Social Icons

Pages

Wednesday, March 18, 2015

HOFU YATANDA WADAU KUTOSHIRIKISHWA MUSWADA WA HABARI

Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, Saidi Mtanda.
Muswada wa Sheria ya Kupata Habari wa mwaka 2015, utawasilishwa bungeni Machi 27, mwaka huu, huku wadau wakihofia kuwa kutoshirikishwa kwao kunaweza kusababisha kutungwa sheria za kuathiri sekta ya habari.
Kwa mujibu wa ratiba ya mkutano wa 19 wa Bunge linaloendelea mjini Dodoma, muswada huo na mingine, utasomwa kwa mara ya kwanza na hatua zake zote kwa hati ya dharura. Kwa maana hiyo, muswada huo umeshakamilika na wadau wa habari hawatakuwa na fursa yoyote ya kushirikishwa kuutolea maoni kwa lengo la kuuboresha.
Hata hivyo, kuwasilishwa kwa muswada huo kunaweza kuleta furaha au kiama kwa wadau wa habari hasa kutokana na kwamba wadau hawajashirikishwa katika kuuandaa kama taratibu na sheria zinavyoelekezwa. Kulingana na taratibu, kabla ya muswada huo kuwasilishwa Bungeni, wadau wa habari wanatakiwa kushirikishwa katika mchakato mzima, lakini katika mchakato wa Muswada wa Sheria ya Vyombo vya Habari wa mwaka 2015, serikali haijafanya jitihada za kushirikisha wadau.
Badala yake, muswada huo uliandaliwa na Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo huku wadau wakilalamikia kutoshirikishwa. Wadau wanahofia kwamba kutokana na kutoshirikishwa, muswada huo utawaathiri ikiwamo kutungwa kwa sheria inayoweza kuwaathiri wanahabari ikiwamo kuweka vigezo vya sifa kwa wanataaluma hiyo.
Vile vile, wanahofia kwamba inaweza kutungwa sheria ya kuminya uhuru wa vyombo vya habari. Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, Saidi Mtanda, alinukuliwa na baadhi ya vyombo vya habari akisema kuwa muswada huo ni moja kati ya kilio cha wadau wa habari nchini ambao unatarajiwa kuikomboa taaluma hiyo kwa kusimamia masuala yote yanayohusu taaluma hiyo muhimu duniani.
 
TEF: SERIKALI INA AJENDA YA SIRI
Akizungumza na NIPASHE jana, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda, alisema kuwasilishwa kwa hati ya dharura muswada huo inaonekana dhahiri serikali ina ajenda ya siri isiyovitakia mema vyombo vya habari nchini.
“Inaonekana dhahiri serikali ina ajenda za siri imezificha, muswada kuwasilishwa kwa hati ya dharura hakuzingatii misingi ya haki na demokrasia,” alisema Kibanda. Kibanda alihoji sababu za muswada huo kutoletwa kwa wadau huku akisisitiza ni vyema ungeletwa kwa wadau wausome ili wautolee maoni sahihi.
Aidha, alisema kwa mtindo huo ni wazi serikali inataka kuendelea kuvinyima uhuru vyombo vya habari na wananchi haki ya kupata habari.
 
MCT: HARAKA YA NINI?
Katibu Mkuu wa Baraza la Habari Tanzania (MCT), Kajubi Mukajanga, alihoji kwa nini muswada huo uharakishwe kuwasilishwa bila kukusanya maoni ya wadau, kitu ambacho ni kuwanyima nafasi ya kuusoma na kutoa maoni yao.
Mukajanga alisema kwa utaratibu wa utungaji wa sheria, muswada huo unatakiwa uchapishwe katika Gazeti la Serikali kwa siku 21 ili kutoa nafasi kwa wadau na wananchi kuusoma, hivyo kama haukuchapishwa matakwa ya msingi yanawekwa pembeni. Aliongeza kuwa, kufanya hivyo ni jambo linaloogopesha na kuhoji: “Kwa nini kunakuwapo na usiri katika jambo hili na kulipeleka kwa haraka bila kushirikisha wadau?”
Alisisitiza kuwa MCT bado inaendelea na juhudi za kuwasiliana na Mawaziri husika ili kuhakikisha wanapata nakala za muswada huo. Kajubi alisema walijitahidi kukutana na Mawaziri bila mafanikio huku akisisitiza kuwa wataendelea na jitihada za kupata nakala.
Alifafanua kuwa ingekuwa vyema kama wadau wangeshirikishwa kwa ukamilifu kwa ajili ya kupitisha muswada wenye mashiko kwa vyombo vya habari na sekta ya habari kwa ujumla.
 
CHANZO: NIPASHE

No comments: