Pages

Tuesday, December 16, 2014

WAKULIMA WALALAMIKIA LUMBESA, MAKOKORO


Wakulima wa vijiji vya Ibingu na Kisongwe, Kata ya Lumbiji wilayani hapa wamelalamikia kukithiri kwa vitendo vya wafanyabiashara kununua mazao kwa kutumia vipimo visivyokubalika kisheria.
Malalamiko hayo waliyatoa mjini hapa jana kwa nyakati tofauti na kuongeza kuwa licha ya vipimo hivyo, ambavyo ni Lumbesa na Makokoro, kupigwa marufuku, bado vinaendelea. Walisema wanunuzi hao wamekuwa wakienda katika maeneo ya vijiji hivyo na kutaka kuuziwa mahindi na mpunga kwenye magunia yaliyojazwa kupita uzito wa kawaida wa kilo 100. Mmoja wa wakulima hao ambaye ni mkazi wa Kijiji cha Kisongwe, Cecilia Simon alisema kuwa ni vyema Serikali ikaingilia kati tatizo hilo ili wafanyabiashara hao wasiendelee kuwanyonya wakulima wakati wanaponunua mazao.
Alisema ununuzi wa mazao hayo kwa kutumia vipimo hivyo hauwanufaishi wakulima ambao wamekuwa wakitumia nguvu kubwa na muda mrefu katika kuzalisha, badala yake huwapa faida wafanyabiashara.
Simon aliitaka Serikali kuwachukulia hatua watakaobainika kukiuka utaratibu na kutumia vipimo hivyo.
“Tunaiomba Serikali iendelee kusimamia na kuwachukulia hatua wafanyabiashara wanaowalaghai wananchi,” alisema Simon. Mkazi wa Kijiji cha Ibingu, Patrick Machemba aliiomba Serikali na wadau wengine wa maendeleo kuwafundisha mbinu bora za usindikaji wa mazao yao ili wayaongezee thamani.
Mwakilishi wa Mtandao wa Jamii wa Usimamizi wa Misitu Tanzania (Mjumita), Elida Fundi alisema Shirika la Kuhifadhi Misitu ya Asili Tanzania (TFCG) na mtandao huo wanaangalia uwezekano wa kuwapatia wakulima mbinu bora za kilimo.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment