Pages

Thursday, January 22, 2015

MAKINDA: SIWATAMBUI CHENGE, NGELEJA

Spika wa Bunge, Anne Makinda akipokea kutoka kwa Balozi wa China hapa Nchini,  Dk Lu Youquing baadhi ya vifaa vya Tehama vilivyotolewa na serikali ya China kwa ajili ya kusaidia shughuli za Bunge, katika hafla iliyofanyika kwenye ofisi ya spika Dar es Salaam jana. Kulia ni Kamishna wa Bunge, Dk Maua Daftari.

Spika wa Bunge, Anne Makinda amesema hawatambui wenyeviti wa kamati tatu za kudumu za Bunge ambao Bunge liliazimia wavuliwe nyadhifa zao kutokana na kutajwa katika kashfa ya Akaunti ya Tegeta Escrow. Pamoja na kuwapo kwa maagizo ya Bunge, baadhi yao wanaendelea kujinasibu kuwa bado ni wenyeviti huku mmoja wao akiongoza vikao vya kamati. Akizungumza Dar es Salaam jana, Makinda alisema anachofahamu ni kuwa wenyeviti hao tayari wamaeshajiuzulu na kamati zao zinatakiwa kufanya uchaguzi wa wenyeviti wengine.
Wanaotakiwa kuachia nyadhifa zao ni Victor Mwabalaswa (Nishati na Madini), Andrew Chenge (Bajeti) na William Ngeleja (Katiba, Sheria na Utawala), ambaye hadi jana mchana alikuwa akiongoza kikao cha kamati hiyo. Siku tano zilizopita Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilillah alieleza kuwa kamati hizo zinatakiwa kufanya uchaguzi na kwamba wenyeviti hao hawakutakiwa kuongoza vikao, lakini hadi jana, hakuna uchaguzi wowote uliokuwa umefanyika na baadhi wanaendelea na majukumu yao.
Katika mkutano wake wa 16 na 17, Bunge katika azimio lake la tatu, liliazimia kuwa watu walioshiriki katika kashfa ya miamala ya Akaunti ya Tegeta Escrow wakiwamo viongozi wa kamati hizo tatu, wachukuliwe hatua kabla ya kuanza kwa mkutano wa 18 wa Bunge unaotarajiwa kuanza Januari 27.
Ngeleja alikaririwa na gazeti hili hivi karibuni akisema kwamba anaendelea kushikilia nafasi hiyo kwa maelezo kuwa uchunguzi sakata hilo bado unaendelea na ikithibitika ndipo Bunge litachukua uamuzi ambao alisema atakuwa tayari kuutekeleza.
Bunge lapata msaada
Katika hatua nyingine, Makinda amesema Bunge litaanza kutumia vifaa teknolojia kuwasilisha taarifa mbalimbali na kuachana na utaratibu wa kudurufu nyaraka nyingi ili kuepusha gharama.
“Bunge linatumia zaidi ya Sh1 bilioni kudurufu miswada na nyaraka nyingine za wabunge. Sasa tunataka kutumia mfumo wa kisasa. Kila kitu kitakuwa katika kompyuta za wabunge,” alisema.
Kauli ya Makinda imekuja wakati akishukuru baada ya kupokea msaada wa vifaa mbalimbali vya mawasiliano na kazi kutoka Serikali ya China. Balozi wa China nchini, Lu Youqing alimpatia Spika Makinda misaada ya vifaa hivyo vya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) vyenye thamani ya Dola100,000.
Vifaa hivyo ni printa kubwa 10, mashine 10 za kudurufu 10, nukushi 10, scanner 10, printa ndogo 11, kamera 10, kompyuta mpakato 23, ipad 13 na hard disk 91. Balozi Youqing alisema mbali na misaada hiyo, Serikali ya China iko katika hatua za mwisho kuanza ujenzi wa bandari ya Bagamoyo pamoja na kuboresha reli ya Tazara.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment