Pages

Wednesday, December 24, 2014

NI DHAHIRI SERIKALI HAIJAVALIA NJUGA TATIZO LA WAHITIMU MBUMBUMBU


Imani ya Watanzania wengi ni kuwa Serikali, kupitia vyombo vunavyosimamia sekta ya elimu, imekuwa ikijipanga vilivyo kuondoa madudu mbalimbali yanayoitia doa sekta hiyo mama.
Hivi ndivyo watendaji mbalimbali wa Serikali wanavyojisifu mara kwa mara, wakituaminisha wananchi kuwa sasa mambo ni shwari katika sekta ya elimu.
Lakini hali inaonekana kuwa si shwari. Taarifa mpya ambayo gazeti hili limeichapisha jana inatupa wasiwasi wananchi kuhusu mikakati ya Serikali ya kuzifanyia kazi changamoto zinazoikabili sekta ya elimu.
Jana tuliandika katika gazeti hili kuwa wahitimu 344 waliomaliza darasa la saba mwaka huu mkoani Arusha, wamebainika kuwa hawajui kusoma, kuandika na kuhesabu. Kati yao wavulana ni 181 na wasichana ni 163.
Bila shaka hii ni taarifa ya kustua hasa kwa kuzingatia kuwa wengi tulifikiri tatizo la watoto kumaliza elimu ya msingi bila ya kuwa na stadi hizi muhimu, lilishapatiwa ufumbuzi. Tulifikiri hivyo kwanza kwa sababu ya kauli za viongozi wa Serikali na pili kutokana na mikakati tuliyoshuhudia Serikali ikichukua kwa watendaji wa shule ambazo mwaka 2011 zilibainika kuwa na wahitimu wasiojua kusoma na kuandika.
Kwa kukumbushia ni kuwa Aprili mwaka 2012, Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, ilibaini kuwapo kwa wanafunzi wa sekondari 5,200 waliokuwa hawajui kusoma na kuandika. Wanafunzi hao walikuwa sehemu ya wahitimu wa darasa la saba mwaka 2011. Kilichofuatia ni kuwa walimu katika shule husika walichukuliwa hatua za kinidhamu kama vile kuhamishwa shule na adhabu nyingine.
Wengi tulifikiri huu ulikuwa mwanzo wa Serikali kujipanga kuhakikisha tatizo hili halijitokezi tena na hata likijitokeza sio kwa ukubwa kama tulioushuhudia katika taarifa ya Arusha. Huu ni mkoa mmoja tu ambao mpaka sasa angalau umetoa taarifa zake kuhusu matokeo ya darasa la saba.
Ni dhahiri, hasa kwa kuzingatia hali ilivyo, matokeo katika mikoa mingine yanaweza kushabihiana na yaliyotokea Arusha.
Ukiondoa taarifa hii ya Arusha na ile ya mwaka 2012, ziko taarifa za mara kwa mara zinazoonyesha ukubwa wa tatizo hili. Kwa mfano, mwaka 2010, asasi ya Twaweza ilitoa ripoti ya utafiti iliyobainisha kuwa kati ya wahitimu watano wa darasa la saba, mmoja hawezi kusoma hadithi ya kiwango cha darasa la pili.
Utafiti huo ulioitwa kwa Kiingereza ‘Are Our Children Learning’ (Je, Watoto Wetu Wanajifunza), ulishirikisha sampuli ya watoto 42,033 kutoka kaya 22,800 nchi nzima.
Baada ya matokeo haya ya Twaweza na hata yale ya mwaka 2012, matarajio ya wengi ni kuwa Serikali ingestuka na kuweka mikakati makini, lakini tunasikitika kupaza sauti kuwa hali haijawa hivyo; tatizo linaendelea. Kilichotokea Arusha mwaka huu ni sehemu ya udhaifu wa wahusika kutolishupalia tatizo hilo. Baadhi ya matukio hapa nchini yanatupa wasiwasi kuwa huenda kuna mkakati maalumu wa kuacha hali hii iendelee ili wachache wanufaike kwa kutumia migongo ya wale wanaokosa elimu.
Kwa mfano, tunajiuliza kwanini wajumbe walio wengi wakati ule wa Bunge Maalumu la Katiba, walipitisha kipengele cha elimu kwa wabunge kuwa darasa la saba badala ya kidato cha nne kama ilivyopendekezwa katika rasimu ya Katiba ya Tume ya Jaji Warioba?
Jambo moja ni dhahiri kuwa kuna watu katika uongozi wa siasa wanaoridhika na hali hii. Kwao elimu sio muhimu, ndiyo maana hawaguswi na matatizo yetu ya msingi kama hili la kuwa na wahitimu mbumbumbu.

CHANZO: MWANANCHI

No comments:

Post a Comment