Social Icons

Pages

Friday, March 13, 2015

SLAA VS KOVA KWA SAA 6:30


Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa, jana alitinga katika ofisi za Jeshi la Polisi Kanda ya Dar es Salaam na kutumia saa 6:30 kuwasilisha malalamiko na ushahidi wa jinsi mlinzi wake, Khalid Kagenzi, alivyokuwa akiwasiliana na baadhi ya viongozi waandamizi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na maofisa usalama kupanga mikakati ya kutaka kumuua.
Dk. Slaa aliwasilisha ushahidi huo ikiwa ni siku mbili tu baada ya Jeshi la Polisi Kanda ya Kinondoni kumuachia Kagenzi ambaye alikuwa akihojiwa na jeshi hilo kwa takribani siku mbili na baadaye maofisa wa Chadema waliomkamata na kumpeleka polisi kugeuziwa kibao kwa kuwekwa rumande hadi sasa.
Katibu Mkuu huyo aliwasili katika ofisi za Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam saa 3:30 asubuhi akiwa amefuatana na mawakili wawili wa Chadema ambao ni John Mallya na Nyaronyo Kicheere. Dk. Slaa aliwasilisha malalamiko yake ambayo alikuwa ameyaandika kwa maandishi katika kurasa tisa na kufanya mahojiano na Kamanda wa Polisi Kanda ya Dar es Salaam, Suleiman Kova, yaliyodumu kwa takribani saa sita na nusu.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana mara baada ya kumaliza mahojiano, Dk. Slaa, alisema kufika kwake kituoni hapo, kulitokana na wito wa Kamanda Kova. “Chadema tuna ushahidi wa kutosha kuhusiana na njama zote za mauaji hayo, kwa mantiki hiyo basi, sijaitwa polisi kuhojiwa bali kufikisha yale niliyokusudia,” alisema Dk. Slaa.
Alisema malalamiko aliyoyawasilisha ni kitendo cha baadhi ya maofisa Usalama wa Taifa kufanya mawasiliano na Kagenzi  na kutoa siri za mikutano ya ndani za chama hicho na kupanga mikakati ya kutaka kumdhuru. “Mlinzi huyu (Kagenzi), ametumika kama kiungo katika njama za kutoa siri za ndani za chama na kupanga njama za kutaka kuniua, tumewasilisha ushahidi tulioufanyia uchunguzi wa kina,” alisema Dk. Slaa.
Kwa upande wake, Mwanasheria wa Chadema, John Mallya, alisema malalamiko yaliyowasilishwa polisi kupitia Dk. Slaa, yako sahihi, kwani kitendo cha Usalama wa Taifa kufanya uchunguzi ndani ya chama fulani na kuwazuia uhuru wa maamuzi yao, ni kosa kwa mujibu wa sheria.
 
KOVA KUZUNGUMZA LEO
Kova jana hakuwa tayari kuzungumzia kuhusiana na kuhojiwa kwa Dk. Slaa, badala yake alisema atazungumza leo. Jumapili iliyopita, Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema, Mabere Marando, aliviambia vyombo vya habari kuwa Kangezi amekuwa akitumiwa na maofisa 22 wa vyombo vya usalama katika miaka miwili iliyopita kufanya mipango hiyo dhidi ya chama hicho.
Alidai Kangezi amekuwa akitumiwa na maofisa usalama wa vyombo hivyo kupata taarifa nyingi za Chadema na kuwasilishwa CCM. Marando alidai mipango hiyo imegunduliwa na Kitengo cha Usalama wa Chadema kupitia simu za Kangezi na kwamba ililenga kuiumiza Chadema kisiasa. Alidai katika hujuma hizo, Kangezi amekuwa akiwasiliana na mmoja wa vigogo wa ngazi ya taifa wa CCM.
Marando alidai kuanzia Desemba, mwaka jana hadi wiki iliyopita, Kangezi alikuwa amekwishafadhiliwa Sh. milioni saba kwa ajili ya matumizi ya mawasiliano ya simu kufanikisha upatikanaji wa taarifa za Chadema kupitia vikao vyake mbalimbali, ikiwamo Kamati Kuu.
Alidai alipohojiwa na Chama, Kangezi aliwapa kitabu chake cha kutunza kumbukumbu, ambacho kinaonyesha mawasiliano kati yake na baadhi ya maofisa wa vyombo vya usalama, aliowataja kwa majina na namba za simu zao za mikononi. Hadi sasa vijana watatu wa Chadema ambao wanadai kumpiga Kagenzi bado wanashikiliwa na polisi.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: