Pages

Tuesday, May 12, 2015

MKUNGA MWENYE TAALUMA HAWANYANYASI WAJAWAZITO

Ukunga ni taaluma muhimu katika kujenga maisha bora ya jamii kwa sababu ndiyo inayohakikisha usalama wa mama na mtoto kuanzia anapobeba mimba, kujifungua na kuelimisha juu ya lishe, chanjo na uzazi wa mpango.
Jumanne wiki hii ilikuwa Siku ya Ukunga Duniani. Ni siku ambayo wakunga wa Tanzania waliungana na wenzao duniani kutafakari juu ya kazi zao. Ni tafakari ambayo pia iliihusisha jamii nzima kwa sababu inahusika.
Mkunga ni mwanataaluma mwenye elimu ya kuhakikisha mama anajifungua salama na wote wanaendelea na afya njema.Kwa kawaida mkunga ndiye hasa anayeshuhudia dakika ya kwanza ya maisha ya  mtoto mchanga anapotoka duniani. Kwa maana hiyo mkunga anafanya kazi ngumu sana ya kuhakikisha maisha ya mtoto mchanga yanakuwa bora.
Mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Chama cha Wakunga Nchini,  Agenes Mtawa anasema kuwa wamekuwa wakisherehekea siku hiyo Mei 5, kila mwaka. Anasema hapa nchini ilikuwa ni siku ya wakunga kukaa pamoja na kutafakari hali halisi ya kazi zao, wako wapi na wanakwenda wapi katika kuhakikisha wanapunguza vifo vya mama na watoto vinavyotokana na matatizo ya uzazi.
Mtawa anasema kauli mbiu ya mwaka huu ni ‘Mkunga kwa maisha mazuri ya baadaye.”
Anasema uzito wa kauli hii ni kwamba mtoto akizaliwa akiwa na afya njema,  mama akijifungua kwa kupata huduma stahiki za mkunga mwenye weledi,  inategemewa mtoto huyo awe kiongozi wa baadaye. Lakini mtoto akizaliwa bila ya kupata huduma stahiki kutoka kwa mkunga mwenye weledi, anaweza kupata matatizo ya kuchelewa kulia au kutopumua vyema. Siyo hivyo pekee, anakuwa na matatizo baadaye kwa hiyo kauli mbiu inaangalia utoaji mzuri wa huduma  ili kuweza kuendeleza kizazi kizuri chenye akili timamu hapo baadaye na ndiyo malengo ya kaulimbiu.
Anasema kauli mbiu pamoja na siku ya wakunga imeanza mwaka 1991 kwa kukaa wakunga na kutafakari vifo vya watoto wachanga na wajawazito, vimepungua au vimeongezeka na kwa nini. Ni mwaka wa 14 kwa sasa wakunga wanasherekea siku yao. “Tumekuwa tukisherehekea siku yetu kila mwaka na kuna kuwa na kauli mbiu tofautitofauti na hulenga katika afya ya mama na mtoto.
“Kumekuwa na mabadiliko kiasi katika kupunguza vifo na kuboresha huduma bora ya afya ya mama na mtoto, ili kuweza kupunguza vifo vya kinamama na watoto,” alisema Mtawa.
Mtawa alisema kuwa, kwa sasa kuna changamoto kubwa ya kuwa na wakunga wachache kwa sababu mjamzito akifika kupima ujauzito ana huduma nyingi  kama kuzuia Virusi Vya Ukimwi (VVU), chanjo ya tetanasi, huduma za afya, kupimwa magonjwa ya kuambukiza,  sukari, wingi wa damu, ukuaji wa mtoto tumboni na mapigo ya moyo.
Mchakato wote huo wa upimaji unamkuta mkunga yuko peke yake, hawezi kufanya kazi hiyo kwa ufanisi na kwa haraka ili aweze kumhudumia mjamzito mwingine.
Anasema kunatakiwa kuwana wakunga zaidi ya watano katika vituo vya afya.

Wajawazito ni wengi
Halimu Juma ni mkazi wa Mbagala Charambe. Yeye ana ujauzito wa miezi saba. Anasema kuwa anafika katika hospitali ya Mbagala Zakhem saa 2:00 asubuhi anapanga foleni ya kusubiri huduma mpaka saa 8:00 mchana.
Mkunga Mkuu katika Hospitali ya Zakhem, Mbagala, Marina Lumambo anakiri kuwa wajawazito wanaofika kwa siku ni wengi sana ukilinganisha na idadi ya wakunga waliopo pamoja na vifaa vya upimaji.
“Kwa siku tunapokea wajawazito 150 hadi 200 wanaohitaji huduma ya upimaji. Kwa upande wa kujifungua kwa siku tunapokea wajawazito 30 hadi 40 na bajeti ya hospitali ni kuhudumia wajawazito 30 tu kwa siku.

Lugha chafu
Mara kadhaa yamekuwepo madai kwamba baadhi ya wakunga huwa na lugha chafu kwa wajawazito wanapoenda kujifungua na hata wakati mwingine hudiriki hata kuwapiga.
Kuhusu suala la wakunga kutumia lugha chafu  Mtawa anaanza kwa kujitetea mwenyewe akisema amefanya kazi hiyo kwa miaka 24 laki hata siku moja hajawahi kutumia lugha ya matusi kwa mjamzito. Anasema kufanya kazi hiyo ya ukunga kwa ufasaha bila ya kutumia lugha ya matusi unapata baraka kwa Mungu.
Isitoshe anasema kwa sasa kuna sheria ya uuguzi na ukunga ya mwaka 2010 ambayo inaeleza kinagaubaga juu ya kutumia lugha ya matusi kwa mkunga akiwa kazini kwa kumwambia mteja.
Mratibu wa Chama cha Wakunga Tanzania (Tama), Martha Rimoy anakiri yamekuwapo mara kadhaa madai ya wakunga kufanya vitendo kinyume na maadili wakati wanahudumia mjamzito.
Hata hivyo, anasema suala la namna hiyo huhitaji uchunguzi wa kina ili kupata uthibitisho ili mhusika achukuliwe hatua. Hata hivyo anasema kuwa yawezekana vikatokea lakini hii itatokana na aliyejihusisha na utovu huo wa nidhamu kuwa na elimu ndogo ya ukunga.
Anasema mkunga halisi, aliyesomea taaluma hiyo, huipenda kazi yake na wala siyo kuichafua. Hivyo humshughulikia mama anayejifungua kwa umakini ili kuhakikisha mama na mtoto wanakuwa salama.
Ahmed Makuwani ni daktari anayefanya kazi ya ukunga ni ya watu wenye moyo wa kuipenda kazi yao.
“Ukitaka kazi ya ukunga lazima ukubali kukesha kwa sababu wajawazito walio wengi hujifungua usiku. Ndiyo maana wakunga wengi ni wanawake na wanaume ni wachache kwa sababu wanaogopa kukesha kuwazalisha wajawazito,” anasema Makuwani.
Dk Makuwani alisema kuwa, hatasahau katika maisha yake mwaka huu, aliwafanyia upasuaji wajawazito tisa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa usiku mmoja na anafurahi kwa sababu wote wana afya njema.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment