Social Icons

Pages

Monday, March 16, 2015

KATOLIKI WAPINGA RASMI KATIBA INAYOPENDEKEZWA

 
Askofu Mkuu Jimbo kuu la Dar es Salaam, Polycarp Pengo.
Kanisa Katoliki Tanzania, limepinga rasmi kufanyika kwa Kura ya Maoni April 30, na limeshauri zoezi la kupitisha Katiba Inayopendekezwa lipewe muda zaidi, au liahirishwe hadi baada ya uchaguzi Mkuu, wa Oktoba mwaka huu.
Msimamo wa kanisa hilo, umetolewa kwenye Barua ya Kichungaji ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), iliyosomwa jana kwenye baadhi ya parokia na vigango vya Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, na baadhi ya majimbo mengine.
Akisoma barua hiyo mbele ya waumini, Padre Venance Tegete, wa Parokia ya Mtakatifu Agostino ya Ukonga, aliungana na maaskofu kuwataka waumini kuipigia kura ya hapana Katiba Inayopendekezwa, iwapo muda zaidi haitatolewa au kuahirishwa hadi baada ya uchaguzi, kama walivyoshauri maaskofu.
“Mchakato mzima wa katiba inayopendekezwa, una kasoro nyingi, zikiwamo zile za muda wenyewe kuwa mfupi, usambazaji wa nakala za katiba inayopendekezwa hauridhishi, na maoni mengi yalitolewa na wananchi yameachwa,” alisema.
Padre Venance alisema, iwapo Kura ya maoni haitaahirishwa au kuongezwa muda, basi wananchi wajiandikishe kwenye daftari la kudumu la wapiga kura, na wakaipigie kura ya hapana, katiba inayopendekezwa. Makanisa mengine ambako barua hiyo ilisomwa jimboni Da r es Salaam, ni Parokia ya Mbezi Louis, Mji Mpya Relini, Kipunguni, na Kigango cha Wazo Hill.
Barua hiyo ya kichungaji pia ilisomwa pia katika Jimbo Katoliki la Iringa, kwenye parokia za Mtakatifu Consolata, mjini Iringa, Parokia ya Moyo Mtakatifu wa Yesu, na parokia ya Kihesa. Aidha kwenye jimbo Katoliki la Bukoba, barua hiyo ilisomwa katika parokia zote za jimbo hilo.
Katika barua hiyo, iliyosainiwa na Rais wa TEC, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa, Kanisa Katoliki limesema, limefikia msimamo huo, kutokana na mashaka mbalimbali juu ya namna mambo yalivyoendeshwa, hadi kupatikana kwa katiba inayopendekezwa.
“Hadi sasa, katiba inayopendekezwa haijawafikia wengi, na kuwa hatua muhimu mno ambayo ni kuelimisha watu juu ya katiba inayopendekezwa haijafanyika, kwa hiyo wananchi wengi, hawana ufahamu wa kutosha, juu ya maudhui na misingi yake,” ilisema
Inasema, zoezi la uandikishaji wa wapiga kura katika daftari la kudumu la wapiga kura, halijafikia hatua yenye mwelekeo wa kulikamilisha. Ilisema hatua hiyo inawapa mashaka makubwa sana, na kwamba hawawezi kuamini kama zoezi hilo litakamilika, kabla ya tarehe ya kupiga kura ya maoni. “Katika hali hii tunabaki na mahangaiko, na mashaka makubwa ya kutakiwa kupigia kura katiba inayopendekzwa, ambayo hawaielewi kikamilifu, wala kujua matokeo yake, kwa mustakabali wa taifa letu.”
Inasema bahati mbaya sana wanasiasa viongozi wa nchi, wanaendelea kutoa maelezo ya kisiasa, yanayotoa majibu mepesi kwa maswali magumu, kwa lengo la kufanikisha malengo yao binafsi ya kisiasa.
“Huu si muda wa kufanya hivyo,” ilisema. Ikizungumzia msimamo wa TEC juu ya mpango wa kura ya maoni, inasema: “Tuangaliapo hali ya nchi yetu leo, tunapata hofu kwamba, uharakishwaji wa zoezi hili unaongeza fadhaa, na mpasuko ambao tayari upo katika jamii yetu,” inaeleza.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: