Pages

Tuesday, December 16, 2014

TAMISEMI: WALIOVURUGA UCHAGUZI SASA KUKIONA


Ofisi ya Waziri Mkuu kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia imeiagiza mikoa yote nchini kuwasilisha taarifa kuhusu kasoro zilizojitokea katika Uchaguzi wa Serikali za Mitaa juzi ili iwachukulie hatua watendaji watakaobainika kuhusika.
Imesema kushindwa kusimamia uchaguzi na kusababisha kasoro, ni moja ya makosa makubwa na kuwa watakaobainika, watachukuliwa hatua kali kulingana na uzito na kiwango cha kuhusika kwao na kwamba wanaweza kufukuzwa kazi, kuvuliwa madaraka, kushushwa cheo au kukatwa mishahara.
Uchaguzi huo ulikumbwa na kasoro nyingi na kuahirishwa katika baadhi ya maeneo kutokana ama kukosekana kwa majina ya wagombea, baadhi yao kuwekewa nembo za vyama wasivyotoka au uhaba wa vifaa vya kupigia kura. Hata hivyo, halmashauri 145 kati ya 162 zilizofanya uchaguzi huo hazikuwa na dosari, tatu hazikufanya uchaguzi kabisa kutokana na vifaa kuchelewa, 14 zilikuwa na kasoro katika baadhi ya vijiji, vitongoji na mitaa na uchaguzi wake kuahirishwa mpaka Desemba 20 na 21. Akitoa taarifa ya awali ya uchaguzi huo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Tamisemi), Hawa Ghasia alisema pamoja na kasoro hizo, uchaguzi huo umefanikiwa kwa zaidi ya asilimia 80. “Katika uchaguzi huu hakukuwa na vitambulisho vya mpigakura kama ilivyo katika Uchaguzi Mkuu. Uchaguzi huu unafanyika katika mtaa au kitongoji hivyo ni rahisi watu kutambuana na pia mtu akishapiga kura si rahisi kurudia mara ya pili na tuliagiza mpigakura awe ama na kitambulisho cha kazi, leseni au kile cha kupigia kura katika Uchaguzi Mkuu kwa ajili ya kutambulika,” alisema. Alisema malalamiko na kasoro zilizoripotiwa katika vyombo vya habari haziwezi kujibiwa wala kutolewa ufafanuzi na Tamisemi hadi baada ya kupata ripoti kutoka mikoani. Akizungumzia malalamiko ya wananchi kutoyaona majina yao, Ghasia alisema ulitolewa muda wa siku tatu kwa wananchi kufanya uhakiki lakini wengine hawakufanya hivyo. “Kuhusu majina kubadilishwa au kuisha kwa wino na kukosekana kwa vitu vidogovidogo hilo linaweza kuwa limefanyika kutokana na uzembe tu. Ndiyo maana tumeagiza tupewe taarifa rasmi.” Akizungumzia kasoro zilizobainika katika karatasi za kupigia kura, alisema utaratibu wa kuandaa vifaa hivyo ulikuwa ukifanywa na halmashauri husika na si Tamisemi, hivyo ni vigumu kwa wizara hiyo kuagiza walioandaa vifaa wachukuliwe hatua. “Mfano Temeke na Ilala walimtumia Mpigachapa Mkuu wa Serikali. Awali, aliwapelekea vifaa vyenye matatizo, hata walipovirejesha ili avirekebishe, vilirudishwa vikiwa bado na kasoro. Mpiga Chapa aliingia mkataba na manispaa na ndiyo aliyepewa zabuni,” alisema. Alisema suala hilo linafanyiwa uchunguzi ili kubaini kama kasoro katika wilaya hizo zimesababishwa na Mpiga Chapa wa Serikali au wilaya husika. Alipotafutwa mpiga chapa mkuu wa serikali, Cassian Chibogoyo kuzungumzia kuhusu tuhuma za ofisi yake kuwa sehemu ya dosari za uchaguzi katika manispaa za Ilala na Temeke, alisema tuhuma amezisikia na kwamba atawasiliana na wizara kabla ya kutoa majibu yake leo. Ghasia alipoulizwa kama yuko tayari kuwajibika, alijibu, “Kama ikibainika kuna halmashauri imefanya vibaya katika uchaguzi huu kwa sababu yangu nitakuwa tayari kuwajibika. Tamisemi tulijipanga kimkoa pia ilikuwa ngumu kwa kila kituo cha kupigia kura kuwa na polisi. Tutahakikisha kasoro hizi hazitokei katika mitaa ambayo uchaguzi utarudiwa,” alisema. Aliitaja mikoa ambayo haikuwa na dosari katika uchaguzi huo kuwa ni Arusha, Mbeya, Kagera, Njombe, Singida, Lindi, Ruvuma, Katavi, Geita, Iringa, Dodoma na Mtwara.
Mikoa yenye kasoro
Alisema mikoa ambayo baadhi ya halmashauri zimeahirisha uchaguzi katika baadhi ya maeneo ni Kilimanjaro, Manyara, Morogoro, Shinyanga, Simiyu, Kigoma, Mwanza, Tabora, Tanga, Mara, Rukwa, Dar es Saalam na Pwani. Mkoa wa Kilimanjaro uchaguzi haukufanyika katika kata nne za Ngoyo, Holili, Chela na Kindikati zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Rombo pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Hai katika Kata ya Machame Kaskazini. Mkoa wa Manyara uchaguzi haukufanyika katika Kata nane za Halmashauri ya Wilaya ya Hanang’ na Halmashauri ya Mbulu katika kata nne za Gehandu, Bargish, Yaedampa na Maretadu. Mkoa wa Morogoro ni Halmashauri ya Ulanga katika kata nane za Mtimbila, Usengule, Chilombola, Itete Njiwa, Ruaha, Ilagua na Sofi na Kata ya Dakawa iliyopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Mvomero. Mkoa wa Shinyanga ni kata za Nyaya, Mtombo, Bulyangulu, Bulige, Mwaketa, Kashishi, Ikinda na Bugala zilizo Halmashauri ya Wilaya ya Msalala. Mkoa wa Simiyu ni kata za Lamadi, Igalukilo, Malili na Mkula zilizopo ni Busega pamoja na Kata ya Mbita iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Itilima. Mkoa wa Kigoma ni halmashauri nzima ya Kasulu na Mkoa wa Mwanza ni kata 18 za Halmashauri ya Kwimba na kata 28 za Halmashauri ya Wilaya ya Sengerema. Mkoa wa Tabora uchaguzi umeahirishwa katika halmashauri yote ya Kaliua. Pia katika kata za Wela, Buge, Janija, Milambo Itogo na Mwakanshahagha zilizopo Nzega. Katika Mkoa wa Tanga uchaguzi umeahirishwa katika kata 20 za Magoloto, Kicheba, Msozwe, Magilla, Mlingano, Pandedarajani, Ngomeni, Pungwe, Kumba, Bwembela, Topwe, Lusanga, Mpapaya, Mhamba, Songe, Kasungo, Mtindilo, Kilulu, Mkuzi na Kwakifua. Mkoa wa Mara ni katika Kata ya Mihingo iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Bunda na Kata 13 za Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti. Mkoa wa Rukwa ni katika Kata za Momoka, Msua, Ntendo, Mafulala, Sumbawanga, Izia, Chanji na Kizwite za Halmashauri ya Manispaa ya Sumbawanga. Mkoani Dar es Salaam uchaguzi haukufanyika katika kata nne za Halmashauri ya Manispaa ya Temeke na mitaa kadhaa katika Manispaa ya Ilala na Pwani ni katika Halmashauri yote ya Wilaya ya Mkuranga.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment