Social Icons

Pages

Thursday, April 23, 2015

JAJI: WANASIASA KUOMBA FEDHA NI KUVUNJA MAADILI

Kamishna wa Maadili, Jaji mstaafu, Salome Kaganda, amesema moja ya mambo ambayo walikabiliana nayo wakati wa sakata la akaunti ya Tegeta Escrow, ni kwa wanasiasa  kujitetea kwamba  kitendo cha kuomba fedha kwao ni jambo la kawaida, kwani kufanya hivyo wanakiuka maadili ya utumishi wa umma.
Jaji Kaganda alitoa kauli hiyo katika warsha ya wadau ya kujadili rasimu ya mwongozo wa maadili wa viongozi wa umma, iliyofanyika jana jijini Dar es Salaam. Warsha hiyo iliwashirikisha  viongozi na  watumishi wa umma, wawakilishi wa asasi za kiraia na wanasiasa.
Akifafanua, Jaji Kaganda alisema tabia ya ukosefu wa maadili ya umma imekuwa ikijirudiarudia katika maeneo mengi yakiwamo matumizi mabaya ya madaraka, vitendo vya rushwa, kuomba, kushawishi na kupata fedha katika mazingira yasiyo halali,  jambo ambalo liliwapa shida wakati wakishughulikia wahusika wa sakata la Escrow kutokana na wanasiasa wakati wanahojiwa kusema kuwa kwao kuomba fedha ni jambo la kawaida.
“Mwongozo huu pia umetaja vitendo vya ukiukwaji wa maadili ya viongozi wa umma…matumizim mabaya ya madaraka, taarifa za serikali, vitendo vya rushwa, mgongano wa maslahi, kushindwa kutoa tamko la rasilimali na madeni, unyanyasaji wa kijinsia, kuomba, kupokea, kushawishi na kujipatia maslahi ya kifedha yasiyostahili..katika hili tulipata shida sana wakati wa suala la Escrow…wanasiaasa wakisema kwao kuomba fedha ni jambo la kawaida,” alisema jaji Kaganda.
Baadhi ya wanasiasa waliohusika na kashfa ya uchotwaji wa zaidi ya Shilingi bilioni 300 kutoka katika akaunti ya Tegeta Escrow, iliyokuwa Benki Kuu (BoT) na kuhojiwa na sekretarieti hiyo  ni pamoja na aliyekuwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Prof. Anna Tibaijuka; Mbunge wa   Bariadi Magharibi, Andrew Chenge na Mbunge wa  Sengerema, William Ngeleja.
Hata hivyo, Chenge alikataa kuhojiwa na kuweka pingamizi mahakamani. Kufuatia sakata hilo, Ngeleja, aliondolewa katika nafasi ya uenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba, Sheria na Utawala huku Chenge akiondolewa uenyekiti wa Kamati ya Bajeti.
Kadhalika, Profesa Tibaijuka, Chenge na Ngeleja walisimamishwa ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: