Mataifa wanachama wa Umoja wa Ulaya EU, yanaonekana kuanza kuchoshwa na 
vitisho vya Uingereza kujitoa katika umoja huo, kutokana na madai ya 
waziri mkuu David Cameron kutaka kubadilisha kanuni za msingi wa umoja 
huo.
Wakati king'ora cha kuashiria moto kilivyokatiza hotuba kubwa ya waziri 
mkuu David Cameron kuhusu Ulaya katika kiwanda kikubwa cha kutengeneza 
mitambo mwezi Novemba 2014, alitania kuwa hadhira yake ilikuwa ikisikia 
kengele zikilia mjini Brussels kuhusiana na uwezekano wa Uingereza 
kuondoka katika Umoja wa Ulaya.
Ukosoaji wa Umoja wa Ulaya ni jambo linalopokelewa vyema nchini 
Uingereza, ambako chama kinachoupinga umoja huo cha UK Independent UKIP,
 kilijizolea ushindi mkubwa katika uchaguzi wa bunge la Ulaya mapema 
mwaka 2014.
Shinikizo la kisiasa
Akikabiliwa na shinikizo kutoka kwa wapinzani wa Umoja wa Ulaya ndani na
 nje ya chama chake, waziri mkuu Cameron ameahidi kura ya maoni kuamua 
ama kubakia au kutoka ndani ya umoja huo mwaka 2017, ikiwa atachaguliwa 
tena kuliongoza taifa hilo mwezi Mei mwaka 2015. Wakati akisema 
angependa kuona Uingereza ikibakia katika umoja wa Ulaya, Cameron 
amedokeza pia kwamba anaweza kubadilisha msimamo wake ikiwa matakwa 
muhimu hayatatekelezwa.
Uchunguzi wa maoni unaonyesha kuwa Waingereza hawana ari ya kuwa katika 
Umoja wa Ulaya, licha ya nchi hiyo kuwa mwanachama wa jumuiya hiyo ya 
kisiasa na kiuchumi kwa miaka 40. Hata uongozi wa chama cha upinzani cha
 Labour, ambacho hakiahidi kura ya maoni, kinapambana kutoonyesha hisia 
kali kuhusu umoja huo wenye wanachama 28.
Suala moja muhimu na linalozua tafrani ni kuhusu uhamiaji, na hasa 
kushindwa kwa Uingereza kuwazuwia wahamiaji wa EU kuingia nchini humo 
kutokana na kanuni ya umoja huo inayowapa raia wake uhuru wa kutoka 
sehemu moja kwenda nyingine bila kuwekewa vikwazo.
Takwimu za hivi karibuni zinaonyesha kuwa raia 228,000 wa Umoja wa Ulaya
 wamewasili nchini Uingereza kufikia Julai mwaka huu -- hii ikiwa ni 
zaidi ya mara mbili ya shabaha ya wahamiaji 100,000 aliyoiahidi Cameron 
kufikia Mei 2015.
Msimamo usiyoeleweka
Lakini Cameron anatuma ujumbe mchanganyiko kuhusu uanachama wa Umoja wa 
Ulaya. Wakati chama chake cha Wahafidhina kikipoteza umaarufu kwa chama 
cha UKIP, wafanyabiashara wengi wanasisitiza umuhimu wa kubaki katika 
Umoja wa Ulaya, ambao unatoa fursa makhsusi za kuwafikia walaji wake 
milioni 500.
Kansela wa Ujerumani Angela Merkel anataka UK ibakie katika EU lakini
 hakubaliani na madai ya Cameron kubadilisha kanuni za msingi za umoja 
huo.
Michael Rake, kiongozi wa shirikisho la viwanda la Uingereza, alionya 
kuwa kuondoka katika Umoja wa Ulaya kutaifanya Uingereza kujifungia nje 
ya ulimwengu katika wakati ambapo dunia inapitia mabadiliko 
yasiyozuwilika.
Jambo la muhimu ni kwamba Cameron aliamua kutoa hotuba yake kuhusu Ulaya
 katika kiwanda cha mitambo mikubwa cha JBC, ambacho pengine 
hakingekuwepo bila faida za soko la pamoja linalotokana na uanachama wa 
Umoja wa Ulaya.
Na licha ya kupendekeza kupunguzwa kwa mafao ya kijamii kwa wahamiaji wa
 EU, Cameron anasisitiza kuwa hataki kuharibu kanuni ya uhuru ya kutoka 
sehemu moja kwenda nyingine, ambayo Waingereza zaidi ya milioni 1.3 
wamenufaika nayo.
Badala yake, mkwara wa Cameron unalenga kuilainisha Brussels kwa 
kutishia kuiondoa Uingereza katika EU ikiwa hakutakuwa na makubaliano 
kuhusu masuala muhimu kama vile uhamiaji. Lakini Umoja wa Ulaya 
umesisitiza msimamo wa kupinga jitihada zozote za kubadili kanuni yake 
hiyo ya uasisi kuhusu uhuru wa watu kutoka nchi moja kwenda nyingine.
Chini ya uongozi wa Cameron, Uingereza imejikuta ikizidi kukwaruzana na 
wanachama wengine, kuhusiana na masuala kuanzia uteuzi wa rais wa 
Halmashauri ya Umoja wa Ulaya Jean-Claud Juncker, na kura ya turufu ya 
Uingereza mwaka 2011 kupinga hatua zilizonuwiwa kushughulikia mgogoro wa
 kiuchumi wa umoja huo. Lakini tabia hii inaonekana kuwachosha wanachama
 wengine.
'Cameron anachezea moto'
Mwezi Oktoba, aliyekuwa rais wa Halmashauri ya Umoja wa Ulaya Jose 
Manuel Barroso alionya kuwa Cameron anachezea moto kwa kuchochea hisia 
za chuki dhidi ya Umoja wa Ulaya, akisema katika mahojiano na 
televisheni ya France 24 kuwa "huwezi kuikosoa EU kuanzia Jumatatu hadi 
Jumamosi, na kuwaomba watu kuipigia kura EU siku ya Jumapili.
Mrithi wake Jean-Claud Juncker, ameahidi kufanya kazi kuibakiza 
Uingereza katika Umoja wa Ulaya, lakini mataifa mengi hayako tayari 
kubadili mikataba ya EU kwa lengo la kubadili sheria za msingi za 
uanachama, yakihofia kuwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha matatizo 
mengine yasiyotarajiwa. Kansela wa Ujerumani Angela Merkel aliripotiwa 
kukosa uvumilivu pale Cameron alipozungumzia kuanzisha ukomo wa 
wahamiaji - hatua ambayo aliamua kutoichukuwa wakati akibainisha mipango
 yake ya kupunguza uhamiaji.
Wengine wanaona katika mtazamo wa Uingereza, ukaida wa kudumu wa 
kuachana na historia yake ya zamani, ilipokuwa taifa lenye nguvu kubwa 
duniani, lenye mahusiano maalumu na Marekani, na pia njozi ya ufahari wa
 utamaduni wake ulioanzishwa karibu miaka 2000 iliyopita, na ambao sasa 
unatishiwa na wale wanaowachukulia kuwa ni washenzi wanaomiminika nchini
 mwao.
CHANZO: DW KISWAHILI 

No comments:
Post a Comment