Social Icons

Pages

Wednesday, January 28, 2015

JUKATA: WAGOMBEA URAIS WAPIMWE AFYA KWANZA

Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba (Jukata), Deus Kibamba.
Wagombea wa nafasi ya urais nchini, wametakiwa kupima afya zao kisha matokeo ya afya zao kutangazwa hadharani, ili umma wa Watanzania uwafahamu kabla ya kufanyika kwa uchaguzi mkuu mwaka huu.

Upimaji huo wa wagombea hao na wagombea wenza, umetajwa kuweza kulipunguzia Taifa gharama kubwa za matibabu nje ya nchi kwa viongozi hao wakishakuwa madarakani. Kauli hiyo ilitolewa jana jijini Dar es Salaam na Mwenyekiti wa Jukwaa la Katiba (Jukata), Deus Kibamba, wakati akizungumza na waandishi na kutoa taarifa kuhusu masuala ya Katiba na uchaguzi wa marudio wa Rais nchini Zambia, uliofanyika Januari 20, mwaka huu. 
Alisema, kutokana na uzoefu walioupata wakati wa uchaguzi nchini humo, serikali ya Zambia ilimpa kazi wakala wa kupima afya za wagombea urais 11 waliokuwa wanawania kiti cha urais. Kauli hiyo imekuja wakati tayari baadhi wa wanaoiwania nafasi hiyo, hususan ndani  ya Chama tawala (CCM) kuonyesha wazi nia ya kuwania urais.
“Mapendekezo yetu ni hayo wagombea wapimwe afya zao, wapo ambao tayari wagonjwa, lakini wanataka kuongoza nchi. Ingawaje nchini hatujawahi kukumbwa na kiongozi kufariki akiwa madarakani, lakini Zambia wameutumia utaratibu huu wa kupima afya za wagombea kabla, kwani wao wamewapoteza marais wawili wakiwa mamlakani,”  alisema. Mwaka Agosti 2008 alifariki rais aliyekuwa madarakani, Levy Mwanawasa na kufanya uchaguzi uliompa ushindi, Rupiah Banda.
Pia Oktoba mwaka jana, aliyekuwa Rais Michael Satta alifariki dunia. Mwaka 2001, wakati Benjamin Mkapa akiwa Rais katika serikali ya awamu ya tatu, Makamu wa Rais, Dk. Omar Ali Juma,  alifariki dunia ghafla jijini Dar es Salaam. Hata hivyo Jukata ilipendekeza kuwa uchaguzi mkuu kufanyika katikati ya wiki badala ya Jumapili, ili kuongeza   idadi ya wapigaji kura.
Alisema uchaguzi ufanyike siku za Jumatatu hadi Alhamisi badala ya siku za Ijumaa, Jumamosi wala Jumapili kwani siku hizo ni za ibada za waumini wa dini tofauti.
CHANZO: NIPASHE

No comments: