Licha ya ujenzi maghorofa marefu
kutajwa kuwa kielelezo cha maendeleo katika miji mikubwa, jijini Dar es
Salaam hali ni tofauti kutokana na hofu iliyopo kuhusu ubora wa majengo
hayo, mfumo wa majitaka, mipango miji na ukosefu wa maeneo ya maegesho.
Miaka 20 iliyopita, ilikuwa vigumu kuzungumzia maghorofa marefu jijini Dar es Salaam bila ya kutaja majina kama Kitega Uchumi (NIC House), kumaanisha jengo la Shirika la Bima la Taifa lenye ghorofa 16 na urefu wa mita 57.40, IPS lenye ghorofa 12 na urefu wa 43.05, au Extelecom House, kumaanisha jengo la Shirika la Posta lenye ghorofa 14 na urefu wa mita 50.23.
Miaka 20 iliyopita, ilikuwa vigumu kuzungumzia maghorofa marefu jijini Dar es Salaam bila ya kutaja majina kama Kitega Uchumi (NIC House), kumaanisha jengo la Shirika la Bima la Taifa lenye ghorofa 16 na urefu wa mita 57.40, IPS lenye ghorofa 12 na urefu wa 43.05, au Extelecom House, kumaanisha jengo la Shirika la Posta lenye ghorofa 14 na urefu wa mita 50.23.
Lakini anga la Dar es Salaam sasa limepambwa na
minara ya maghorofa marefu, yakiongozwa na jengo jipya la PSPF Towers
ambalo urefu wake ni mara tatu ya kimo cha maghorofa yaliyokuwa
yakisifika miaka 20 iliyopita. Jengo hilo lililo mbioni kukamilika lina
urefu wa mita 152.85 likiwa na ghorofa 35.
Maghorofa mengine yaliyochomoza miaka michache
iliyopita ni Uhuru, lenye ghorofa 27, jengo la Kakakuona lenye ghorofa
37, Benjamin Mkapa lenye ghorofa 37.
Mengine ni PSPF Golden Jubilee Towers lenye
ghorofa 24 na urefu wa mita 103.2, jengo la uhuru Heights lenye ghorofa
27 na urefu wa mita 102.6, Umoja wa Vijana lenye ghorofa 26, Viva Tower
lililoko Barabara ya Ali Hassan Mwinyi ambalo lina ghorofa 21 na urefu
wa mita 75.34, BOT Towers lenye ghorofa 20 na urefu wa mita 100 na PPF
Tower lenye ghorofa 16 na urefu wa mita 57.40.
Majengo marefu, ambayo kwa kawaida hupatikana
kwenye miji mikubwa ambako hujengwa kutokana na ukosefu wa ardhi kubwa,
yanatumika kwa ajili ya shughuli za kiofisi, makazi na kibiashara, hasa
hoteli na klabu za usiku.
Lakini majengo hayo yameongezeka kwenye sehemu
ndogo ya katikati ya jiji yakitegemea miundombinu iliyowekwa miaka 150
iliyopita, isipokuwa majengo machache kama Mawasiliano House, Millenium
Towers na Ubungo Plaza yaliyo nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.
Mahitaji ya umeme sasa ni makubwa kuliko wakati
mwingine wowote, hali kadhalika majisafi wakati kuingia katikati ya jiji
nyakati za asubuhi na kutoka jioni ni shughuli kubwa kutokana na
misululu mirefu inayosababishwa na idadi kubwa ya magari yanayobeba
wafanyakazi wanaoenda kwenye ofisi zinazoendelea kuongezeka.
“Master plan (ramani kuu) ya Dar es Salaam iliisha
muda wake miaka 36 iliyopita,” alisema meya wa Halmashauri ya Wilaya ya
Ilala, Jerry Silaa hivi karibuni.
Alisema kukosekana kwa mpango huo, majengo marefu
yanajengwa kiholela katikati ya jiji na kusababisha matatizo mbalimbali
yakiwamo ya mafuriko na foleni kutokana na maji kujaa barabarani wakati
wa mvua.
Silaa alisema baadhi ya sehemu ya zilizokuwa kwa
ajili ya mashamba na makazi holela ya watu, hivi sasa zimegeuzwa viwanja
vya kujenga majengo marefu.
Hata hivyo, alisema kutokana na ongezeko la watu
katikati ya jiji, baadhi ya ofisi zimeanza kuhamishiwa sehemu za kando
ili kukwepa foleni.
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Saidi Meck Sadiki alikiri kuwa
miundombinu iliyopo hailingani na mahitaji ya ongezeko la maghorofa. “Ni kweli kuwa miundombinu yetu ina walakini
wakati maghorofa nayo yakichipuka kila siku,” alisema mkuu wa Sadiki
alipoulizwa na Mwananchi kuhusu kushamiri kwa majengo marefu. “Hata hivyo, ni dalili ya maendeleo ya kiuchumi kwa upande mwingine,” alisema.
Sadik alishauri maghorofa haya kujengwa katika miji mipya au ‘satelite cities’ ili kuepusha msongamano katikati ya Jiji.
Majengo hayo mengi yanamilikiwa na taasisi za
fedha, kampuni za ujenzi na mifuko ya hifadhi ya jamii, matajiri
wakubwa na mashirika mengine. Imeelezwa kuwa kiasi cha Sh800 bilioni
zimewekezwa kwenye miradi mikubwa mitano, ukiwamo wa PSPF Towers.
Maghorofa ni lazima
Mkurugenzi wa kampuni ya maendeleo ya makazi ya
Watumishi Housing, Dk Fred Msemwa alisema ongezeko la maghorofa jijini
halizuiliki kutokana na mahitaji makubwa ya maeneo ya kufanyia biashara
na ofisi. “Kasi ya kuongezeka kwa maghorofa ilitokana na
kuwepo tofauti kubwa kati ya huduma za makazi na mahitaji, hivyo kampuni
nyingi ziliwekeza eneo hilo ili kutoa huduma inayokosekana. Mpaka sasa
bado kuna tofauti ndiyo maana majengo yanaendelea kujengwa na yanajaa
haraka,” alisema.
Ripoti ya Kituo cha Makazi ya Gharama Nafuu (CAHF)
ya 2014 inaeleza kuwapo kwa miradi mingi mikubwa ya ujenzi ambayo
itaongeza wingi ya maghorofa hayo kwa kiwango kikubwa.
Ripoti hiyo inasema Shirika la Nyumba (NHC) pekee
lina miradi lukuki ya ujenzi wa maghorofa na inaeleza kuwa shirika hilo
lina miradi minne na wabia kutoka China ya ujenzi wa majengo pacha
yenye ghorofa 26 yatakayojengwa kwa Sh70 bilioni.
Inaongeza kuwa yapo majengo matatu yenye ghorofa
16 yatakayojengwa kwa gharama ya Sh30.3 bilioni kila moja na Group Six
International na mengine mawili ya ghorofa 16 yanayojengwa na Estim
Construction.
Pia ipo miradi mingine inayoendelea kama jengo la
Kakakuona lenye ghorofa 36 litakalokamilika 2017 na Mzizima Tower
litakalokuwa na ghorofa 33.
Hata hivyo, bado wasiwasi mkubwa ni kasi ya ujenzi huo
kutolingana na kasi ya uboreshaji huduma hizo kwa jamii kama miundombini
mibovu ya majitaka ambayo hufurika muda mfupi tu baada ya mvua kubwa
kunyesha yakiacha takatakla zikizagaa barabarani, wakati ufinyu na
uchache wa barabara hufanya kuwe na misululu mirefu ya magari wakati
wakazi wakiwahi kwenye ofisi zinazoongezeka katikati ya jiji kutokana na
ujenzi wa majengo hayo.
Athari zake
Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa baadhi ya
majengo yanajengwa chini ya kiwango kutokana na ujuzi mdogo, uzembe na
rushwa na watu kadhaa wameshapoteza maisha kutokana na majengo hayo
kuporomoka.
Machi 2013, jengo lililozidishwa urefu kinyume cha
taratibu Mtaa wa Indira Gandhi liliporomoka na kuua watu zaidi ya 30.
Maofisa wa Manispaa ya Ilala, mmiliki na mkandarasi walishtakiwa.
Ukiacha miradi mikubwa, majengo mengi yamejengwa
sehemu zisizo na nafasi ya kutosha na hivyo kutoruhusu kirahisi magari
ya uokoaji.
Mfano mwaka 2013 moto uliposhika ghorofa ya 17 ya
jengo la PPF Tower, ilichukua saa kadhaa kwa Kikosi cha Zimamoto
kukabiliana nao.
Matumizi ya umeme
Hadi kufikia Februari, 2014 Tanesco ilikadiria
kuwa majengo manne tu ya PSPF Twin Tower, Uhuru Height, Viva Tower na
Benjamin Mkapa Tower kwa pamoja yatatumia megawati 12 za umeme, ambazo
ni zaidi ya megawati nane zinazotumika na mkoa mzima wa Mtwara.
Kiasi hicho cha umeme ni sawa na umeme unaotumiwa na mkoa huo na Lindi.
Afisa habari wa Tanesco, Adrian Severin alisema
kuwa idadi ya maghorofa haijawa kubwa kiasi cha kuzidi kiwango cha
mwisho cha ugavi, lakini akaongeza “tuna hofu tutazidiwa siyo muda refu
ndiyo maana tunakamilisha ujenzi wa substation ya zaidi ya megawati 100
kuongeza nguvu kwa iliyokuwepo Barabara ya Sokoine”.
Ofisa Uhusiano wa Shirika la Majisafi na Majitaka
Dar es Salaam (Dawasco), Everlasting Lyaro alisema baadhi ya majengo
katikati ya jiji yalijengwa kwa ajili ya makazi ya watu nane, lakini
yamebadilishwa kuwa ya biashara hivyo kutumiwa na zaidi ya watu 500 huku
mfumo wa maji taka ukibaki kuwa ule ule wa zamani.
CHANZO: MWANANCHI
CHANZO: MWANANCHI

No comments:
Post a Comment