tatu kwa idadi ya wabunge bungeni kikaungana na
Conservatives kuunda serikali ambayo ilidumu mpaka mwaka 2015. Safari
hii Chama cha Conservatives kimeunda serikali peke yake. Huu ni mfano wa
ushirikiano wa vyama baada ya uchaguzi.
Mwaka 2002 nchini Kenya kuliundwa ushirikiano wa
vyama ili kukishinda chama cha Kanu na kuunda Serikali. Ushirikiano huo
uliitwa NARC na ulihusisha wanasiasa wote wakubwa wa nchi hiyo. Umoja
ule kimsingi ulikuwa ni ‘Umoja dhidi ya Moi’
Uchaguzi uliofuata kila chama kiliingia serikalini
kivyake na kwa muundo mwingine kabisa wa vyama. Madhara ya umoja ule wa
mwaka 2002 yalikuwa makubwa mno, kwani vurugu za mwaka 2007 zilitokana
hasa na chuki za kikabila kati ya makabila makubwa kulingana na
wanasiasa waliowaunga mkono.
Hapa Afrika mifano mingi ya ushirikiano baada ya
uchaguzi inatokana na vurugu na uchaguzi kuibwa na yote iliishia na
matokeo mabaya kwa vyama vya upinzani. MDC ya Zimbabwe ilitupwa nje na
kukataliwa na wananchi baada ya kukaa madarakani na Robert Mugabe kwa
miaka mitano.
Chama hicho sasa kimevunjikavunjika katika pande
nne na hakina tena ushawishi. ODM ilipoteza madaraka nchini Kenya kwani
ilikuwa ni rahisi kwa wananchi na wachambuzi wa kisiasa kuhusisha
masuala mabaya serikalini na uwepo wa Raila Odinga katika serikali hiyo.
Pia uchaguzi wa 2013 nchini humo ukajengeka kwenye ukabila zaidi na
makabili yenye watu wengi yakashinda uchaguzi huo.
Ukawa ijifunze haya
Mifano hii ndio ambayo Ukawa inapaswa kuitazama na
kuichambua inapoelekea kuunda umoja kabla ya uchaguzi. Chama cha
Wananchi (CUF) chenye nafasi kubwa ya kushinda huko Zanzibar kiasi cha
kutohitaji kabisa Ukawa kinaweza kufutika kabisa upande wa Bara, kama
hakitakuwa makini katika namna ya mgawanyo wa majimbo ya uchaguzi na
nafasi gani watachukua baada ya uchaguzi.
Kwa mujibu wa taarifa za vyombo vya habari, CUF
itaachiwa majimbo takribani 100, na nusu ya majimbo haya yapo Zanzibar.
Hata hivyo, kwa uamuzi huu CUF itapoteza nafasi kubwa sana ya kupata
kura kwa ajili ya mgawo wa wabunge wa viti maalumu na ruzuku za
kuendesha chama chao.
Kwa mujibu wa Sheria ya vyama vya siasa ya mwaka
1992 kama ilivyofanyiwa marekebisho mara kwa mara, chama cha siasa
hupata ruzuku kutokana na moja Idadi ya kura ambazo kila chama kimepata
katika uchaguzi mkuu wa wabunge; pili idadi ya wabunge wa majimbo.
Sifa ya kwanza ni lazima kwanza chama kipate zaidi ya asilimia tano ya kura zote ambazo zimepigwa katika uchaguzi huo.
Hii ndiyo sifa pia ya kupata wabunge wa viti
maalumu. CUF wameachiwa majimbo ya Zanzibar ambayo idadi ya wapiga kura
wake hawazidi wapiga kuwa wa wilaya ya Kahama na pia imeachiwa majimbo
ya Pwani ( Tanga, Lindi, Pwani na Mtwara) ambayo yana wapiga kura
wachache kulinganisha na mshirika wake Chadema.
Hivyo CUF wanaweza kumaliza uchaguzi wa mwaka 2015
wakiwa na wabunge wachache zaidi wa viti maalumu kuliko wakati wowote
ule na pia wakiwa hawana fedha za kuendesha chama chao.
Kwa Chadema, chama ambacho kimetumia miaka mitano kujijenga na
kusambaa kila kona ya Tanzania, ushirikiano huu una faida kubwa kwa
maana ya kuondoa propaganda ya udini na ukabila. Hata hivyo, kukua kwa
kasi kwa chama kipya cha ACT-Wazalendo kutanyofoa kura nyingi kutoka
Chadema.
Kitendo cha Chadema kutoweka wagombea nchi nzima
na ikitokea ACT-Wazalendo wakaweka wagombea nchi nzima na hivyo kuwa
chama kikubwa cha pili kwa idadi ya wagombea ubunge na kuweza kuokota
kura nchini nzima, kunaweza kuifanya kuwa chama cha tatu kwa idadi ya
kura hata kama kitapata wabunge wengi zaidi ya ACT- Wazalendo.
Hii maana yake itasababisha Chadema kuwa na
wabunge wachache wa viti maalumu na vilevile ruzuku ndogo. Chama cha
NCCR Mageuzi kitaendelea kuwa chama kinachosindikiza kutokana na ukweli
kuwa kwa mgawanyo wa majimbo ulivyo hawatapata zaidi ya asilimia tatu ya
kura. NCCR Mageuzi inaweza kubakia na wabunge wawili tu baada ya
uchaguzi mkuu. Hiki ni chama ambacho Ukawa utakifuta katika ramani ya
siasa.
Hata hivyo, kwa ajili ya malengo ya nchi na
kuiondoa CCM madarakani Ukawa bado ni umoja ambao ni muhimu kwa nchi.
Kuendelea kuwepo kwake au la kutatokana na iwapo viongozi wa vyama
watakubali madhara yaliyoainishwa katika makala haya.
Hata hivyo, ni dhahiri kuwa baada ya uchaguzi mkuu
wa mwaka 2015, Ukawa ikiunda serikali au la, vyama hivyo vitagombana
na uchaguzi wa mwaka 2020 utakuwa na ‘hesabu’ tofauti kabisa za
kisiasa. Chama kitakachotoa Rais mwaka 2015, ndicho kitakachodumu
kutokana na kuwa na dola, kwa kuwa ndiyo chombo muhimu katika nchi za
Kiafrika.
Mwai Kibaki wa Kenya ni mfano tosha kabisa.
Ukitaka mfano nje ya Afrika, tazama nchini Uingereza ambapo chama cha
Liberal Democrats kimefutika kutoka wabunge 58 mpaka wabunge wanane tu
ndani ya miaka mitano. CUF wasome zaidi alama hizi kuliko chama kingine
chochote.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment