Social Icons

Pages

Monday, January 05, 2015

MAONI: POLISI WADHIBITI MAKUNDI YA WAHALIFU

Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova 
Jana katika tovuti hii tulichapisha habari iliyokuwa ikielezea kikundi cha wahuni wanaojiita ‘Panya Road’ walizua taharuki  jijini Dar es Salaam juzi baada ya kuvamia wananchi na kuwapora mali zao.
Taarifa za kundi hilo lililopora watu katika baadhi ya maeneo ya jiji hilo, zilienea kwa kasi ya ajabu kupitia mitandao ya kijamii watsapp, twitter, jamii forum, blog, instagram na ujumbe mfupi wa simu.
Kutokana na kuenea kwa taarifa hizo zilizotisha baadhi wafanyabiashara walifunga maduka, baa na wengine wakijifungia majumbani mwao kuwakwepa wahalifu hao.
Baadhi ya maeneo ambako kundi hilo linadaiwa kufanya uporaji ni Tabata, Magomeni Kagera, Sinza, Mwananyamala, Kinondoni, Kijitonyama, Manzese, Kigogo na Buguruni, huku wanafunzi wanaoishi katika Hosteli za Chuo Kikuu Dar es Salaam, wakitoka nje ya mabweni yao kwa kuhofia kuvamiwa na kikundi hicho. Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova alikaririwa akikiri kuwapo kwa vijana hao waliokuwa wametanda katika eneo la Magomeni Kagera na kwamba polisi walifika eneo hilo kuwadhibiti na kufanikiwa kuwakamata wawili.
Alisema kwa sasa wananchi wana hofu tu ya tukio lile la Magomeni kutokana na kusambaa kwa uvumi na hakukuwa na jambo tofauti na uhalisia wenyewe. Kova alisema hakuna taasisi inayoitwa Panya Road na kusisitiza kuwa vijana hao ni watoto wadogo waliokosa msingi wa malezi katika jamii, huku akiwataka wananchi wakiwaona vijana hao kutowapiga ili kuepusha vijana hao kulipiza kisasi.
Tunachukua nafasi hii kulishauri Jeshi la Polisi kuacha kutoa taarifa za kisiasa katika jambo kubwa kama hili.
Hatukutarajia kuona Kamanda Kova akitoa taarifa kama hiyo ya kwamba vijana waliokuwa wakifanya uhalifu huo ni vijana wadogo waliokosa msingi wa malezi katika familia zao.
Hata makundi makubwa ya wahalifu yaliyopo duniani yote yanaanza kama hawa Panya Road, huwezi kuwadharau wakati wamesababisha karibu jiji zima  kutikiswa.
Tunajiuliza, hivi jukumu la kulinda raia na mali zao ni la nani? Ni wazi kuwa ni la polisi ambao sasa Kamanda Kova anasema kuwa Panya Road ni watoto wadogo waliokosa msingi wa malezi, hivyo kwa maana nyingine hawana madhara. Jeshi la Polisi sasa lijipange vyema kudhibirti makundi ya uhalifu kama haya ambayo yapo mengi katika Jiji la Dar es Salaam na yamekuwa yakifunga mitaa na kupora wananchi bila kudhibitiwa.
Lakini kinachoshangaza ni kwamba Jeshi la Polisi limekuwaa likionekana kupata taarifa za kiintelijensia mapema zaidi katika kudhibiti mikutano ya siasa au maandamano ya wanasiasa ambayo Serikali imeyazuia.
Tulitarajia kwamba Jeshi la Polisi ambalo limejaa vijana wenye ujuzi wa kuchunguza, Panya Road wangekamatwa kabla ya kufanya uhalifu huo.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: