 
  
50% Watu waliojifungua kwa upasuaji mwaka jana.
Wakati idadi ya wanawake wanaojifungua kwa 
upasuaji ikizidi kuongezeka nchini, utafiti mpya umeonyesha kuwa 
migogoro baina ya wahudumu wa afya ya uzazi imechangia ongezeko la 
wajawazito wanaofanyiwa upasuaji bila kuwapo sababu za lazima.
Utafiti huyo uliowahusisha wanawake 13 
waliojifungua kwa upasuaji hivi karibuni, madaktari 18 na wakunga 14 
jijini Dar es Salaam, umebaini kuwa baadhi ya wahudumu wa afya ya uzazi 
huwafanyia upasuaji wajawazito kwa sababu zilizo nje ya uwezo wao.
Akiwasilisha matokeo ya utafiti huo, mwanafunzi wa
 Shahada ya Uzamivu, kutoka Chuo Kikuu cha Uppsala cha nchini Sweeden, 
Helena Litorp anasema, migororo na ‘presha’ ya kazi ni moja ya sababu za
 ongezeko la wanawake wanaojifungua kwa upasuaji.
Akizungumza kwa kujiamini, Litorp anasema pamoja 
na ukweli kwamba wanawake wanaogopa kujifungua kwa njia ya upasuaji 
wakihofia kifo, huku baadhi ya wahudumu wa afya nao wakiamini kuwa njia 
hiyo siyo salama kwa wajawazito ikilinganishwa na njia ya kawaida, 
makundi yote mawili yanakubali kufanyika upasuaji huo kwa lengo la 
kumwokoa mtoto anayezaliwa.
Hata hivyo, anasema matokeo ya utafiti huo 
uliofanyika mwaka jana, yanaonyesha kuwa kati ya mwaka 2000 na 2002 
asilimia 19 ya wajawazito walijifungua kwa upasuaji huku kiwango hicho 
kikipanda hadi kufikia asilimia 49 kati ya mwaka 2009 na 2011.
“Tuligundua kuwa madaktari vijana ambao wamepewa 
jukumu la kuzalisha kwa njia ya upasuaji wanakosa msaada kutoka kwa 
viongozi wao jambo ambalo wakati mwingine husababisha migogoro baina 
yao. Madaktari na wakunga wote walisema wanaogopa kulaumiwa kwenye vikao
 kwa uzembe, hivyo wakati mwingine wamejikuta wakilazimika kuzalisha kwa
 upasuaji bila kuwa na sababu ya lazima,” anasema.
Madaktari na wakunga wanasema ongezeko la wanawake
 wanaojifungua kwa upasuaji linatokana na sababu zilizo nje ya uwezo 
wao. Wanawake hufikishwa katika hospitali zisizo na vifaa vya kutosha. 
Pia, wengine wanachelewa kwenda kupata huduma kutokana na elimu na 
ndogo, lakini wapo baadhi yao ambao hutaka kujifungua kwa upasuaji.
Hata hivyo, anasema kuwa idadi kubwa ya vifo 
vilivyotokana na uzazi vilisababishwa na shinikizo la damu wakati wa 
ujauzito/kifafa cha mimba na kupoteza damu nyingi muda mchache baada ya 
kujifungua, lakini wamebaini kuwa sehemu kubwa ya vifo hivyo (7 asilimia
 .9), na vifo (asilimia 13) vinahusiana moja kwa moja na kujifungua kwa 
upasuaji.
“Tulipiga hesabu kwa kila operesheni 1,000 na 
kubaini kwamba hatari imeongezeka mara tatu zaidi katika hospitali ya 
mkoa kuliko ile ya chuo kikuu. Changamoto nyingi zilitokana na utoaji wa
 nusu kaputi ama dawa ya usingizi kwa njia ya uti wa mgongo na uambukizi
 wa vimelea katika kovu la upasuaji.
Tuliyatafsiri matokeo hayo kama ushahidi wa 
ongezeko la kujifungua kwa upasuaji katika maeneo yenye vifaa vya huduma
 vichache, hasa katika hospitali ndogo na pia kuna haja ya kuongeza 
ubora wa huduma hasa huduma za utoaji dawa za usingizi.
Vilevile, Litorp anasema katika utafiti huo 
walitaka kubaini iwapo wanawake wenye makovu yaliyotokana na upasuaji 
wapo katika hatari zaidi ya kupoteza maisha yao au watoto wao. Matokeo 
yameonyesha kuwa hakuna uhusiano wowote kati ya mambo hayo mawili, 
badala yake wanawake hao walijifungua salama.
“Matokeo yanatofautiana na vitabu kadhaa 
vilivyoandikwa awali, lakini yanaweza kuwa hivyo kutokana na kwamba 
wanawake waliowahi kujifungua kwa upasuaji huangaliwa kwa makini 
wanapopewa huduma ya afya. Kwa sababu hiyo hutakiwa kuja hospitali 
mapema wanapokaribia kujifungua, mara nyingi hupelekwe kwenye hospitali 
zenye huduma bora zaidi,” anasema.
Mkurugenzi wa Kitengo cha Uuguzi MNH, Dk Agnes Mtawa anasema, 
operesheni hizo zimeongezeka kwa asilimia 31 katika kipindi cha miaka 11
 iliyopita. “Ongezeko la ghafla la idadi ya kina mama 
wanaojifungua kwa operesheni kutoka asilimia 19 mwaka 2000 hadi asilimia
 50 mwaka 2011 linatisha na linahitaji kufanyiwa utafiti wa kina,” 
anasema Mtawa.
Mtawa anaeleza kuwa pamoja na kwamba kujifungua 
kwa njia ya upasuaji ni njia ya kuokoa maisha, utaratibu huo umegeuka 
tishio kwa wajawazito na jamii kwa ujumla.
Anasema hali hiyo imefika hapo ilipo kutokana na 
sababu mbalimbali zikiwamo miundo mbinu hafifu ya afya, uhaba wa 
rasilimali watu, ukosefu wa vifaa na wafanyakazi kukosa motisha. “Ninafurahi kutambua kwamba zipo tafiti 
zinazoendelea kufanywa kuhusu uzazi kwa njia ya upasuaji na kueleza 
mtazamo wa watoa huduma za afya kuhusu upasuaji huo. Nina hamu ya 
kusikia matokeo ya tafiti hizo,” anasema.
Hata hivyo, anasema pamoja na wajawazito 
wanaojifungua kwa upasuaji kuongezeka, vifo vya kinamama hao vimepungua 
kwa kiasi kikukwa katika miaka 10. Hivi sasa takwimu zinaonyesha kuwa 
wanafariki wajawazito 478 kati 100,000 wanaokwenda kujifungua.
Mkurugenzi huyo anasema pamoja na mafanikio hayo, 
Tanzania haijaweza kufikia Malengo ya Maendeleo ya Milenia yanayotaka 
kuwe na vifo chini ya 200 kwa kila wajawazito 100,000. Pia, anasema 
idadi kubwa ya wajawazito hufariki dakika 30 tangu wamefika hospitalini 
kutokana na kuchelewa.
Mkunga katika hospitali hiyo, Gloria Mkusa anasema
 kwa mwaka anazalisha wanawake wengi wanaojifungua kwa upasuaji kuliko 
wanaojifungua kwa njia ya kawaida. “Zaidi ya nusu ya wamama tunawapokea wanajifungua 
kwa upasuaji. Sababu zinategemeana, mara nyingine inakuwa sababu ni 
mtoto, mara nyingine ni mama,” anasema na kuongeza kuwa mwaka 2014 
hospitali hiyo ilipokea wajawazito zaidi ya 11,000.
Hata hivyo, Mkunga na Mhadhiri wa Ukunga wa Chuo 
Kikuu cha Tiba cha Muhimbili, Dk Sebalda Leshabari aliwahi kunukuliwa na
 gazeti hili, akisema kuwa upasuaji si jambo zuri kwa wajawazito. “Upasuaji siyo jambo zuri kabisa katika muktadha wa uzazi na ndiyo maana watu huita ni kujifungua kusiko kwa kawaida,” anasema.
Anataja madhara yanayowapata wajawazito wengi 
baada ya kujifungua kwa upasuaji kuwa ni pamoja na maziwa kutotoka kwa 
siku kadhaa baada ya kujifungua. “Maziwa yasipotoka ina maana mtoto anakosa yale maziwa ya kwanza ya mama ambayo huwa na virutubisho vyote,” anasema.
CHANZO: MWANANCHI
Anaongeza kuwa wajawazito wengi wanaofanyiwa 
upasuaji hulalamika kupata maumivu ya kichwa kwa muda mrefu pamoja na 
maumivu ya uti wa mgongo. Pia, anasema baadhi ya wanawake hutaka 
kujifungua kwa upasuaji bila kuwa na sababu maalumu kutokana na kuwa na 
dhana potofu.
Taarifa nyingine zinaonyesha kuwa hospitali 
binafsi zina tabia ya kulazimisha wanawake kujifungua kwa njia ya 
upasuaji kwa malengo ya kuongeza mapato.
Taarifa hizo zinaeleza kuwa kujifungua kwa upasuaji katika hospitali binafsi ni gharama inayozidi mara tatu ya ile ya kawaida.
Hii ina maana kwamba wanawake watatu wanaojifungua
 kwa njia ya kawaida kwenye hospitali hizo, gharama zake ni sawa na 
mmoja anayejifungua kwa upasuaji.
Tatizo jingine linatokana na wanawake wenyewe ambao huona taabu au karaha kujifungua kwa njia ya kawaida.
Hii inaweza ikawa ni kwa kushauriwa vibaya na 
jamii ama watu wa karibu. Baadhi ya watu mitaani wanadai njia hii 
haiathiri viungo vya uzazi vya mwanamke na wala hapati maumivu. Ukweli ni kwamba wataalamu wanapendekeza njia ya kawaida kuwa ni bora zaidi.
CHANZO: MWANANCHI
No comments:
Post a Comment