Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara), Philip Mangula akizungumza wakati wa
mkutano wa viongozi wa chama hicho katika jimbo la Ukonga, Dar es Salaam
jana.
Makamu Mwenyekiti wa CCM, Philip
Mangula amesema kanuni za uchaguzi za chama hicho zitawameza makada wake
wanaotumia fedha kuwanunua wapigakura kama maandazi.
Mangula alisema hayo jana alipokuwa akizungumza na
wanaCCM wa Jimbo la Ukonga, Dar es Salaam katika ziara yake katika
majimbo mawili ya Ukonga na Segerea.
Mangula alisema wapo wagombea wanaodhani kuwa wao
ni maarufu na wanasahau kuwa fedha walizotanguliza mbele ndiyo maarufu
na siyo wao wenyewe, hivyo wanajidanganya. “Unatawanya fedha kila kona, kwa kila kundi,
halafu unajiita maarufu badala ya kuona fedha zako ndiyo maarufu
unajidanganya ukijua kuwa unajidanganya,” alisema.
Aliwataka wanachama hao kuwa makini na watu wenye
tamaa ya kwenda Ikulu, huku akinukuu alichowahi kukisema Baba wa Taifa,
Mwalimu Nyerere kuwa; “mtu yeyote anayetafuta kwenda Ikulu kwa fedha
muogopeni kama ukoma.”
Akifafanua maadili na kanuni za wagombea wa CCM,
Mangula anayeongoza pia Kamati Ndogo ya maadili, alisema, “Yeyote
anayekukuruka kuutafuta uongozi kwa kutumia fedha, kununua wanachama ili
apigiwe kura au apitishwe, akiona jina lake halikutoka ajue limemezwa
na kanuni na sheria za uchaguzi.”
Kauli hiyo ya Mangula imekuja wakati kamati ya
maadili anayoiongoza ikiendelea kuwachunguza makada sita wa chama hicho
kwa madai ya kuanza kampeni mapema na kufanya vitendo vinavyokiuka
maadili.
Alisema CCM ni umoja, hivyo wanaoleta migogoro ni
watu waliopotoka ambao wanashindwa kutekeleza sheria walizojiwekea na
wenye tamaa ya madaraka.
Mangula alisisitiza kuwa anayowaeleza makada hao
si hadithi, bali ni ya kweli na yaliwahi kufanyika huko nyuma akitolea
mfano mwaka 2000 akiwa Katibu Mkuu wa CCM walipowasimamisha wagombea wa
majimbo ya Morogoro ambao wagombea sita walihonga, uchunguzi ukafanyika
ilipobainika walisimamishwa wote na wahusika wakapigwa marufuku
kugombea.
Alisema hata mkoani Singida makada waliobainika kusambaza fedha ili wachaguliwe walitimuliwa na nafasi ikatangazwa upya. “Wakalalamika demokrasia ipo wapi, tukawajibu hakuna cha demokrasia, unalazimisha vipi demokrasia kwa kutumia fedha?” alisema.
Alisema kutumia fedha kwenye uchaguzi ni tatizo
sugu, hadi watendaji wanakula rushwa kwa wagombea mpaka wanafikia
kupanga hadi bei ya hongo. “Ni aibu, watu wanajua kabisa watapata shilingi ngapi, wamepanga
hadi bei ya hongo na wanachukua kila upande, wanasema ndiyo wakati wao
wa kuvuna, wamekuwa malaya wa kisiasa, kutokana na kutokuwa na maamuzi
wala kufuata kanuni za chama,” alisema Mangula. Alisema kutokana na
kukithiri kwa tabia ya utovu wa nidhamu kwa wagombea wa CCM, hivi sasa
kadi za chama ni kama keki ya moto, kila mtu anazitaka, wagombea
wanawanunulia kadi wanachama, wanawalipia kadi za Jumuia ya Wazazi ili
waje kuwachagua baadaye, jambo ambalo ni kosa.
Makundi ndani ya chama
Machafuko na vurugu
Alisema kuna watu wana mawakala wa kuwasikilizia
kama majina yao yamepita au la, hao wanakiuka kanuni na sheria za chama,
hawana sifa ya kuwa wagombea, ikibainika watashughulikiwa.
Makundi ndani ya chama
Alisema makundi ndani ya chama yanakisababishia
udhaifu, kwani vita ya panzi furaha ya kunguru, hivyo makundi hayo
yanawapa nafasi wapinzani kufanya vizuri.
Alisema katika uchaguzi uliopita, wapinzani
hawakushinda kwa uwezo wao, bali walishinda kutokana na kuwapo kwa
makundi ya tangu baada ya uchaguzi wa mwaka 2000. “Mnataka kukiingiza chama katika udhaifu mkubwa,
hakiwezi kuwa chenye nguvu iwapo kuna makundi yanayolazimisha
lisilowezekana liwezekane, baada ya uchaguzi anayechaguliwa kugombea
anakuwa wa CCM na siyo yeye binafsi,” alisema.
Machafuko na vurugu
Makamu mwenyekiti huyo pia alizungumzia machafuko
kwa kuweka wazi kuwa katika hilo wanaotakiwa kuangaliwa ni viongozi wa
dini, kwani mengi huanzia huko.
Alisema siyo dini moja, bali zote Waislamu na
Wakristo “utakuta dhehebu moja halielewani na jingine na kwa Waislamu
pia dhehebu hili halipatani na jingine.”
Alisema mbali na viongozi wa dini, wanaoleta
machafuko wengine ni wanasiasa kwa kutaka madaraka, huku wakitumia kauli
mbaya kama patachimbika, lazima kieleweke ambazo ni za kichochezi.
Alisema ikitokea hali hiyo, madhara ni makubwa na nchi itakuwa ngumu kutawalika, hakutakuwa na amani wala maelewano.
Alitolea mfano wa Somalia akisema ilikuwa nchi
inayojiamulia mambo yake lakini tamaa ya kwenda Ikulu ikaleta yote hayo,
ikiwamo kuwapo kwa makundi ya yaliyoishia kutukanana, kukashifiana na
mwisho wa yote wakaingia katika mapigano na nchi hiyo sasa haitawaliki.
CHANZO: MWANANCHI
Alisema nchi kama Sudan Kusini, ilikuwa na chama kimoja cha
Sudan People’s Liberation Army (SPLA), lakini kwa uroho wa madaraka ya
kuingia Ikulu, kikagawanyika na kuwa makundi matatu ambayo yameiingiza
nchi hiyo kwenye vurugu kubwa. “Kwenda barabarani, kutupa mawe, siasa za chuki, siyo suluhisho la matatizo bali ni kuyaongeza,” alisema.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment