Pages

Wednesday, January 28, 2015

KARIAKOO WAFUNGA MADUKA KUPINGA MWENYEKITI KUKAMATWA

Kaimu Kamanda wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro.
Wafanyabiashara wa Soko Kuu Kariakoo mtaa wa Kongo, jijini Dar es Salaam, jana walifunga maduka yao na kuandamana hadi katika Kituo cha Polisi Kati, wakishinikiza kuachiwa kwa Mwemyeti wao, Johnson Minja.

Minja alikamatwa juzi na Jeshi hilo na kusafirishwa kupelekwa mjini Dodoma kujibu mashitaka yanayomkabili ya kuhamasisha wafanyabiashara wa mkoa huo wagome kufungua maduka kupinga matumizi ya mshine za kielektroniki (EFDs). Kaimu Kamanda  wa Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Simon Sirro,  alithibitisha kukamatwa  kwa Mwenyekiti huyo kwa kosa la kuhamasisha wafanyabishara wa mkoani Dodoma wagome.
Sirro alisema Minja alikamatwa na polisi jijini Dar es Salaam, lakini kesi yake ipo mjini Dodoma na baada ya kumkamata alipelekwa mkoani humo ilikujibu tuhuma hizo. Aidha, Sirro alisema walikasirishwa na wafanyabiashara hao kufanya maandamano kumfuata Minja kituo cha polisi. “Anayeweza kuzungumza vizuri kuhusiana na swala hilo ni Kamanda wa Jeshi la Polisi mkoa wa Dodoma,” alisema Sirro.
Wakizungumza na NIPASHE wafanyabishara hao walisema kuwa hawatafungua maduka yao hadi hapo Mwenyekiti wao atakapoachiwa huru. Mmoja wa wafanyabiashara hao, Jafari Mauya, alisema hawatafungua maduka yao kwani hawafahamu sababu ya kukamatwa kwa Minja. Hata hivyo, baadhi ya maduka yalifunguliwa majira ya mchana baada ya maandamano.
Walipoulizwa sababu za kufungua maduka yao licha ya kukubaliana kuyafunga, walisema waliofungua ni miongoni mwa wafanyabishara wachache ambao hawajajiunga na chama cha wafanyabishara Kariakoo. Msemaji wa wafanyabiashara, Stephen Chamle, alisema wao watafunga safari kwenda Dodoma kumuona Minja. “Tangu jana (juzi) tulikuwa tunamtafuta Minja, lakini hakupatikana, leo (jana), wamemtafuta kwa njia ya simu yake ya mkononi na kuwapa taarifa kuwa yuko Dodoma,” alisema Chamle.
Awali, wafanyabishara hao walikusanyika na kuteua wawakilishi ambao walikwenda kuzungumza na Jeshi la Polisi na kukubaliana kuwa warudi ili wakafungue maduka. Katibu wa wafanyabishara hao, Christopher Kionda, alisema walikubaliana kuwa wengine wakafungue maduka na wengine waende Dodoma kumuona Mwenyekiti wao. “Leo (jana) tunaondoka kwenda Dodoma kumuona Mwenyekiti wetu, wengine wataendelea tu na biashara,” alisema Kionda.
Alipotafutwa Kamanda wa Polisi mkoani Dodoma, David Misime, kwa njia yasimu alijibu kuwa alikuwa katika kikao na kuelekeza atafutwe baadaye ingawa hakupatikana hadi tunakwenda mitamboni. Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipakodi wa Malaka ya Mapato Tanzania (TRA), Richard Kayombo, alisema alisikia taarifa hizo za kufunga maduka na kuwa wanazifuatilia.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments:

Post a Comment