Social Icons

Pages

Monday, November 02, 2015

WATETEZI HAKI ZA BINADAMU WALAANI POLISI KUVAMIA TACCEO

Mtandao wa Watetezi wa Haki za Binadamu (THRDC), umelaani kuvamiwa na kukamatwa kwa wafanyakazi 36 wa Kituo cha Uangalizi wa Uchaguzi (TACCEO).
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, alisema kitendo hicho ni kinyume cha utawala bora, kwani kituo hicho kilipewa kibali cha uangalizi wa uchaguzi kutoka Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) na kimekuwa kikifanya kazi hiyo kila kunapokuwa na uchaguzi na kutoa ripoti za uchaguzi na kasoro zilizojitokeza.
Alisema asasi za Tanzania zimeendelea kufuatilia mchakato wa uchaguzi mkuu 2015 tangu uandikishwaji wapigakura, uhamasishaji hadi kampeni kwa umakini na kwamba tukio hilo la uvamizi ni la pili baada ya la mkoani Njombe waangalizi wa uandikishaji wapigakura kuvamiwa na kupigwa na polisi.
"Kitendo cha kuhisi kuwa TACCEO wanakusanya na kutoa matokeo ya uchaguzi na kuwavamia kimefanywa na Jeshi la Polisi siyo kwa hiari yao bali kwa shinikizo la wanasiasa hasa walioshiriki mchakato wa uchaguzi mkuu," alisema na kuongeza:
"Taarifa zetu za kiuchunguzi zinaonyesha kuwa, kulikuwa na mawasiliano mengi siku hiyo kati ya vyombo mbalimbali ikiwamo Kurugenzi ya Azaki (asasi za kiraia) iliyopo Wizara ya Maendeleo, Jinsia na Watot na siku hiyo hiyo askari walikwenda TGNP -Matandao lakini hawakufanikiwa chochote na kisha kwenda TACCEO."
Olengurumwa alisema hali hiyo ni viashiria vibaya kwa mustakabali wa Azaki nchini na kwamba vyombo vinavyopaswa kuwa mtetezi wa asasi hizo vinakuwa sehemu ya kudidimiza uhuru wake.
Alilitaka Jeshi la Polisi kutokubali kutumiwa na baadhi ha vyama vya siasa/wanasiasa, kwani kufanya hivyo kunawanyima raia haki zao za msingi za kushiriki masuala ya umma na kupunguza uhuru wa asasi za kiraia katika utendaji kazi zake.
"Jeshi la Polisi na vyombo vingine vya dola vifuate kanuni za demokrasia na utawala wa sheria na kuheshimu mikataba mbalimbali ya kimataifa ambayo Tanzania ni mwanachama ili kulinda amani na utulivu nchini," alisema.
Aidha, Olengurumwa alitoa wito kwa waangalizi wa uchaguzi na Umoja wa Mataifa kuendelea kutoa ushauri na kuingilia kati vitendo vya ukiukwaji wa sheria na haki za binadamu vilivyojitokeza katika mchakato mzima wa uchaguzi mkuu wa mwaka huu vinavyorudisha nyuma demokrasia," alisema.
Waangalizi hao walivamiwa Oktoba 29, mwaka huu, katika eneo la Kawe, jijini Dar es Salaaam na baadhi ya wafanyakazi na vifaa ikiwamo komyuta mpakato mbili, kampyuta za kawaida 36 na simu zao kukamatwa.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: