Social Icons

Pages

Wednesday, December 17, 2014

WAZIRI GHASIA ATIMUA WAKURUGENZI WALIOBORONGA CHAGUZI SERIKALI ZA MITAA

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) Hawa Ghasia amewasimamisha kazi wakurugenzi wa halmashauri  mbalimbali kutokana na kuchelewa kuandaa  na kupeleka vifaa vya kupigia kura pamoja na uzembe katika kutekeleza majukumu yao katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa uliofanyika nchi nzima Jumapili iliyopita.
Akizingumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam, Waziri Ghasia amesema uamuzi huo umefanyika baada ya Rais kwa mujibu wa sheria kuridhia adhabu hizo zitolewe. Alisema wakurugenzi waliosimamishwa kazi  ni watano ili kupisha uchunguzi zaidi wa kiwango cha ushiriki wao katika kasoro zilizojitokeza kwenye halmashauri zao.
Wakurugenzi hao waliosimamishwa kazi na halmashauri zao kwenye mabano ni Fotunatus Fwema (Mbulu), Issabela Chilumba (Ulanga), Pendo Malabeja (Kwimba), Wiliam Shimwela (Sumbawanga Manispaa) na Felix.T.Mabula (Hanang).
Kwa mujibu wa Ghasia, wakurugenzi ambao uteuzi wao umetenguliwa ni sita na watapangiwa kazi za kufanya kutokana na taaluma zao huku wakurugenzi watatu wakipewa onyo kali na watakuwa chini ya uangalizi  kama wanaudhaifu wachukuliwe hatua zaidi.
Aliwataja wakurugenzi watendaji waliotenguliwa nyadhifa zao ni  Benjamin Mjoya aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi (Mkuranga), Abdalla Ngodu (Kaliua), Masalu Mayaya (Kasulu), Goody Pamba (Serengeti), Julius Madiga (Sengerema) na Simon Mayeye (Bunda). 
Aliwataja wakurugenzi waliopewa onyo kali  ni pamoja na Mohamed Maje (Rombo), Hamis Yuna (Busega) na Jovin Jungu (Muheza) na watakuwa chini ya uangalizi kubaini kama wana udhaifu mwingine wachukuliwe hatua zaidi. Waziri Ghasia alionya kuwa ofisi yake haitasita kuchukua hatua stahiki kwa wote watakaokiuka maadili ya kazi  au watakaopungukiwa uwezo wa kutekeleza  majukumu waliokabidhiwa.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: