Miongoni mwa wazee wa Dar es Salaam wakimsikiliza Rais Jakaya Kikwete alipokuwa akizungumza nao juzi. Swali ambalo
limekuwa likiulizwa kila mara Rais anapozungumza na Taifa kupitia wazee
ama wa Dar es Salaam au Dodoma la jinsi gani wazee hao wanapatikana sasa
limepata jibu.
Kwa muda mrefu imekuwa ikielezwa kuwa wazee hao
huchaguliwa kwa itikadi za kisiasa ili kupata wale wanaounga mkono kile
anachoeleza Rais.
Akijibu hoja hizo, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam,
Saidi Meck Sadiki alisema, “Tulitumia njia za matangazo ya televisheni,
redio na magazeti kupitia habari mbalimbali. Isingekuwa rahisi kuwaalika
wazee kwa njia ya barua kwani tungewaandikia wangapi?
“Sisi ambao ndiyo tulikuwa na jukumu la kuwaalika
wazee hatukusema kuwa wana CCM ndiyo waje hapana, kila mmoja anaruhusiwa
kuja hapa na hata uliona mwenyewe hakuna aliyekuja akazuiwa kisa siyo
mwana CCM,” alisema.
Kuhusu baadhi kuvaa sare za CCM, Sadiki alisema,
“Huwezi kuwaalika wazee halafu ukawapangia nguo za kuvaa, huu ni mkutano
wa Rais Kikwete kama mtu anapenda kuvaa sare ya CCM, Chadema, CUF,
NCCR-Mageuzi au chama chochote hazuiwi.
Aliongeza, “Kama chama fulani kimeshindwa kuvaa
sare na kingine kimevaa huwezi kusema eti hatujawaalika, si
kweli...tuache propaganda za uongo na kudai waliohudhuria ni wana CCM
pekee.”
Baadhi ya wazee waliohudhuria mkutano wa jana
katika Ukumbi wa Diamond Jubilee walikuwa wamevalia sare za CCM na
kukiwa hakuna mzee au mtu mwingine yeyote aliyekuwa amevaa sare za vyama
ama vya NCCR-Mageuzi, CUF, Chadema au chama kingine.
Akimkaribisha Rais Kikwete kuzungumza na wazee
hao, Sadiki alianza kwa kusema, “Tunakushukuru kwa kukubali kuongea na
wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam kwa mara ya kwanza tangu ulipotoka kupata
matibabu.”
Sadiki alisema, “Wazee wa Mkoa wa Dar es Salaam
wanakuomba sana ukimaliza kuzungumza nao uende ukapumzike Msoga
(Bagamoyo, mkoani Pwani kijijini kwake) hadi sikukuu
zitakapomalizika...utuache sisi katika jiji hili lenye uzushi wa kila
aina.”
Mkuu huyo wa mkoa aliendelea kusema: “wakati
unakwenda kupumzika, waliomba wakupatie zawadi mbili ambazo ni ujenzi wa
maabara na matokeo ya uchaguzi wa serikali za mitaa uliomalizika juzi.
Matokeo
Mkuu huyo wa Mkoa wa Dar es Salaam, alisema katika
jumla ya mitaa 555 kati ya 557 iliyofanya uchaguzi huo ulioanza Desemba
14, mwaka huu na kumalizika juzi, ni mitaa miwili tu haikufanya
uchaguzi wa marudio kutokana na vurugu. Akizungumzia ujenzi wa maabara ikiwa ni utekelezaji wa agizo la
Rais, Sadiki alisema mkoa huo ulitakiwa kujenga maabara 281 ambazo
zimekamilika.
Akizungumzia zawadi hizo za ujenzi wa maabara na
uchaguzi, Rais Kikwete alisema, “Imenifurahisha sana, tulijenga shule za
kata tukasahau ujenzi wa maabara, tulikosea na tukiikosa hatuwezi kuwa
na Taifa lisilo kuwa na wanasayansi, hongereni sana na hongereni kwa
uchaguzi wa Serikali za Mitaa hongereni sana.”
Mkutano huo uliohudhuriwa na mawaziri, manaibu
mawaziri, makatibu wakuu, wabunge, wakuu wa taasisi mbalimbali akiwamo
Mbunge wa Maswa Mashariki (Chadema), John Shibuda.

No comments:
Post a Comment