Chama cha 
Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) vimepata 
hati zenye mashaka katika ukaguzi wa hesabu zake, uliofanywa na Mkaguzi 
na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), kwa kipindi cha mwaka wa 
fedha ulioishia Juni 2013.
                
              
Kwa mujibu wa taarifa hiyo iliyopatikana jijini 
Dar es Salaam jana, CAG ameainisha vigezo saba tofauti vilivyosababisha 
hesabu za CCM kupata hati yenye mashaka na kueleza kuwa CCM imekosa 
uhalali wa kisheria kumiliki baadhi ya mali ilizonazo. Upande wa Chadema,  CAG ameanisha vigezo vitatu 
vya kupata hati hiyo na kubainisha kuwa zaidi ya Sh500 milioni 
zilitumika na chama hicho kununulia magari kumi bila kuidhinishwa na 
bodi ya zabuni.
Ukaguzi huo wa CAG umefanyika kwa mujibu wa Sheria
 namba 5 ya mwaka 1992 ya Vyama vya Siasa, iliyofanyiwa marekebisho na 
Sheria namba 7 ya mwaka 2009,  inayompa CAG mamlaka ya kukagua hesabu za
 vyama vya siasa. “Naamini ushahidi niliopata unatosha na sahihi 
kutoa maoni kuhusu ukaguzi wangu,” ilisema sehemu ya taarifa ya CAG kwa 
mwaka 2012/13 kwa vyama hivyo na kuongeza:
“CCM haikutenganisha thamani ya ardhi na nyumba
 vilivyo na thamani ya Sh 11,422,576,990.52. Hatukuweza kupata taarifa 
ya fedha ya CCM iliyokaguliwa kuhusu rasilimali zake zinazofikia 
Sh 9,632,576,701.57.”
Ilibainisha vigezo vingine vya hati yenye mashaka 
kuwa ni CCM kutowasilisha taarifa ya mapato yake ya fedha kutoka kwa 
wafadhili mbalimbali zilizofikia Sh1,526,536,802, huku CAG pia 
akishindwa kupata nyaraka za kuthibitisha matumizi na malipo 
yaliyofanywa na chama hicho yanayofikia Sh6,045,438,052.
Hata hivyo, mwaka jana CCM kilitangaza kuwa CAG, amekamilisha ukaguzi wa hesabu za chama hicho zilizoishia Juni mwaka 2012/13.
CCM ilieleza kuwa ukaguzi huo ulikuwa wa hesabu 
zilizoishia Juni 30, 2013 na ulifanywa kuanzia Mei 19, 2014 mpaka Oktoba
 2014 na kueleza kuwa imekuwa ikikagua hesabu zake kwa wakati kila mwaka
 bila kutoa wito kwa CAG kutosita kutoa taarifa kwa umma inapotokea 
chama cha siasa hakitoi ushirikiano katika kutimiza matakwa ya ukaguzi 
kisheria.
Kwa upande wa Chadema, taarifa hiyo ya CAG 
ilisema: “Katika ukaguzi tulibaini kwamba Chadema ina zaidi ya akaunti 
200 katika benki mbalimbali nchini lakini fedha zilizotajwa kuwapo 
katika taarifa zake katika mwaka ulioishia  Juni 2013 ni 
Sh224,824.750.56 kati ya hizo Sh221,060,446.41 zikiwa ni salio katika 
akaunti zake sita na kuacha salio la Sh3,764,304.15 kwa akaunti zaidi ya
 194 zilizosalia:
Magari 10 yalinunuliwa kwa Sh559,031,330 bila 
kuidhinishwa. Sh27,500,000 zilitumika kukodi jenereta bila kuwa na 
nyaraka zinazohalalisha matumizi yake.”
Taarifa hiyo ya CAG ilieleza kuwa katika vitabu 
vya risiti vya Chadema pia ilishindwa kuwasilisha  kwa ukaguzi kitabu 
cha risiti chenye namba 451-500 kilichotumika kukusanya Sh30,163,152 
hivyo kuzuia kufanyika kwa ukaguzi.
Hata hivyo, mwaka uliopita Chadema pia kilieleza kuhusu kuwepo kwa akaunti hizo na kufafanua kwamba akaunti kuu ya chama ndiyo inatoa fedha kwa akaunti za mikoani, hivyo wanaona kwamba mgao wa fedha walioufanya ni sehemu ya matumizi yao.
CHANZO: MWANANCHI
Hata hivyo, mwaka uliopita Chadema pia kilieleza kuhusu kuwepo kwa akaunti hizo na kufafanua kwamba akaunti kuu ya chama ndiyo inatoa fedha kwa akaunti za mikoani, hivyo wanaona kwamba mgao wa fedha walioufanya ni sehemu ya matumizi yao.
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment