Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen
Wasira, amewasimamisha kazi wakurugenzi watatu wa Mamlaka ya Ustawishaji
wa Bonde la Mto Rufiji (Rubada) kwa tuhuma za ufisadi wa zaidi ya Sh.
bilioni mbili.
Wasira alitangaza uamuzi huo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jijini Dar es Salaam. Aliwataja waliosimamishwa kazi rasmi kuanzia jana kuwa ni Kaimu
Mkurugenzi wa Rubada, Aloyce Masanja; Mkurugenzi wa Fedha,
Filozi Mayayi na Mkurugenzi wa Mipango na Utawala, Tabu Ndatulu.
Alisema kusimamishwa kazi kwa vigogo hao kunafuatia kamati
iliyoundwa na wizara hiyo chini ya Mwenyekiti wake ambaye ni Kaimu
Mkurugenzi wa Mkaguzi wa Serikali, Semloki Mwanjika, kuchunguza tuhuma
na malalamiko mbalimbali yaliyokuwa yanatolewa na wawekezaji kuhusu
Rubada, kufanya kazi kwa zaidi ya miezi mitano na kubaini ubadhirifu
huo.
“Kwa mamlaka niliyonayo mimi, nawasimamisha kazi rasmi kuanzia leo,
kwa hatua nyingine za makosa ya ubadhirifu wa fedha na rushwa
nitaliachia Jeshi la Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
(Takukuru) wafanye kazi yao baada ya mimi kukamilisha kazi ya
kuwawajibisha kwa kosa na ukosefu wa nidhamu kazini, ripoti zote
nitaziwasilisha Polisi na Takukuru,” alisema Wasira. Alisema hatua
nyingine zitachukuliwa dhidi ya vigogo hao baada ya Polisi na Takukuru
kukamilisha uchunguzi dhidi yao kuhusiana na tuhuma hizo.
Alisema wawekezaji walitoa Sh. bilioni 2.7 kwa ajili ya kuwekeza
kwenye miradi mbalimbali ya kilimo, Sh. milioni 714 zitumika kwa kazi
hiyo na Sh. bilioni 2.3 matumizi yake hayajulikani. Wasira alisema Sh. milioni 329 zilizotengwa kwa mradi wa ujenzi wa
bonde la mto Rufiji nazo hazijulikani zilipo na nyingine Sh. milioni 58
ambazo wafanyakazi walikatwa kuchangia Mfuko wa Hifadhi ya Jamii kwenye
Shirika la NSSF hadi sasa hazijapelekwa.
Alisema katika kipindi chote kulikuwa na malalamiko ya utendaji
mbovu wa viongozi hao na baada ya tume kufanya uchunguzi wake kuanzia
Novemba mwaka jana, ilibaini walikuwa ni wabadhirifu wa fedha, ubinafsi
na wala rushwa. “Kwanza wamejitengenezea mfumo mbaya wa kujinufaisha
wenyewe na usiokuwa na mgawanyo wa majukumu kwa watendaji wote hali
inayosababisha ulegevu kwenye kuwajibika na kusababisha hadi maofisa
wanasafiri na fedha mifukoni,” alisema Wasira.
Alifafanua kwa mujibu wa uchunguzi wa kamati hiyo, kiasi cha Sh.
milioni 13 zilitumika kwa matumizi binafsi na Sh. milioni 13 vigogo hao
kujikopesha wenyewe. Wasira, alisema pia kamati hiyo ilibaini kuwa licha ya matumizi
mabaya ya fedha pia mamlaka hiyo ilikuwa haifuatilii malipo ya kampuni
binafsi ambazo zinafanyakazi na Rubada.
Kuhusu wawekezaji ambao walitoa fedha zao kuwekeza, lakini
hawakupewa maeneo ya uwekezaji, alisema wanaidai serikali fedha hizo au
wapewe ardhi kwaajili ya uwekezaji. Wasira alitaja mapendekezo mengi yaliyotolewa baada ya kupokea
ripoti ya kamati hiyo kuwa ni bodi itafute mtu mwenye sifa ya kukaimu
nafasi ya Kaimu Mkurugenzi wa Rubada. Mengine ni bodi ianze mara moja
mchakato wa kutafuta viongozi watakaosimamia nafasi hizo baada ya
wakurugenzi hao kusimamishwa.
“Wakati haya yote yakiendelea, taratibu rasmi za utumishi wa umma
za kuwasimamisha kazi na utaratibu wa kushughulikia tatizo zinaendelea,”
alisema Wasira. Kuhusu uteuzi wa Mkurugenzi Mtendaji, Wasira alisema suala hilo analifahamu Rais Kikwete na analifanyia kazi.
KAULI YA MASANJA
Masanja, alipoulizwa na NIPASHE kuhusu hatua ya Waziri Wasira
kumsimamisha kazi na wenzake kwa tuhuma za ufisadi, alidai kuwa yeye
siyo mfanyakazi wa Rubada tangu Septemba mwaka jana baada ya kuacha kazi
kutokana na sababu zake binafsi.
Alisema aliandika barua ya kuomba kuacha kazi kwa Katibu Mkuu wa Wizara hiyo na kupewa baraka zote. Tangu Masanja ateuliwe na bodi ya mamlaka hiyo kukaimu ukurugenzi
wa Rubada ni takribani miaka mitatu kutoka kwa aliyekuwa Mkurugenzi wa
Mamlaka hiyo.
Tangu wakati huo, Rais Jakaya Kikwete alikuwa hajateua Mkurugenzi
wa Rubada, hivyo Masanja kukaimu nafasi hiyo kutoka kwa bosi wake huyo.
Rubada ilianzishwa mwaka 1970 kwa lengo la kuendeleza bonde la Mto
Rufiji na Pwani, Morogoro, Iringa, Njombe, Ruvuma, Mbeya na sehemu ya
Lindi.
Mbali na kuendeleza maeneo hayo, pia Rubada iliundwa kwa lengo la kutangaza vivutio na uwekezaji kwenye sekta ya kilimo nchini.
CHANZO:
NIPASHE

No comments:
Post a Comment