Pages

Wednesday, January 28, 2015

MAAZIMIO ESCROW KUTIKISA BUNGE

 
Mwenyekiti Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), Zitto Kabwe.
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania linaanza mkutano wake wa 18 leo, ambao pamoja na mambo mengine, wabunge wanatarajia kuhoji utekelezaji wa serikali wa maazimio nane ya Bunge kuhusu kashfa ya kampuni ya IPTL ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 kifisadi katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT).

Maazimio hayo yaliyopitishwa na Bunge Zima, Novemba 29, mwaka jana, yalifuatia taarifa maalumu iliyowasilishwa bungeni na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu ukaguzi maalumu wa malipo yaliyofanyika katika akaunti hiyo. Ukaguzi huo ulifanywa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) pamoja na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru).
Taarifa hiyo ya PAC, iliyowasilishwa na Mwenyekiti wake, Zitto Kabwe, bungeni, Novemba 26, mwaka jana, ilieleza kuwa mmiliki wa kampuni ya Pan African Power Solutions Ltd (PAP), Harbinder Singh Sethi, mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering & Marketing (VIP), James Rugemalira, walihusika kwa namna moja au nyingine katika kufanikisha kufanyika miamala haramu ya fedha katika akaunti hiyo kwenda kwa kampuni hizo. Wengine waliotajwa na taarifa hiyo ya PAC kuhusika katika kashfa hiyo, ni Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini aliyesimamishwa kazi, Eliakim Maswi na aliyekuwa Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo aliyetajwa na PAC kuwa dalali kati ya Rugemalira na Sethi kufanikisha uchotwaji wa fedha hizo.
Wamo pia aliyekuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Frederick Werema na waliokuwa wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco). Hivyo, Bunge likaazimia kuwa Jeshi la Polisi na vyombo vingine husika vya ulinzi na usalama viwachukulie hatua stahiki za kisheria kwa mujibu wa sheria za nchi watu wote waliotajwa na taarifa hiyo ya PAC kuhusika na vitendo vyote vya kijinai kuhusiana na miamala ya akaunti hiyo na wengine watakaogundulika kuhusika katika vitendo hivyo.
Kwa mujibu wa taarifa hiyo ya PAC, vitendo vilivyofanywa na watu hao vinaashiria makosa mbalimbali ya jinai, kama vile uzembe, wizi, ubadhirifu, kutakatisha fedha haramu, matumizi mabaya ya madaraka, rushwa na kupokea mali ya wizi. Hata hivyo, licha ya kutokuwapo yeyote kati ya waliotajwa aliyekwishachukuliwa hatua, ambazo Bunge liliazimia, tayari Prof. Muhongo na Jaji Werema walikwishajiuzulu nafasi zao serikalini, huku Maswi akiendelea kuchunguzwa.
Maazimio mengine ya Bunge, ambayo hadi sasa bado hayajatekelezwa ni pamoja na lile linalotaka mitambo ya kufua umeme ya IPTL kutaifishwa na lile linalotaka kuundwa kwa Tume ya Kijaji ya Uchunguzi kuchunguza utovu wa maadili dhidi ya majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Profesa Eudes Ruhangisa na Aloysius Mujulizi. Majaji hao walitajwa katika taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) iliyowasilishwa na Mwenyekiti wake, Zitto Kabwe, bungeni, Novemba 26, mwaka jana, kupata mgawo katika fedha zilizochotwa kutoka katika akaunti hiyo.
Walitajwa kupewa mgawo wa fedha hizo na mmiliki wa kampuni ya VIP Engineering, James Rugemalira. Katika taarifa hiyo ya PAC, Jaji Profesa Ruhangisa alitajwa kupata mgawo wa Sh. milioni 404.25 na Jaji Mujulizi Sh. milioni 40.4 kutoka katika fedha zilizochotwa katika akaunti hiyo.
Jaji Mkuu, Othman Chande, kupitia Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Ignas Kitusi, alikaririwa hivi karibuni akitaka aachiwe suala la majaji hao, akisema atalishughulikia yeye mwenyewe. Akihutubia taifa kupitia wazee wa Dar es Salaam Desemba 22, mwaka jana, Rais Kikwete, alisema amelipokea azimio dhidi ya majaji hao na kulijadili na washauri wake. Hata hivyo, alisema itabidi wafuate utaratibu wa kikatiba na kisheria wa kushughulikia masuala ya namna hiyo.
Rais Kikwete alisema kwa mujibu wa utaratibu huo, inatakiwa suala kama hilo lianzie kwenye mhimili wa Mahakama yenyewe na siyo kwa Rais au Bunge. Alisema Tume ya Mahakama ndiyo yenye mamlaka ya kumtaka Rais aunde Tume ya Kijaji ya kumchukulia hatua jaji yeyote pale inaporidhika kuwa amepoteza sifa za kuendelea kufanya kazi hiyo. “Nashauri suala hili tumuachie Jaji Mkuu wa Tanzania alishughulikie atakavyoona inafaa,” alisema Rais Kikwete.
Kwa mujibu wa PAC, fedha zinazodaiwa kuchotwa kutoka akaunti hiyo, ni zaidi ya Sh. bilioni 300 wakati kwa mujibu wa Rais Jakaya Kikwete, ni Sh. bilioni 202.9. Wengine waliotajwa kufaidika na mgawo wa fedha hizo, ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka (Sh. bilioni 1.6). Tayari Prof. Tibaijuka ameshatimuliwa kazi na Rais Kikwete kwa kupokea fedha hizo kupitia akaunti yake binafsi iliyoko benki ya Mkombozi, badala ya akaunti za shule na kwamba ni kinyume cha maadili.
Wengine waliopata mgawo kutoka katika fedha hizo, ni Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Bajeti, ambaye ni Mbunge wa Bariadi Magharibi (CCM), Andrew Chenge (Sh. bilioni 1.6); Mbunge wa Sengerema (CCM), William Ngeleja (Sh. milioni 40.4) na Mbunge mstaafu wa Sumbawanga Mjini (CCM), Paul Kimiti (Sh. milioni 40.4). Pia wamo aliyewahi kuwa Waziri wa Nishati na Madini, Daniel Yona (Sh. milioni 40.4); aliyekuwa mjumbe wa Bodi ya Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Dk. Enos Bukuku (Sh. milioni 161.7), Jaji Profesa Ruhangisa (Sh. milioni 404.25) na Jaji Mujulizi (Sh. milioni 40.4) pamoja na Mkurugenzi mstaafu wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (Rita), Philip Saliboko (Sh. milioni 40.4).
Wengine ni aliyekuwa Mkurugenzi wa Kituo cha Uwekezaji (TIC), Emmanuel Ole Naiko (Sh. milioni 40.4), Ofisa wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Lucy Appollo (Sh. milioni 80.8); Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki la Bukoba, Dk. Methodius Kilaini (Sh. milioni 80.9); Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Eusebius Nzigilwa (Sh. milioni 40.4) na Padri Alphonce Twimannye Simon (Sh. milioni 40.4). Azimio lingine, ambalo bado halijatekelezwa, linataka Bodi ya Wakurugenzi wa Tanesco kuwajibishwa. Rais Kikwete akihutubia taifa kupitia wazee wa Dar es Salaam, alisema bodi hiyo tayari ilishamaliza muda wake.
Hata hivyo, kuna hoja, ambazo zimekuwa zikitolewa na watu wa kada mbalimbali kwamba, bodi hiyo kumalizika muda wake, hakuzuii wajumbe wake kuchukuliwa hatua za kisheria kutokana na kuhusishwa katika kashfa ya akaunti hiyo.
 
RATIBA YA MKUTANO WA BUNGE LA 18
Bunge jana lilitoa ratiba ya mkutano wake wa 18 unaoanza leo mjini hapa, ambao pamoja na mambo mengine, litajadili taarifa za CAG zilizowasilishwa katika mkutano wa 15. Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Bunge kupitia Afisa Habari wake, Owen Mwandumbya, taarifa hizo za CAG zitajadiliwa kwa siku mbili mfululizo, kuanzia kesho.
Taarifa hizo ni ya hesabu zilizokaguliwa za serikali kuu, serikali za mitaa na mashirika ya umma. Mwandumbya alisema leo Bunge litaanza kwa kiapo cha utii cha Mwanasheria Mkuu (AG), George Masaju, aliyeteuliwa na Rais Kikwete baada ya Jaji Werema kujiuzulu nafasi hiyo. Alisema Ijumaa Bunge litajadili taarifa za kamati za kisekta na zisizo za kisekta, ambazo ni Kamati ya Bunge ya Miundombinu na Kamati ya Bunge ya Nishati na Madini.
Jumamosi, taarifa za Kamati ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Mazingira na Kamati ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji zitajadiliwa. Kamati hizo zitaendelea kujadiliwa Februari 2, 3 na 4 na kamati zitakazojadiliwa ni pamoja na ya Katiba, Sheria na Utawala, ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na ya Masuala ya Ukimwi. Nyingine ni Kamati ya Ulinzi na Usalama, Kamati ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa na Kamati ya Uchumi, Viwanda na Biashara.
Katika mkutano huo wa Bunge, pia jumla ya miswada mitatu itasomwa na kupitishwa na wabunge. Miswada hiyo ni ya Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa mwaka 2014, Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Kodi wa mwaka 2014 na Muswada wa Sheria ya Takwimu wa mwaka 2013.
Kabla ya kuahirishwa kwa Bunge, linatarajia kupokea taarifa ya Kamati Teule iliyoundwa kuchunguza na kuchambua sera mbalimbali zinazohusu masuala ya ardhi, kilimo, mifugo, maji na uwekezaji ili kubaini kasoro zilizomo katika matumizi ya ardhi. Katika Mkutano huo wa Bunge, maswali ya msingi 125 yanatarajiwa kuulizwa pamoja na maswali 18 ya msingi yataulizwa papo kwa papo kwa waziri mkuu.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment