Social Icons

Pages

Friday, January 23, 2015

ASKOFU KKKT ATISHIA KUPINGA KURA YA MAONI

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kiluteri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kusini, Isaya Mengele, amesema iwapo rasimu ya Katiba nayopendekezwa haitasambazwa na kuwafikia wananchi kote nchini mapema, atatangaza kuwahamasisha  wasiipigie kura ya maoni.

Kura ya maoni ya wananchi kuamua ama kuikubali au kuikataa rasimu ya katiba hiyo inatarajiwa kupigwa Aprili, mwaka huu, lakini hadi kufikia jana, ilikuwa haijaanza kusambazwa kwa wananchi. Askofu Mengele alisema hayo katika hafla ya kukabidhi Shule ya Sekondari ya Ruhuji iliyokuwa chini ya Balozi mstaafu wa Tanzania nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC), Gidion Ngilangwa.
Alisema amezunguka sehemu nyingi nchini, lakini hajaona mahali ambako wananchi wanakosema kuwa wanaifahamu katiba hiyo. Askofu Mengele alisema wananchi wanatakiwa kuisoma na kuielewa ili wapige kura kukifanyia maamuzi kile walichokisoma na kukielewa. “Sisi kama kanisa hatutakubali kuwaruhusu wananchi kupigia kura katiba inayopendekezwa kama haitafikishwa kwa wananchi, kwani wanatakiwa kuisoma na kuielewa kabla ya kuipigia kura,” alisema Askofu Mengele.
Aliongeza: “Endapo itafika tarehe 30 mwezi wa nne, tutawaambia wananchi wasiipigie kura na wasubiri waisome kwanza.” Alisema kanisa linajiuliza itakapofika Aprili 30, mwaka huu wananchi watapigia kura ya ndiyo au hapana juu ya nini wakati hawajui kilichopo ndani ya katiba hiyo.
Kwa mujibu wa Askofu Mengele, kamwe hawawezi kukubaliana na kitu hicho na kwamba, watatangaza kwa umma ulimwenguni kote wajue, ikiwa ni pamoja na kuwakataza kupiga kura. Hata hivyo, alisema wataungana na Watanzania wote kuhakikisha kunakuwapo na amani wakati wote wa mchakato wa katiba na uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
“Sasa mwezi Januari karibu unaisha. Uandikishaji wapigakura haujaanza. Muda uliopo ni mfupi kweli. Rais alikutana na maaskofu tukamshauri kuwa apitishe mchakato huo mpaka uchaguzi upite, lakini alishawishiwa na Bunge la Maalumu la Katiba na kutangaza kufanyika upigaji wa kura ya maoni kabla ya uchaguzi mkuu,” alisema Askofu Mengele.
Mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Sarah Dumba, ambaye ni Ofisa Tarafa ya Njombe, Lilian Kembele, alisema serikali ina mpango mkakati wa kuhakikisha inasambaza Katiba inayopendekezwa kwa wananchi kabla ya muda wa kuipigia kura haujafika. Aliwataka wanasiasa kuwa makini katika kipindi hiki cha kuelekea kwenye mchakato wa kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa ili kuepuka kuiingiza nchi katika machafuko.
Alisema serikali haitakuwa na jinsi kama viongozi wa dini watawazuia wananchi kuipigia kura katiba hiyo, kwani ile ya zamani ipo. Kauli hiyo ya Askofu Mengele, imetolewa siku chache baada ya aliyekuwa Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba, kutamka kwamba hakuna uwezekano wa kura ya maoni kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Jaji Warioba alisema ameona taarifa inayoeleza kuwa kura ya maoni inatarajiwa kufanyika Machi, mwakani na kusema kama kuna umakini, kura hiyo haitawezekana kufanyika. Naye Mbunge wa Ubungo (Chadema), John Mnyika, amewasilisha taarifa kwa Katibu wa Bunge akitaka Bunge lijadili udhaifu wa katiba inayopendekezwa na kupitisha azimio la kuahirishwa kufanyika kwa kura ya maoni ya wananchi kuamua ama kuikubali au kuikataa katiba hiyo.
Pia amemtaka Rais Jakaya Kikwete kutangaza kufuta tangazo la serikali la kufanyika kwa kura hiyo mwishoni mwa Aprili, mwaka huu, hadi uchaguzi mkuu utakapofanyika. Mnyika alisema kama ambavyo Rais Kikwete alitumia sheria kutangaza upigaji kura hiyo, ni vema pia akafanya hivyo kuutengua kwa kuwa kuna udhaifu katika mchakato mzima. Alisema zimebaki siku chache kufanyika mchakato huo, lakini hadi sasa elimu kuhusiana na suala hilo haijatolewa kwa wananchi.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: