Pages

Friday, April 17, 2015

SITTA: SITAJIUNGA NA CKU, NITABAKIA CCM

Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta, amesema hana mpango wa kuhama Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kujiunga na chama kingine cha siasa, ingawa anavutiwa na baadhi ya sera za vyama vinavyoeleza tunu za Hayati Mwalimu Julius Nyerere.Sitta alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na NIPASHE kuhusu taarifa zilizoenea kwamba anakifadhili chama kipya cha siasa kinachojulikana kama Chama cha Kijamaa na Uzalendo Tanzania (CKU) Jumatatu iliyopita kilipata usajili wa muda. “Sera za CCM zinajitosheleza,japo navutiwa na baadhi ya vyama kama ACT Wazalendo ambacho kinazungumzia tunu za Mwalimu Nyerere na kutetea wanyonge,” alisema.
Alisema taarifa kwamba anataka kuhamia CKU ni uzushi na kwamba mvuto wake aliokuwa nao kwa jamii ndio unaosababisha  baadhi ya vyama kutamani ajiunge navyo. Viongozi wa chama hicho kipya, wakisema hawatakuwa tayari kupokea wanachama wanaotaka kujiunga nacho kutoka vyama vya upinzani na kutoa mwaliko kwa Sitta kujiunga nacho akitaka.
Aidha, chama hicho kilijigamba kuwa katika uchaguzi mkuu wa Oktoba kitajipenyeza na kupata mgombea urais atakayetoka CCM ambaye atapeperusha bendera ya chama hicho kupambana na vyama vingine.
Mwenyekiti wa CKU, Ramadhani Semtawa, alisema ameanzisha chama hicho kwa malengo na madhumuni ya kutaka kuirejesha nchi katika maadili mazuri.
Alisema hivi sasa nchi inakabiliwa na matatizo kadhaa ikiwamo ukosefu wa umoja wa kitaifa, kukithiri kwa vitendo vya rushwa, ufisadi, ulanguzi na magendo ambavyo bado serikali haijachukua jitihada za kutosha kupambana navyo.

CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment