Social Icons

Pages

Thursday, June 04, 2015

WANASIASA WAKUMBUSHWA KUMRUDIA MUNGU

Askari wa Bunge wakiwa wamebeba jeneza lenye mwili wa Mbunge wa Ukonga, Marehemu Eugune Mwaiposa ulipowasili katika Viwanja vya Bunge kwa ajili ya wabunge kutoa heshima za mwisho, Dodoma jana.
Wanasiasa wanaojiandaa kuingia katika Uchaguzi Mkuu, wametakiwa kumuomba Mungu ili awape nafasi hizo kwa njia sahihi kuliko kutumia ‘sangoma’. Wito huo ulitolewa jana na Mchungaji Samuel Mshana kwa niaba ya Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Dodoma katika ibada ya kuuaga mwili wa marehemu Eugen Mwaiposa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Ukonga (CCM).
Mwaiposa alifariki dunia juzi akiwa usingizini kwa kile kilichoelezwa kuwa alikuwa akisumbuliwa na ugonjwa wa shinikizo la damu, mwili wake ulisafirishwa jana kwa ndege ya kukodi kupelekwa Dar es Salaam ambako utazikwa keshokutwa nyumbani kwake Kipunguni, Dar es Salaam.
Ilikuwa ni siku ya huzuni jana, wakati wa ibada iliyofanyika kwenye Viwanja vya Bunge mjini Dodoma, iliyohudhuriwa na umati wa waobelezaji wakiwamo wabunge, wafanyakazi, viongozi wa mkoa na Taifa akiwamo Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue.
Katika Bunge la kumi, huyu ni mbunge wa saba kufariki dunia. Akihutubia kwenye ibada hiyo, Mchungaji Mshana alisema ni wakati wa kuangalia namna watu wanavyopaswa kutafuta madaraka kupitia njia zisizofaa.
Serikali katika ibada hiyo iliwakilishwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera na Bunge, Jenister Mhagama, ambaye alisema hadi Mwaiposa kabla ya kukutwa na umauti alionekana mwenye afya njema na aliomba kuchangia katika hotuba ya Wizara ya Afya. Mhagama alisema, Serikali na Chama cha Mapinduzi vimepoteza mtu mahiri ambaye pengo lake halitazibika na kutoa rambirambi ya Sh5 milioni.
Akiwakilisha Kambi ya Upinzani, Tundu Lissu alisema kuwa mbunge huyo alikuwa kipenzi cha kila mmoja na wakati wote walipenda kumuita ‘Dear’ kuonyesha kuwa alikuwa anapendwa.
Mwili wa marehemu uliwasili Dar es Salaam jana saa 9:32 alasiri, huku ndugu, jamaa na viongozi wa kada mbalimbali wakijumuika nyumbani kwake Kipunguni. Majonzi na vilio vilitanda nyumbani kwa marehemu Mwaiposa, huku baadhi ya viongozi akiwamo Meya wa Ilala, Jerry Silaa akielezea kusikitishwa kwake na kifo hicho. Mwili huo ulienda kuhifadhiwa katika Hospitali ya Lugalo huku taratibu za mazishi zikiendelea.
Wakati huohuo Rais Jakaya Kikwete ameelezea masikitiko yake kutokana na kifo cha Mbunge wa Jimbo la Ukonga, Eugen Mwaiposa.
Katika salamu za rambirambi kwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Anne Makinda, Rais Kikwete alisema: “Nimepokea kwa mshtuko na masikitiko taarifa za kifo cha Mbunge Mwaiposa ambaye nimejulishwa ameaga dunia mjini Dodoma ambako alikuwa anaendelea kuhudhuria vikao vya Bunge.”
Pia, Rais Kikwete ambaye kwa sasa yuko nchini Finland, alitoa pole kwa familia kwa kuondokewa na mama na mchangiaji mkubwa katika maisha yao.

CHANZO: MWANANCHI

No comments: